martes, 19 de julio de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 16 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 16 YA MWAKA-C
Somo: Yer 2:1-3, 7-8, 12-13
Zab: 36:6-7ab, 8-9, 10-11
Injili: Mt 13:10-17
Nukuu:
Enenda ukalie masikioni mwa Yerusalemu, ukisema, Bwana asema hivi, Nakukumbuka, hisani ya ujana wako, upendo wa wakati wa uposo wako; Jinsi ulivyonifuata huko jangwani, katika nchi isiyopandwa mbegu,” Yer 2:2 

Israeli walikuwa utakatifu kwa Bwana; malimbuko ya uzao wake; Wote watakaomla watakuwa na hatia; uovu utawajilia; asema Bwana,” Yer 2:3 

 “Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. Kwa sababu hii nasema nao kwa mifano; kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa,” Mt 13:11, 13 

 “Lakini, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia,” Mt 13:16 
Kwa maana, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie,” Mt 13:17 

TAFAKARI: Enyi mbingu, staajabuni kwa ajili ya jambo hili, mkaogope sana, na kuwa ukiwa sana, asema Bwana.”

Wapendwa wana wa Mungu, hakika yapo mambo ya ajabu sana katika jamii yetu leo ambayo twahitaji ujasiri wa ndani na imani kuyasema, kuyakemea, na kusema iliyo kweli kadiri ya mapenzi ya Mungu. Nabii Yeremia anaitwa kwenye jamii ambayo haikuwa tena na hofu ya Mungu. Hata wale ambao waliujua ukweli kuhusu matakwa ya Mungu waliingiwa upofu na kufuata mkondo wa ‘upepo uovu’ kama ulivyokuwa. Haikuwa ajabu kuwaona makuhani kusimama na kuwatetea watawala hata pale walipokwenda kinyume na mapenzi ya Mungu katika ubovu na uovu wao. Makuhani hawa waliyafanya hayo kwa kuwapendezesha watawala ili kukidhi mahitaji yao binafsi. Ni katika mazingira haya Mungu anamwinua Nabii wake Yeremia na kusema ujumbe wa Mungu na matakwa yake.

Wapendwa wana wa Mungu, maisha yako katika ulimwengu huu licha ya kwamba kuwa siyo ya bahati mbaya, yanamaanisha kwa kiasi kikubwa kwa wakili wa Mungu katika utume maalumu pale ulipo. Pamoja na mambo yote mazuri ambayo waweza kufanya, mimi na wewe kama wana wa Mungu, na wafuasi wake Kristo, kila siku tunaitwa kupambana na aina yoyote ile ya uovu na yenye kufifisha uwepo wa Mungu pale ulipo. Na hivi ndivyo Nabii Yeremia anatumwa na kuwajibika katika vita hii ya kweli dhidi ya uovu, kwamba, Enenda ukalie masikioni mwa Yerusalemu, ukisema, Bwana asema hivi, Nakukumbuka, hisani ya ujana wako, upendo wa wakati wa uposo wako; Jinsi ulivyonifuata huko jangwani, katika nchi isiyopandwa mbegu,” Yer 2:2. Kwanza kabisa Mungu anataka watu wake waelewe nafasi yake na yao ikiwa ni pamoja na yale yote aliyowatendea. Israeli walikuwa utakatifu kwa Bwana; malimbuko ya uzao wake; Wote watakaomla watakuwa na hatia; uovu utawajilia; asema Bwana,” Yer 2:3. Bila utakatifu hakuna uwezekano wa kuwa rafiki na Mungu, kwa sababu asili ya Mungu ni Takatifu na Utakatifu wenyewe. Mungu wetu ni Mtakatifu!

 Pili, Mungu anatoa angalizo la kuuacha uovu huo ambao unaweka tengano kati yake na wao-‘watu wake.’ Naye Mungu anawakumbusha, na anatukumbusha pia leo kwamba, Nami nikawatia katika nchi ya shibe, mpate kula matunda yake na mema yake; lakini ninyi mlipoingia katika nchi ile, mliitia unajisi nchi yangu, na urithi wangu mliufanya kuwa chukizo,” Yer 2:7. Mungu aliye huruma, hapendi watu wake waangamie katika ujinga na upumbavu wao. Kwa maana “Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma, si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema,” Zab 145:8. Kumbe ni jambo la busara kujirudi pale unatambua kwenda kinyume na mapenzi ya Mungu.

Tatu, hata kama mwanadamu ataenenda katika njia yake hatoweza kushinda vita hiyo bila uwepo wa Mungu. Katika hili Mungu anawaambia wana wa Israeli, na sisi pia kwamba,Nami nikawatia katika nchi ya shibe, mpate kula matunda yake na mema yake; lakini ninyi mlipoingia katika nchi ile, mliitia unajisi nchi yangu, na urithi wangu mliufanya kuwa chukizo,” Yer 2:7. Ndugu yangu na Mtanzania mwenzangu, hakuna aliyejichagua kuzaliwa katika Taifa hili. Ni maajabu yake Mungu wakati ulipotimia na alipoona inafaa, akafanya kile ambacho leo ndicho ulicho ikiwa ni utaifa wako kama Mtanzania. Hata kwa kutokuchagua kwako kuwa kile tulicho leo, ikiwa ni pamoja na kuzaliwa kwako na utaifa wako leo kama Mtanzania, haikuondolei kutokuwajibika kwa kile Mungu alichokukirimia bure, ikiwa ni pamoja na rasilimali za Taifa hili. Leo kila mwenye nguvu na nafasi bila kujali umma uliompa nguvu hizo, tumekuwa chukizo mbele ya macho ya Mungu kwa kutapanya urithi tuliopewa bure ikiwa si kwa kizazi hiki tu, bali kwa vizazi vyote. Watu hawa wanaishi kama vile kesho haipo, na leo ndiyo mwisho wa kila kitu. Hivyo wajibu wao wa kwanza ni kujinufaisha wenyewe na familia zao, huku kundi kubwa la watu maisha yakiwa heri ya jana.

Jambo lingine la ajabu nyakati zile za Nabii Yeremia lilikuwa kwamba hata wale ambao kwa uhakika walijua matakwa ya Mungu, na hivyo kuwa sauti ya wasio na sauti, waliingiwa upofu na mwisho wa siku waliyapigania matumbo yao na katika ubinafsi wao. Makuhani hawakusema, Yuko wapi Bwana? Wala wana-sheria hawakunijua; wachungaji nao waliniasi, nao manabii walitoa unabii kwa Baali, wakafuata mambo yasiyofaidia kitu,” Yer 2:8. Je! leo ni jambo la ajabu ‘kuibuka manabii wa kujitengeneza mwenyewe’ na kutoa sifa kemkem juu ya udhalimu, utawala dhalimu, na wala rushwa na mafisadi? Leo wako wapi ‘wana-sheria’? Leo wapo wapi wachungaji wenye hofu ya Mungu wenye kuona kweli kama ilivyo, na sivyo kama walivyo? Leo wapo wapi wasemaji wa wasio na sauti? Hakika sote tunaangamia kwa upofu wakujitakia na kwa kuliheshimu tumbo kuliko kweli ya Mungu. Na hiki ndicho kilio cha Mungu kwetu leo, kwamba, Enyi mbingu, staajabuni kwa ajili ya jambo hili, mkaogope sana, na kuwa ukiwa sana, asema Bwana,” Yer 2:12. Ndugu yangu, inawezekana kabisa kutoka katika hadha hii ikiwa wewe uliye mwananchi mwema na mwenye hofu ya Mungu ukajua wajibu wako msingi katika Taifa hili na kufanya sehemu yako kikamilifu. La sivyo Taifa linaangamia licha ya kuzisadifu mbwembwe za hapa na pale. Hivyo, Wewe uliye mwana sheria, simama katika kweli na haki, na kwa kufanya hivyo ‘kweli na haki’ ya Mungu itaonekana kwa watu wake na Taifa lake. Wewe uliye mchungaji, simama vizuri hapa ulipo, lisimamie vyema kundi ulilopewa, jua wajibu wako wa kusimama katika kweli, haki, huruma, msamaha, na upendo wa Mungu. Mara zote usukumwe na kiu ya kweli na haki ya Mungu kwa neno lile ulisomalo kila siku na kulitafakari, na siyo upofu wa tumbo na hitaji binafsi ambalo mwisho wa siku ni kihama kitupu.

Na kama ilivyokuwa enzi za Nabii Yeremia, hata leo uovu huja vaa suti mpya na kubadili madhari yake kama asemavyo Mungu, kwamba, Kwa maana watu wangu hawa wametenda maovu mawili; wameniacha mimi, niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavujayo, yasiyoweza kuweka maji,” Yer 2:13. Ndugu yangu, hakuna uhai bila Mungu, hakuna njia bila Mungu, na hakuna kweli bila Mungu. Yesu anasema,  “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Je, njia zako za panya zitakufikisha kwa Mungu? Kweli yako ya kughushi ghushi itaifunua kweli ya Mungu ndani yako? Na uzima wako wa kuzikanyaga haki za watu, na kudhulumu haki za watu una umilele ndani yake? TAFAKARI!

Wapendwa wana wa Mungu, yote tuliyoyaona hapo juu, yanasemwa kwa ufupi wa maneno machache kutoka Injili ya leo; Kwa maana ye yote mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini ye yote asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang'anywa,” Mt 13:12. Ndugu yangu, elewa kweli hii kwamba, wewe leo katika ulimwengu huu haupo hapa kwa bahati mbaya. Upo hapa kuwa wakili wa kweli wa Mungu katika wito na utume ule uliokirimiwa na Mungu mwenyewe kadiri ya hali na nafasi yako. Kwa maana nyingine, usipolifanya jambo hili ilhali Mungu kakupa uwezo huo bure, ni sawa na mfano ule wa chumvi. Naye Yesu anasema, “Chumvi ni njema; lakini chumvi ikiwa si chumvi tena, mtaitia nini ikolee? Mwe na chumvi ndani yenu, mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi,” Mk 9:50. Ni kweli kwamba mimi na wewe kama chumvi lazima tuthibitishe hilo. La sivyo hakuna sababu ya kuendelea kuwa kama tulivyo. Naye Yesu anasema, “ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13. Na hiki ndicho kihama katika ujumbe wa Injili ya leo, na ndiyo maana ya maneno hayo ya Yesu kwamba,  ‘mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini ye yote asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang'anywa.’ Mt 13:12.

Ni kweli isiyo shaka kwamba kwa uwezekano wa kuwa wana wa Mungu kwa sadaka ile ya Yesu pale msalabani, na kwa kuzaliwa upya kwa Sakramenti ya Ubatizo kama ishara ya wazi ya kufa pamoja na Kristo na kufufuka pamoja naye, mimi na wewe tumefunuliwa siri za ufalme wa mbinguni. Hivyo mifano anayoitumia Yesu yatupasa kutufikirisha juu ya siri hiyo kwa sababu hatma yetu ni maisha ya milele. Hivyo, Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. Kwa sababu hii nasema nao kwa mifano; kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa,” Mt 13:11, 13. Ni heshima kubwa sana kuwa wana wa Mungu na warithi wa ufalme wake. Na huku ndiko kule kuhesabiwa haki. 

Wapendwa wana wa Mungu, mambo haya niyasemayo leo siyo mageni masikioni mwenu. Ila hili ni dhahiri kama wasemavyo waswahili, ‘sikio la kufa halisikii dawa.” Ni wajibu wa kila kwenye hofu ya Mungu kuusema ukweli, kuutetea ukweli, na kusimama katika kweli na haki hata kama kwa kufanya hivyo kutakugharimu maisha yako. Ndugu yangu, Yesu katika hili anahoji nafsi yako na yangu kwa kuuliza, “itamfaidi mtu nin kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake. Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake?” Mk 8:36-37. Nisipo kuwa tayari kupokea kweli hii leo, unabii wa Isaya kama asemavyo Yesu ni dhahiri kwetu leo pia, kwamba, Neno likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; Kutazama mtatazama, wala hamtaona,” Mt 13:14. Huku ni kuukubali upofu kwa kuitanguliza nafsi na maslahi binafsi. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, Na kwa masikio yao hawasikii vema, Na macho yao wameyafumba; Wasije wakaona kwa macho yao, Wakasikia kwa masikio yao, Wakaelewa kwa mioyo yao, Wakaongoka, nikawaponya,” Mt 13:15. Je, katika hali na mazingira kama haya, twaweza kuushinda uovu ilhali tunauatamia?

Ndugu yangu, hakuna lisilowezekana kwa Mungu kama kila mmoja wetu atajua sababu ya kuumbwa kwake kama tunavyojifunza kutoka kwenye Katekisimu yetu Katoliki, kwamba, ‘tumeumbwa ili tumjue Mungu, tumpende, tumtumikie, na mwisho turudi kwake Mbinguni.’ Wenye kufanya haya watakuwa katika mikono salama ya Mungu kwa sababu wapo tayari ‘kuona kwa macho yao, na kusikia kwa masikio yao.’ Hawa ni wale wanye hofu ya Mungu. Na hawa ndio Yesu anaosema kwamba, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia,” Mt 13:16. Hawa wenye uwezo huu wa ‘kuona kwa vile wana macho yenye uwezo huo, na kusikia kwa sababu wana masikio yenye uwezo huo wa kusikia, ni zaidi ya manabii. Katika kweli hii Yesu anatuambia, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie,” Mt 13:17. Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, je, wahitaji malaika washuke kutoka mbinguni na kusema ili uelewe?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia,” Mt 13:16


Tusali:-Ee Yesu, nikumbushe kila siku sababu ya kuumbwa kwangu, na niwe mwaminifu kwa hilo daima. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario