JUMATATU
WIKI YA 14 YA MWAKA-C
Somo: Hos 2:14, 15-16, 19-20
Zab: 145:2-3 4-5, 6-7, 8-9
Injili: Mt 9:18-26
Nukuu:
“Nami
nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu, na
kwa ufadhili, na kwa rehema,” Hos 2:19
“Nami
nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua Bwana,” Hos 2:20
“Alipokuwa
akiwaambia hayo, tazama, akaja jumbe mmoja, akamsujudia, akisema, Binti yangu
sasa hivi amekufa; lakini njoo, uweke mkono wako juu yake, naye ataishi,” Mt
9:18
“Yesu akageuka,
akamwona, akamwambia, Jipe moyo mkuu, binti yangu; imani yako imekuponya. Yule
mwanamke akapona tangu saa ile,” Mt 9:22
TAFAKARI: “Njoo uweke mkono juu yake, naye ataishi.”
Wapendwa wana wa Mungu, wakati
nyakati zilipotimia Mungu aliyekuwa mbali sana katika uelekezaji na utendaji
alikuwa Emmanueli yaani, Mungu pamoja nasi (Yoh 1:14, Ebr 1:1-2, Gak 4:4-5).
Ukaribu wa ‘Mungu nasi’ ambaye ndiye Yesu Kristo, ni hakikisho la uzima ndani
yetu. Mungu wetu ni hai muda wote. Uwepo wa Neno aliyefanyika mwili ni uhai
katika miili yetu hii inayokufa. Na hivyo, “Alipokuwa
akiwaambia hayo, tazama, akaja jumbe mmoja, akamsujudia, akisema, Binti yangu
sasa hivi amekufa; lakini njoo, uweke mkono wako juu yake, naye ataishi,” Mt
9:18. Uhai ndani na katika Kristo unaonekana kwa wote wale waliomridhia. Kristo
ndiye kimbilio letu na uhai wetu. “Na
tazama, mwanamke aliyekuwa na ugonjwa wa kutoka damu muda wa miaka kumi na
miwili, alikuja kwa nyuma, akaugusa upindo wa vazi lake,” Mt 9:20. Mwanamke
huyu anaona uhai ndani na katika Kristo. Analishika pindo la vazi la Yesu kwa
imani na anapona. Naye Yesu anamwambia, “Jipe moyo mkuu, binti yangu; imani
yako imekuponya. Yule mwanamke akapona tangu saa ile,” Mt 9:22. Je, unaimani
thabiti na Yesu Kristo, Bwana na mwokozi wa Maisha yako? Na katika hali ya kufa
unashika wapi na nani?
Wapendwa katika Kristo,
Bwana wetu Yesu Kristo akiwa njiani kufanya uponyaji, anakutana na taarifa za
kuhuzunisha kwamba uhai ule anaoukimbilia haupo tena. Kwa vile yeye ni Bwana wa
Uhai na amekuja kwa sababu hiyo ya uhai tena tuwe nao wa kutosha, anasema,
“Ondokeni; kwa maana kijana hakufa, amelala tu,” Mt 9:24. Kifo ni usingizi tu.
Wote wenye kumridhia Mungu wataamshwa kutoka uzingizi wao siku ya mwisho. Je,
bado umelala? Amka na mfuate Kristo.
Maisha mapya na yenye
matumaini ya kweli twayapata pale tunapokuwa na uhusiano mzuri na Muumba wetu.
Fundisho hili ndilo alitoalo Nabii Hosea kwa wana wa Israeli waliokwisha kukata
tamaa. Mungu yupo tayari kuanza nasi upya na kusahau historia yetu mbaya, Lk
15:11-32. Agano hili jipya na Mungu lategemea utayari wako. Ukiwa tayari Mungu
anasema haya juu yako kama alivyowaambia wana wa Israeli, “Nami
nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu, na
kwa ufadhili, na kwa rehema,” Hos 2:19. Tendo hili limebebwa katika misingi ya
pendo, kweli, haki (ambayo huenda na hukumu), na huruma ya Mungu.
Posa hii yenye
kuonyesha upendo wa ndani kati ya mposa-Mungu, na mposwa-mimi na wewe, hudumu
katika uaminifu wa kweli. Kumbe yanipasa kuwa kile nilicho kwa nyakati zote na
wakati huo nikiutazama ule wokovu kama alama ya mabadiliko yangu ya ndani,
yaani, maisha yangu ya kiroho. Mahusiano
haya ndiyo sababu na uwezekano wa kumjua Mungu.
Naye Mungu anasema, “Nami
nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua Bwana,” Hos 2:20. Haya yote yamekamilika
ndani na katika Kristo Yesu. Je, maisha yako yamefungamanishwa na upendo wa
Kristo ndani yako?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Jipe moyo mkuu, binti yangu; imani
yako imekuponya,” Mt 9:22a
Tusali:-Ee
Yesu Kristo nakuamini. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario