JUMAMOSI
WIKI YA 15 YA MWAKA-C
Somo: Mik 2:1-5
Zab: 10:1-2, 3-4, 7-8, 14
Injili: Mt 12:14-21
Nukuu:
“Ole
wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao! Kunapopambazuka
asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao,” Mik 2:1
“Nao hutamani
mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na
nyumba yake, naam, mtu na urithi wake,” Mik 2:2
“Basi
Bwana asema hivi, Angalia, nakusudia jambo baya juu ya jamaa hii, ambalo
hamtazitoa shingo zenu, wala hamtakwenda kwa kiburi; kwa maana ni wakati
mbaya,” Mik 2:3
“Naye
Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya
wote, akawakataza
wasimdhihirishe,” Mt 12:15-16
“Mwanzi
uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo
hukumu ikashinda,” Mt 12:20
“Na jina lake Mataifa watalitumainia,” Mt 12:21
TAFAKARI: “Na
jina lake Mataifa watalitumainia.”
Wapendwa wana wa
Mungu, ni ukiri ulio wazi kwamba jumuiya ya kwanza ya Wakristo waliona ‘Ukuu na
Utukufu’ wa jina ya ‘Yesu Kristo’ katika maisha na changamoto zao za kila siku.
Na kwa matiki hiyo, Mtume Petro anayasema haya; “hakuna wokovu katika mwingine
awaye yote, kwa maana ‘hapana jina’ linguine chini ya mbingu walilopewa
wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Ndugu yangu unayesafiri
nami katika tafakari hii, pamoja na Imani yangu kama Mkristo, kuna jambo moja
ambalo sina shaka nalo kabisa katika njia hii niifuataya. Tuitazamapo historia
ya mwanadamu na wokovu wake, wametokea watu wengu na wenye uwezo (kiimani na
kimaadili) kiasi cha kwamba waliweza hata kuanzisha mitindo ya maisha na imani
zake na kupokelewa kwa wingi wa watu. Hata pamoja na ukweli huo, watu hawa
waliishi na mwisho wa siku walikufa.
Pamoja na ukweli kwamba Bwaba wetu Kristo naye
aliishi na mwisho wa siku alikufa, tofauti na hawa wengine ni kwamba, ‘Kristo
baada ya siku tatu alifufuka kutoka wafu.’ Kwa kweli hii na tendo hili, sina
shaka kabisa kwa njia hii niifuatayao hasa kwa maneno haya ya uzima ya Bwana
wangu Yesu Kristo, kwamba, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa
Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Yesu anaenda mbali zaidi na kusema, “Na
uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo
uliyemtuma,” Yoh 17:3. Ni katika mantiki hii kwamba, kama wote tupo hapa
duniani kwa sababu na malengo, na mwisho wa siku kuna maisha baada ya kifo, ni
dhahiri kwamba, “jina lake
(Yesu Kristo) Mataifa watalitumainia,” Mt 12:21.
Kuishi
katika tumaini la kweli na haki ni kutenda yale yampendezayo Mungu. Ni kuishi
maisha ya ukamilifu kila siku ingawa udhaifu upo. Na hivi ndivyo Mfalme
Sulemani anavyowaswa na Mungu kuishi; “na wewe,
ukienda mbele zangu kama alivyokwenda Daudi, baba yako, kwa ukamilifu wa moyo,
na kwa adili, kufanya hayo yote niliyokuamuru, na kuzishika sheria zangu na
hukumu zangu, ndipo
nitakapokifanya imara kiti cha ufalme wako juu ya Israeli milele; kama
nilivyomwahidia Daudi, baba yako, nikisema, Hutakosa kuwa na mtu wa kukaa
katika kiti cha enzi cha Israeli,” 1Fal 9:4-5. Kwa wanyofu wa moyo ‘ukamilifu’
ni akiba ya ‘hekima kamili,’ kama
tusomavyo kutoka kitabu cha Mithali, “kwa kuwa Bwana huwapa watu hekima;
Kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu; Huwawekea wanyofu akiba ya hekima
kamili; Yeye ni ngao kwao waendao kwa ukamilifu,” Mit 2:6-7. Kumbe njia iliyo
salama ni kutenda kadiri ya Hekima ya Mungu tukilenga ule ukamilifu ingawa
udhaifu upo. Na angalizo ni hili; “Ole
wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao! Kunapopambazuka
asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao,” Mik 2:1. Mimi na
wewe yatupasa kuwaza na kutenda lililo kweli na haki kwa yeyote yule
ninayekutana naye. Wale wote wasio na
soni machoni mwao na kupoteza kweli na haki, “hutamani
mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na
nyumba yake, naam, mtu na urithi wake,” Mik 2:2. Ni kuwa na tamaa ya kila kitu,
ilihali uwezo huo hauna kwa sababu katika ulimwengu huu sote twaishi kwa wakati
tu.
Ndugu yangu, “Bwana asema
hivi, ‘Angalia, nakusudia jambo baya juu ya jamaa hii, ambalo hamtazitoa shingo
zenu, wala hamtakwenda kwa kiburi; kwa maana ni wakati mbaya,’” Mik 2:3. Kumbe
hatupaswa kuuchukulia upole na huruma ya Mungu kama nafasi ya kukwepa wajibu
wetu. Hakuna haki pasipo wajibu.
Hata hivyo ni vigumu sana kuukataa mfumo wa
maisha ambao kwayo tumeishi muda mrefu hata kama hauna tija. Wengi wetu huogopa
sana kile tusichokijua kwa yale tuyatarajiayo. Ni ndani na katika Kristo
tunapata uhakika wa kile tusichokijua na tusichokuwa nacho katika uhasilia wake
licha ya shida na dhiki tuzipatazo kadiri ya wito kwa kila mmoja wetu. Mungu
anasema hivi juu ya Yesu, yaani, uwezo na mamlaka aliyonayo, kwamba, “Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi
utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda,” Mt 12:20. Huyu ndiye
Yesu!
Wapendwa wana wa Mungu,
ni kupitia jina lake Yesu Kristo twaponywa na twalitumainia milele yote. Ukweli
huu si kwa sisi tu wafuasi wake, yaani wabatizwa-wakristo, bali kwa mataifa
yote. “Na jina lake Mataifa
watalitumainia,” Mt 12:21. Kwa hiyo ndugu yangu, popote pale ulipo mfanye Yesu
kuwa sababu ya ukweli ndani yako, njia ya maisha yako, na uhai wako.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ole
wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao!” Mik 2:1a
Tusali:-Ee Yesu Mwema
nitalihimidi jina lako milele. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario