lunes, 18 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 16 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 16 YA MWAKA-C
Somo: Yer 1:1, 4-10
Zab: 71:1-2, 3-4a, 5-6ab, 15ab y 17
Injili: Mt 13:1-9
Nukuu:
Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa,” Yer 1:5

Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto,” Yer 1:6

 “Akawaambia mambo mengi kwa mifano, akisema, Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda,” Mt 13:3

 “nyingine zikaanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini,” Mt 13:8

TAFAKARI: Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa.”

Wapendwa wana wa Mungu, kuzaliwa siyo lazima, ila ukisha zaliwa kufa ni lazima. Kama kufa ni lazima, basi yakupasa kufa kifo chenye hadhi, yaani uache simulizi jema. Hapa ndipo penye tofauti kati ya “Lihoka na Muhenga.” Lihoka ni Roho Chafu au mbaya, na ndani yake hakuna chochote cha kujifunza, zaidi ya uharibifu. Mhenga ni Roho njema, na yenye kuigwa hata baada ya nafsi husika kutoka kwenye ulimwengu huu na kuingia katika ulimwengu wa roho. Mfano: leo kila mtu anapotaka kuelezea Tanzania anayoipenda na angependa iwe hivyo haachi kumnukuu Mwalimu Nyerere, Rais wa kwanza wa Jamuhuri ya Tanzania. Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa Taifa la Tanzania leo ni Mhenga, yaani, ameacha mazuri ya kujifunza. Leo Baba huyu anatambulika kama “Baba wa Taifa la Tanzania,” pasipo kikao chochote rasmi cha kumtambulisha hivyo. Sifa hii imekuja kama ilivyo kutokana na mastahili yake kama yalivyo. Hakika ni jambo la ajabu sana, na kama muhujizi wa kutambua utakatifu wake, basi tuanze hapa.

Ndugu yangu tunayesafari sote katika tafakari hii, ni vyema ukaelewa jambo hili; kama leo upo hai na unapumua, elewa kwamba “kabla hujaumbwa katika tumbo la Mama yako Mungu alikujua, na kabla hujatoka tumboni mwa Mama yako alikutakasa.” Nini maana ya maneno haya? Moja, wewe si wa bahati mbaya hapa duniani. Inawezekana kuna utata fulani katika kuzaliwa kwako kusikofuata utaratibu wa bila na desturi zetu, yaani, (Baba halali, nk), lakini elewa kwamba Mungu ndiye aliyekupa kibali cha kuishi na ndivyo ulivyo leo kama ulivyo. Pili, kwa uhai wako leo, Mungu anapenda mwisho wa siku uwe Mhenga, yaani, ‘uache kitu cha kuigwa katika ulimwengu huu.’ Na hii ndiyo maana ya maneno haya; Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Kumbe mwisho wa siku wa maisha yangu kama Mhenga ni kuwa Mtakatifu kama Baba yangu wa Mbinguni alivyo Mtakatifu. Utakatifu kwa hakika ndicho cheo chetu cha juu kabisa kuliko vyeo vyote. Bila Utakatifu huwezi kumwona Mungu hata kama leo katika ulimwengu huu kila mwanadamu atakuabudu na kukutukuza. Lakini kwa ubinadamu wao hawawezi kukupatia cheo hiki, yaani, utakatifu. Ndiyo twasema, ‘waweza kuwa na marafiki wengi, ila siyo ‘watakatifu.’

Hivyo, kama leo uwepo wako hapa duniani ‘sio kwa bahati mbaya,’ Mungu anamaanisha haya aliyomaanisha alipo mwita Nabii Yeremia, kwamba, Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa,” Yer 1:5. Mungu asemapo ‘ndiyo,’ hakuna malaka yoyote hapa duniani yenye uwezo wa kupindisha matakwa ya Mungu. Mamlaka hizi hapa duniani zinaweza kuchelewesha tu (na Mungu kuruhusu hali hiyo) kile apendacho Mungu uwe kwa lengo la kukuimarisha, na wakati huo huo kutoa fundisho wa jamii husika.

Ni kweli isiyo shaka kwamba tuupimapo uwezo wetu na mazingira yetu, ni vigumu kukubaliana na matakwa ya Mungu kwa sababu sisi kama wanadamu tuna mipaka na kikomo chetu. Mungu ni zaidi ya mipaka na vikomo vyetu. Katika mazingira na hali hii, Yeremia anajibu wito huo mbele ya Mungu kama ifuatavyo, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto,” Yer 1:6. Ni kweli hakuna anayekua kwa mzazi wake. Kama mzazi wako yu hai, basi kwa hakika huwezi kuondoa ukweli wa wewe kuwa mtoto. Ila utoto huu si katika hali ya ‘kitoto,’ bali utoto wa ‘kujitambua,’ na wenye kubeba wajibu. Kwa mantiki hii, Mungu alimjibu Yeremia na kumwambia, Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru,” Yer 1:7. Hapa ndipo kwenye wajibu. Ndugu yangu, uwepo wako hapa ulipo ni ‘WAJIBU.’ Kile kisichokuwa na wajibu si ‘hai.’ Mimi na wewe leo tunaposema ‘sina cha kufanya,’ ni sawa na kuukubali ‘ufu’ ungali hai. Ni kweli kabisa kwamba ‘wajibu’ fulani ututia hofu kwa sababu wajibu huo unatutaka ‘kuvuja’ ili ‘uhai’ uwepo pale tulipo. Hata katika mazingira haya ya hofu, Mungu anasema, Usiogope kwa sababu ya hao maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe,” Yer 1:8. Je, kwa hakikisho hili la Mungu bado waikumbatia hofu yako?

Ndugu yangu, ni pale tu unapoishinda hofu yako ndipo Mungu huunyoosha mkono wake na kuyatakasa mapungufu yako na kukupa uwezo ya kuyakabili yote katika njie ile aliyokuitia. Hivi ndivyo anavyokiri Nabii Yeremia, Ndipo Bwana akaunyosha mkono wake, akanigusa kinywa changu; Bwana akaniambia, Tazama, nimetia maneno yangu kinywani mwako; angalia, nimekuweka leo juu ya mataifa na juu ya falme, ili kung'oa, na kubomoa, na kuharibu, na kuangamiza; ili kujenga na kupanda,” Yer 1:9-10. Je, naamini nguvu ya Mungu ndani yangu?

Wapendwa wana wa Mungu, Injili ya leo inatoa mifano mbalimbali namna tuupokeapo ujumbe wa Mungu na kuufanyia kazi. Yesu anatumia lugha ya picha kuelezea kweli hiyo ndani ya mioyo yetu. Kuufikisha ujumbe huo, Yesu anatupa mfano wa mpanzi. Afanyacho mpanzi huyu ni namna neno la Mungu lifanyavyo kazi ndani ya mioyo yetu na kutubadilisha. Ili neno la Mungu liwe tumaini la kweli, na ushuhuda wa kweli ndani yetu na kwa wale wanaotuzunguka, lazima neno hilo tulisikie, tulipokee, kulitafakari, kulishirikishe, na mwisho tuwe sehemu ya neno hilo kwa kuwa mashahidi wa neno hata ikibidi kufa kwa kweli hiyo. Kulipokea neno lazima uwe na utayari wa kulisikia neno. Usipokuwa na utayari huu ni sawa na  “mbegu nyingine zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila,” Mt 13:4.

Kulitafakari neno la Mungu kunakuhitaji kulisikia neno hilo na liguse maisha yako. Kutafakari neno ni kama kucheua kile ulichokula. Kama hili halikufanyika ni sawa na mbegu zile zilizoanguka penye miamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara zikaota, kwa udongo kukosa kina, na jua lilipozuka ziliungua; na kwa kuwa hazina mizizi zikanyauka,” Mt 13:5-6.

Ndugu yangu, kuwa na uwezo wa kulishirikisha neno la Mungu kunategemea sana namna tunavyolicheua neno la Mungu, yaani, uwezo ule wa kulitafakari neno la Mungu. Tunaposhindwa kufanya hivyo ni sawa na mbegu  “zilizoanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikazisonga,” Mt 13:7. Kumba tunaweza kushirikisha neno la Mungu vizuri pale tunapokuwa na mazingira mazuri ya kulitafakari neno la Mungu kama lilivyo, na siyo tulivyo kwa kujionea huruma. Tunapofanikiwa katika hatua hii, ni wazi tu mashahidi wazuri wa neno la Mungu ndani yetu na wale wote wanaotuzunguka.

 Kuwa mashahidi na washuhuda wa neno ni sawa na mbegu zile zilizoanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini,” Mt 13:8. Hiki ndicho atakacho Yesu kwako na kwangu, yaani, tuwe mashahidi wa kweli wa neno la Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo

Nyingine zikaanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini,” Mt 13:8


Tusali:-Ee Yesu, tufanye mbegu bora na zenye kuzaa vizuri pale tulipo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario