jueves, 28 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 17 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI  YA 17 YA MWAKA-C
Somo: Yer 26:11-16, 24
Zab: 69:15-16, 30-31, 33-34
Injili: Mt 14:1-12
Nukuu:
Ndipo hapo makuhani, na manabii, wakawaambia wakuu na watu wote, wakisema, Mtu huyu amestahili kufa, kwa sababu ametabiri juu ya mji huu, kama mlivyosikia kwa masikio yenu,” Yer 26:11 

Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote, akisema, Bwana ndiye aliyenituma kutabiri juu ya nyumba hii, na juu ya mji huu, maneno hayo yote mliyoyasikia,” Yer 26:12

 “Maana Herode alikuwa amemkamata Yohana, akamfunga, akamtia gerezani, kwa ajili ya Herodia, mke wa Filipo nduguye,” Mt 14:3 

Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4 

 “Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani,” Mt 14:9-10

TAFAKARI: “Kuwa tayari na jiandae kwa kulipa gharama pale utakapo simama katika kweli na haki.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo kwa namna ya pekee tunapotafakari ule ‘utayari wa kulipa gharama pale utakapo simama katika kweli na haki,’ Nabii Yeremia na Yohane Mbatizaji ndiyo dira na kielelezo cha kweli hiyo. Ipo vita kubwa sana kati ya giza na mwanga. Popote pale kinapokuwepo kimoja, ni kwa namna hiyo hiyo kwamba kingine kipo vitani kukipindua kile kinachoonekana. Hata kama hakionekani haimaanishi kwamba hakipo.

Na sasa tuanze kwa kumtazama Nabii Yeremia kwa kile alichokisimamia katika kweli na haki, na madhara anayokumbana nayo. Utabiri ule wa Yeremia ambao ni ujumbe kutoka kwa Mungu, Yer 26:4-6, unazua taharuki na kufikia hatua ya makuhani na manabii kuitoa roho yake. Ukitaka urafiki na ulimwengu huu, waambie watu kile wanachopenda kusikia. Hapa utapigiwa magoti na makofi kuanzia walevi hadi wafalme wa ulimwengu huu. Kwa vile Yeremia alisimama katika kweli na haki ya Mungu, mambo yalimwendea ndivyo sivyo katika mizania ya kibinadamu. Ndipo hapo makuhani, na manabii, wakawaambia wakuu na watu wote, wakisema, Mtu huyu amestahili kufa, kwa sababu ametabiri juu ya mji huu, kama mlivyosikia kwa masikio yenu,” Yer 26:11. Kutokana na mtafaruku huu, Yeremia haachi kuwaeleza chanzo na sababu ya ujumbe ule wa Mungu. Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote, akisema, Bwana ndiye aliyenituma kutabiri juu ya nyumba hii, na juu ya mji huu, maneno hayo yote mliyoyasikia,” Yer 26:12. Mara nyingi hata baada ya kuujua ukweli kwa vile twapenda kuendelea katika uovu, hutumia nguvu kubwa kuushikilia uovu, badala ya kubadilika na kuwa mikono salama zaidi.

Ndugu yangu, katika hali na mazingira kama haya, yakupasa kujiandaa vizuri kwani vitisho huwa vingi sana ili tu kukukatisha tamaa na kurudi nyuma. Je, katika hali na mazingira haya tujisalimishe na kuifunga midomo yetu? La hasha! Pamoja na vitisho hivyo, Yeremia anasimamia maneno yake, na kuwaambia, tengenezeni njia zenu, na matendo yenu, mkaisikilize sauti ya Bwana, Mungu wenu; naye Bwana atayaghairi mabaya aliyoyanena juu yenu,” Yer 26:13. Licha ya kuyasimamia maneno yake, Yeremia anataka waone ukweli kama ulivyo kwa sababu yote hayo ni kwa faida yao wenyewe. Lakini kwangu mimi, tazama, mimi nipo hapa mikononi mwenu; nitendeni myaonayo kuwa mema na haki mbele ya macho yenu,” Yer 26:12. Penye ukweli uongo hujitenga. Na hivi ndiyo asemavyo Yeremia, kwamba, Lakini jueni yakini ya kuwa, mkiniua, mtajiletea juu yenu damu isiyo na hatia itakuwa juu yenu, na juu ya mji huu, na juu ya wenyeji wake; kwa maana ni kweli Bwana amenituma kwenu, kuwaambieni yote mliyoyasikia,” Yer 26:15. Huu ni ujumbe mzito sana kwa wale watesi wake Yeremia. Na walioguswa na neno lile waliuona ukweli na kusema, Mtu huyu hastahili kuuawa; kwa maana amesema nasi katika jina la Bwana Mungu wetu,” Yer 26:16b. Na pona ya Yeremia ilikuwa hivi, mkono wa Ahikamu, mwana wa Shafani, alikuwa pamoja na Yeremia, wasimtie katika mikono ya watu auawe,” Yer 26:24.

Mpendwa, katika Injili ya leo tunaona hathari za matumizi mabaya ya madaraka yanayosababisha maafa makubwa kwa wale watetezi wa haki katika jamii inayowazunguka. Ni jambo la hatari sana kuwa na kiongozi anayeongozwa na mihehuko ya hisia zake, huku akitegemea sifa kutoka kwa watu. Kiongozi mwenye misukumo hii ya kihisia ni rahisi sana kuzikanyaga haki za wale anaowaongoza. Hii ni pamoja na kuwa kutokuwa makini katika ahadi azitoazo kiongozi mbele za watu. Herode anamwahidia binti yake chochote apendacho baada ya kucheza vizuri na kuufurahisha umati wa watu siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7. Mfalme Herode anajifunga kwa kauli yake mwenyewe. Mfalme Herode hakuwa na lakusema binti yake alipokitaka kichwa na Yohane Mbatizaji zaidi ya kutimiza ahadi yake na kulinda heshima yake kama kiongozi. Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe,” Mt 14:9. Je, ni watu wangapi huwa kafara kunakotokana na utafutaji wa sifa na umaarufu wa baadhi ya viongozi wetu?

Ni mbaya sana kutafuta umaarufu kwa kukanyaka haki za watu, na hasa wale ambao wapo kinyume chetu kutokana na matendo yetu yasiyo haki na hofu ya Mungu. Yohane Mbatizaji ni mhanga wa viongozi wale wenye kupenda sifa na umaarufu. Kosa la Yohane Mbatizaji ni kusimama katika kweli. Umauti unamfika Yohone Mbatizaji kwa sababu alimwambi Mfalme Herode Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4. Wapo wahanga wengi wa mtindo wa Yohane Mbatizaji katika familia zetu, Jumuiya zetu ndogondogo za Kikristo, Jumuiya zetu za kitawa, Makanisani mwetu, sehemu zetu za kazi, na mbaya zaidi leo katika mfumo mzima wa utawala.

Herodia ameitumia nafasi hii ipasavyo kumwangamiza mtesi wake ambaye alikuwa kero kubwa hasa pale alipomsaliti mumewe na kuishi na Herode. Kamwe hatuwezi kuhalalisha kosa kwa kutenda kosa. Tunachofanya ni kupata haueni ya muda mfupi tu, ila dhambi na kusutwa kwa ndani hubaki na hata kuongezeka kwa sababu hapa tunacheza na haki ya mtu katika kweli, na kilio kisichokoma cha damu ya mwenye haki. Ni vyema tukayatafakari kwa kina matendo yetu katika kupima faida na hasara zake. Hakika hutobaki salama kwa kufanya dhuluma kwa mtu mwenye haki. Yohana Mbatizaji anawawakilisha wengi leo katika jamii yetu. Wapo wengi leo wamenyamazishwa hata kuuwawa kwa sababu tu za kisiasa na hasa pale waliposema ‘hii halili jambo hili kuwa kama lilivyo.’ Wapo pia wengi walionyamazishwa na hata kuuwawa kwa vile tu walijaribu kuufichua uovu katika maana ya kugusa maslahi ya watu fulani.

Wapendwa tuutafute kwanza ufalme wa Mbinguni na mengine yote tutapewa kwa ziada.

Tumsifu Yesu Kristo!

Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani,” Mt 14:9-10


Tusali:-Ee Mungu, tujalie hekima na busara katika uongozi. AminaT

No hay comentarios:

Publicar un comentario