domingo, 24 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 17 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI  YA 17 YA MWAKA-C
Somo: Yer 14:17-22
Zab: 79:8, 9, 11, 13
Injili: Mt 13:36-43
Nukuu:
 “Nikitoka kwenda shambani, tazama, wako huko waliouawa kwa upanga! Na nikiingia mjini, tazama, wamo humo wanaougua kwa sababu ya njaa! Maana nabii na kuhani, wote wawili, huenda huko na huko katika nchi, wala hawana maarifa,” Yer 14:18 

Je! Umemkataa Yuda kabisa? Roho yako imeichukia Sayuni? Mbona umetupiga, tusiwe na dawa ya kutuponya? Tulitazamia amani, lakini hayakuja mema yo yote, tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu!” Yer 14:19 

Ee Bwana, tunakiri uovu wetu, na ubaya wa baba zetu; maana tumekutenda dhambi,” Yer 14:20 

 “Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia,” Mt 13:40

Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika ufalme wake machukizo yote, na hao watendao maasi, na kuwatupa katika tanuru ya moto, ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno,” Mt 13:41

TAFAKARI:Ee Bwana, tunakiri uovu wetu, na ubaya wa baba zetu; maana tumekutenda dhambi.”
Wapendwa wana wa Mungu, pasipo na amani hakuna chochote kile ambacho mimi na wewe twaweza kukifanya kwa utulivu. Pasipo amani hakuna matumaini. Na kama hakuna matumaini ni vigumu kuwashawishi watu juu ya kile utakacho waelewe hata kama dhamiri yako ni safi na njema. Pamoja na hali hiyo, Mungu anamtuma Nabii Yeremia kulisema hili ambalo Yeye, Mungu amekwisha liona. Nawe utawaambia neno hili, Macho yangu na yatiririke machozi, usiku na mchana, wala yasikome; kwa maana bikira, binti ya watu wangu, amevunjika mavunjiko makuu, kwa jeraha isiyoponyeka,” Yer 14:17. Lililo la kweli lisemwe kama lilivyo ili kuleta uponyaji, na kufungua milango ya kukabiliana nayo. Ni ajabu sana, na hasa kwenye jamii yetu leo, wengi wetu wamefikia hatua ya kuubatiza uongo na kuwa “kweli au utakatifu buniwa.” Je, tunayafanya haya kwa faida ya nani kama siyo kujichimbia kaburi?

Kwa nini hatupendi kusema kweli na badala yake twapamba lililo ovu? Kwa nini tunashindwa kusema na kuona iliyo kweli kama afanyavyo Nabii Yeremia? Nabii Yeremia anaona iliyo kweli na kusema, Nikitoka kwenda shambani, tazama, wako huko waliouawa kwa upanga! Na nikiingia mjini, tazama, wamo humo wanaougua kwa sababu ya njaa! Maana nabii na kuhani, wote wawili, huenda huko na huko katika nchi, wala hawana maarifa,” Yer 14:18. Badala yake, leo waliopewa dhamana na umma wamejiridhisha na kujisahau. Wimbo wao kila siku ni ule wa kurembesha iliyo ovu na kusema “yote yapo salama, hakuna haja ya kuwa na hofu.” Kama hakuna hofu kwa nini watu hawana furaha? Kwa nini kila kukicha ni kilio? Kwa nini watu wanapigwa butwaa muda wote?

Kukosa matumaini katika maisha, ni kifo halisi cha maisha. Maisha hukosa mvuto na mwelekeo. Katika mazingira ya mtindo huu, mwanadamu huzika rasmi uwezo wake katika ubunifu. Mtu ubaki kuwa kama tenga tupu! Na hii ndiyo hali iliyowafika wana wa Israeli katika ya ‘toweko’ la lile tumaini na kusema, Je! Umemkataa Yuda kabisa? Roho yako imeichukia Sayuni? Mbona umetupiga, tusiwe na dawa ya kutuponya? Tulitazamia amani, lakini hayakuja mema yo yote, tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu!” Yer 14:19. Jamii yoyote ile inapofikia hatua ya kufanya ‘maamuzi mazito juu ya mstkabali wa maisha yao,’ na mambo kwenda ndivyo sivyo, matokeo yake ndiyo wingi wa maswali haya yasiyo na majibu na wakujibu, na mwisho wa siku jamii husika kukosa mwelekeo. 

Hata hivyo hakuna jambo lolote lisilo kuwa na chanzo chake. Ni kweli pasipo shaka kwamba wakati fulani, na watu fulani, hawakufanya yastahiliyo kweli na haki. Na kuanzia hapo tatizo hilo lawezekana kukuzwa na kuendelezwa kama utamaduni fulani usio na kweli ndani yake. Hakika kwa ung’ang’anizi huu wa mila na desturi hizi, wachache huneemeka nazo ilhali kundi kubwa la watu uteseka na kulipa gharama za wachache, ‘akina mangi meza.’ Uponyaji wa dhambi hii ya kijamii, yaani “social sin,” ni kujirudi tu. Na hivi ndivyo Nabii Yeremia anavyotambua chanzo cha uovu wote na kusema, Ee Bwana, tunakiri uovu wetu, na ubaya wa baba zetu; maana tumekutenda dhambi,” Yer 14:20. Ukiri wa kweli ni tiba ya kweli na mwanzo mpya wa kulitatua tatizo.

Je, ni wangapi walio tayari kuzivua tai zao na kuvaa mavazi ya kawaida na kuonekana wa kawaida mbele ya jamii iliyowakuza na kuwa mamangi meza? Wengi wa watu hawa hukubali kufa na tai zao shingoni, yaani uovu wao. Lakini bila kujisalimisha hakuna usalama. Ifike mahali tukiri na kusema,  Usituchukie, kwa ajili ya jina lako; usikifedheheshe kiti cha enzi cha utukufu wako, kumbuka, usilivunje agano ulilofanya nasi,” Yer 14:21. Hivi Mungu akivunja agano lake, yaani, ‘kuto kuurithi ufalme wa mbinguni,’ umaana wa maisha yako ya kujibohofisha kwa anasa na starehe yana nafasi na faida gani? 

Kumbe ni vyema nikafahamu njia zangu, na uhalisia wa ufalme wa Mungu. Na hivi ndivyo Yesu anavyofafanua mfano ule wa magugu na ngano kuota pamoja. Naye anasema, Azipandaye zile mbegu njema ni Mwana wa Adamu,” Mt 13:37. Mbegu hizi ni wana wa ufalme wa Mungu, kwa kupitia Yesu Kristo kwa kifo kile cha Msalaba tulichohesabiwa haki. Magugu ni wana wa yule mwovu shetani mwenye kwenda kinyume cha lolote lile jema katika kweli na haki. Hivyo, lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu,” Mt 13:38. Wana wa hawa mwovu hawawezi kuyafanya hayo bila kusukumwa na roho ovu ndani yao. Na msukumo huu ni kuridhia hali hiyo. Shetani hawezi kufanya chochote bila maridhiano nawe. Kwa maana hiyo, yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi; mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wavunao ni malaika,” Mt 13:39. Kumbe si vyema kumsingizia shetani tu na kuitoa nafsi yetu iliyoshiriki moja kwa moja au kwa sehemu katika kweli hiyo.

Hata hivyo, pamoja na huruma na upendo wa Mungu kuwa mkubwa kuliko dhambi zetu, na mwisho wa siku tukashindwa kuuridhia upendo na huruma hiyo, kifuatacho ni hukumu ya kweli na haki. Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia,” Mt 13:40. Kumbe hukumu ya mwisho ni hakikisho la haki tu, yaani, ‘justification’ kwa yale yote tuliyoyatenda ambayo kwayo ndiyo kweli ipasayo hukumu. Neno aliyefanyika mwili na kukaa kwetu, ndiye mwenye kuyaratibisha yote hayo siku ile ya mwisho kwa sababu kwa kumwilishwa kwake kumempa fursa kubwa ya kuujua ubinadamu wetu katika wema na mabaya. Na hivi ndivyo itakavyo kuwa, yaani, Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika ufalme wake machukizo yote, na hao watendao maasi, na kuwatupa katika tanuru ya moto, ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno,” Mt 13:41-42. Ndugu yangu, utalikwepa fekeo hili?

Tumsifu Yesu Kristo!

Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia,” Mt 13:40


Tusali:- Ee Yesu na Mkombozi wetu, tujalie nguvu ya kuushinda uovu kwa wema nasi kuwa watu wema. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario