IJUMAA
WIKI YA 16 YA MWAKA-C
Somo: Yer 3:14-17
Zab: Yer 31:10, 11-12ab, 13
Injili: Mt 13:18-23
Nukuu:
“Rudini,
enyi watoto wenye kuasi, asema Bwana,” Yer 3:14a
“nami
nitawapa ninyi wachungaji wanipendezao moyo wangu, watakaowalisha kwa maarifa
na fahamu,” Yer 3:15
“Naye aliyepandwa
penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye
ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini,” Mt 13:23
TAFAKARI: “Bwana asema, Rudini, enyi watoto
wenye kuasi.”
Wapendwa wana wa Mungu, ujumbe wa Mungu mara
zote, nyakati zote, na kwa namna moja au nyingine, ujumbe huo uelezea upendo na
huruma yake. Hivyo kazi kubwa ipo upande wako na wangu kuridhia upendo na
huruma hii ya Mungu. Ni upendo na huruma yake Mungu anasema, “sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na
kuiacha njia yake mbaya, akaishi,” Eze 33:11. Ni kwa huruma na upendo wa ajabu aliokuwa nao Mungu
kwetu kwamba ‘neema na huruma yake ni kubwa kuliko dhambi zetu.’ Na hiki ndicho
Mungu kwa upendo na huruma yake anacho kidhihirisha kwetu kwa kusema, “Dhambi
zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa
nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu,” Isa 1:18. Mungu hakuacha kamwe na
hataacha daima kutupenda na kutuhurumia pale tunapokuwa tayari kwa kufanya toba
ya kweli na majuto ya dhambi zetu na kuridhia upendo na huruma yake. Kama
watoto wake, Mungu kwa kupitia kinywa cha Mtumishi wake Nabii Yeremia
anatuambia, “Rudini, enyi watoto wenye kuasi,” Yer 3:14a. Kumuasi
Mungu hakuna heri wala usalama.
Tunapomrudia Mungu kwa wema na unyenyekevu hatoshindwa
kuijenga tena nyumba yake iliyobomoka, yaani, Taifa lake, kama tokeo la dhambi.
Naye anasema, “nami nitawapa ninyi
wachungaji wanipendezao moyo wangu, watakaowalisha kwa maarifa na fahamu,” Yer
3:15. Huyu ndiye Mungu aliye Upendo na Huruma, “amejaa huruma na neema, haoni
hasira upesi, ni mwingi wa fadhili,” Zab103:8. Ni Mungu mwenye kutimiza ahadi
zake na mwenye kumtakia kila mmoja heri na neema kwa sababu ndani ya kila mmoja
kuna chapa yake, Mwa 1:27. Na kwa ahadi zake Mungu anasema, “Wakati
ule watauita Yerusalemu kiti cha enzi cha Bwana; na mataifa yote watakusanyika
huko Yerusalemu, kwa ajili ya jina la Bwana; wala hawatakwenda tena kwa ukaidi
wa moyo wao mbaya,” Yer 3:17. Hakika hakuna lisilowezekana kwa Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu, Injili ya leo inatoa ufafanuzi wa
habari ile ya Mpanzi. Leo Yesu anafafanua lugha ile ya picha aliyoitumia kadiri
ya mazingira na watu wake. Lengo la lugha ile ya picha kuhusu Mpanza, ni
kuelezea kweli hiyo ya Mungu ndani ya mioyo yetu. Hivyo alichokifanya Mpanzi ilikuwa ni namna neno la Mungu
lifanyavyo kazi ndani ya mioyo yetu na kutubadilisha. Ili neno la Mungu liwe
tumaini la kweli, kama tulivyokwisha kuona siku mbili zilizopita, na ushuhuda
wa kweli ndani yetu, na kwa wale wanaotuzunguka, lazima neno hilo tulisikie,
tulipokee, kulitafakari, kulishirikishe, na mwisho tuwe sehemu ya neno hilo kwa
kuwa mashahidi wa neno hata ikibidi kufa kwa kweli hiyo. Kulipokea neno lazima
uwe na utayari wa kulisikia neno. Usipokuwa na utayari huu ni sawa na “mbegu
nyingine zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila,” Mt 13:4. Na huu
ndio ufafanuzi wa Yesu; “Kila mtu
alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua
lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia,” Mt 13:19
Kulitafakari neno la
Mungu kunakuhitaji kulisikia neno hilo na liguse maisha yako. Kutafakari neno
ni kama kucheua kile ulichokula. Kama hili halikufanyika ni sawa na mbegu zile “zilizoanguka
penye miamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara zikaota, kwa udongo kukosa
kina, na jua lilipozuka ziliungua; na kwa kuwa hazina mizizi zikanyauka,” Mt
13:5-6. Na hapa Yesu anatuambia kwa kuifafanue lugha ile ya picha, kwamba, “Naye aliyepandwa penye miamba, huyo ndiye
alisikiaye lile neno, akalipokea mara kwa furaha; lakini hana mizizi ndani yake, bali
hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara
huchukizwa,” Mt 13:20-21. Kulipokea neno kwa furaha na kukosa mizizi ndani
yake, ni kukosa tafakari ya kina juu ya kile ulichokisikia au kukisoma. Ni
kutokulicheua neno, na hivyo neno hilo kutokuwa sehemu ya maisha yako, na
kutokukupa uwezekano wa kulishirikisha kwa wengine. Huwezi kutoa usichokuwa
nacho. Je, itawezekana kweli kushirikisha kwa wengine kile usichokuwa nacho?
Wapendwa wana wa Mungu,
kuwa na uwezo wa kulishirikisha neno la Mungu kunategemea sana namna
tunavyolicheua neno la Mungu, yaani, uwezo ule wa kulitafakari neno la Mungu na
kuleta mabadiliko kwanza ndani yetu. Tunaposhindwa kufanya hivyo ni sawa na
mbegu “zilizoanguka
penye miiba; ile miiba ikamea, ikazisonga,” Mt 13:7. Kumbe tunaweza
kushirikishana neno la Mungu vizuri pale tunapokuwa na mazingira mazuri ya
kulitafakari neno la Mungu kama lilivyo, na siyo tulivyo kwa kujionea huruma.
Na hapa Yesu anafafanua lughu hii ya picha na kusema, “Naye
aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na shughuli za dunia,
na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai,” Mt 13:22. Leo ni wangapi tu sehemu ya Jumuiya ndogo ndogo
iliyopo kwenye eneno lako, ikiwa ni pamoja na kwenda kwenye jumuiya hiyo na
kuwa sehemu ya familia hiyo, ukiumega mkate na kushirikishana neno la Mungu?
Leo jumuiya hizi sehemu nyingi zimekuwa kundi la watoto, akina mama, tena
wajane, na wazee. Hakuna vijana, na wala hakuna akina Baba. Je, hayo malimwengu
unayoyakubatia yana uzima ndani yake au umebaki kujifariji katika upumbavu? Tukifanikiwa
katika hatua hii, yaani, kuliishi neno la Mungu, ni wazi tu mashahidi wazuri wa
neno la Mungu ndani yetu na wale wote wanaotuzunguka.
Kuwa mashahidi na washuhuda wa neno ni sawa na
mbegu zile zilizoanguka “penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja
sitini, moja thelathini,” Mt 13:8. Hiki ndicho atakacho Yesu kwako na kwangu,
yaani, tuwe mashahidi wa kweli wa neno la Mungu. Na huu ndio ufafanuzi wa Yesu
juu ya udongo mzuri; “Naye aliyepandwa
penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye
ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini,” Mt 13:23.
Kuzaa huku matunda kwa viwango tofauti tofauti kunatokana na nguvu ya Roho ile
isukumayo ufahamu wetu juu ya neno ambalo sasa siyo tu tumelisika, bali
tumelipokea. Na siyo tu tumelipokea, bali tumelitafakari kwa kina na kulicheua.
Na siyo tu tumelitafakari kwa kina na kulicheua, bali kwa sasa tumelishirikisha
vyema kwa wengine (uinjilishaji upya). Na mwisho siyo tu tumelishirikisha neno
hilo kwa wengine bali tumekuwa sehemu ya neno hilo, kwa kuwa mashahidi na
washuhuda wa kweli kwa sababu maisha yetu yanaakisi kweli hiyo. Kumbe haitoshi
kufanya mambo mazuri katika ukamilifu wake, bali yakupasa kuwa mkamilifu katika
maana halisi ya ukamifu kama anavyotuasa Yesu, “Basi
ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt
5:48.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Naye
aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa
nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini,”
Mt 13:23
Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie nguvu, neema,
hekima na uwezo wa kulisikia neno lako, kulipokea, kulitafakari,
kulishirikisha, na kuwa mashahidi na washuhuda wa Neno hilo. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario