lunes, 4 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 14 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 14 YA MWAKA-C
Somo: Hos 10:1-3, 7-8, 12
Zab: 105:2-3, 4-5, 6-7
Injili: Mt 10:1-7
Nukuu:
Israeli ni mzabibu, utoao matunda yake; kwa kadiri ya wingi wa matunda yake, kwa kadiri iyo hiyo ameongeza madhabahu zake,” Hos 10:1ab

 “kwa kadiri ya wema wa nchi yake, kwa kadiri iyo hiyo wamefanya nguzo nzuri,” Hos 10:1cd 

 “Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina,” Mt 10:1

 “Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 10:7
TAFAKARI: Jipandieni katika haki, vuneni kwa fadhili,” Hos 10:12a

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu akiwa ndiye udongo na nchi yenye rutuba, wana wa Israeli wanafananishwa na  mzabibu. Hivyo, Israeli ni mzabibu, utoao matunda yake; kwa kadiri ya wingi wa matunda yake, kwa kadiri iyo hiyo ameongeza madhabahu zake,” Hos 10:1ab. Ni kweli isiyo shaka kwamba, mmea hukua na kuzaa kadiri ya kipimo na uwezo wake pale unapostawi kwenye udongo mzuri na wenye rutuba. Itakuwa kituko cha hali ya juu kama mahitaji yote ya mmea yamekidhiwa, na mmea huo mwisho wa siku kutokufikia lengo lake la kuzaa matunda mengi na mazuri. Ni “kwa kadiri ya wema wa nchi yake, kwa kadiri iyo hiyo wamefanya nguzo nzuri,” Hos 10:1cd. Kwa hali ya kawaida tunategemea wewe na mimi uliye na hofu ya Mungu kutenda kadiri ya sifa ya Mungu, yaani, haki, amani, upendo, huruma, na msamaha. Kinyume chake ni kuasi kuliko wazi katika maana ya kutokuzaa matunda mema kulingana na yale Mungu aliyokukirimia bure na kwa upendo. Ni kutokumcha Bwana kuliko kwa wazi, na mfalme au mwenye dhamana katika umma katika kweli hii hata hesabiwa haki. Hatuna mfalme; kwa maana hatumchi Bwana,” Hos 10:3a. Mfalme au kiongozi yeyote yule na kwa nafasi yoyote ile pamoja na mambo yake mengi, ni alama ya ‘umoja na mshikamano kwa umma ule anaoungoza.’ Kiongozi mbaguzi na mwenye makundi hamwakilishi Mungu.

Hathari za kiongozi mwenye ghiliba kama hii huonekana mara. Miiba na mbigili huonekana kwenye himaya yake kwa sababu ndivyo visukumavyo fikra na utendaji wake. Hapa ndipo kwenye kulia na kusaga meno, na ‘tungejua nyingi’ zisizo na idadi kwa sababu, mwiba na mbigili imemea juu ya madhabahu zake; nao wataiambia milima, Tusitirini; na vilima, Tuangukieni,” Hos 10:8b. Kiongozi asiyejifunza kupanda katika haki na badala yake kupanda katika chuki na visasi, mavuno yake ni uharibifu. Hivyo ndugu zangu ‘tupande katika haki, ili tuvune kwa fadhili,’ Hos 10:12a. 

Kwa mantiki hiyo, ni vizuri kutambua pale tulipowaumiza wenzetu, au mwenzako na kujaribu kwa namna yoyote ile kupaponyesha. Hili ni jambo la muhimu sana tunapoishi kama familia, au jumuiya yoyote ile ya Kikristo. Kutambua kosa na kufanya juhudi ya kuleta uponyaji, kitendo hicho hutuponya pia. Agizo la Yesu kwenye injili ya leo linatupa fursa ya kupambana na uovu bila kushindwa.  Yesu akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina,” Mt 10:1. Hapa pia tunaalikwa kuushinda uovu kwa kutenda mema. Kama asemavyo Mt. Agustino; “ovu ni kutokuwa na mafaa,” kushinda lililo ovu ni kutenda lililo jema.

Ndugu yangu unayesafiri nami sasa, ‘misioni’ yetu hapa duniani kama watu wenye hofu ya Mungu ni kuwarudisha kundini wale waopotea au kukwazika kutoka na utendaji wetu wa awali au sasa. Ni mwaliko pia wa kujisahihisha pale tunapokosea. Yatupasa sana kuepuka kishawishi kile cha kusema ‘mkubwa na mwenye madaraka au cheo hakosei.’ Kasumba hii ni saratani mbaya sana katika utume wetu kama Kanisa mahalia na taasisi yoyote ile ya kiraia. Kama sisi ni binadamu, na ndivyo tulivyo, basi kukosea kupo. Kama kukosea kupo, kutambua na kujirekebisha ndipo kunakotuhesabia haki mbele ya Mungu juu ya utendaji wetu na dhamana tuliyopewa na Mungu mbele za watu na kondoo wa malisho yake. Hivyo Yesu anawatuma,  na kuwaagiza, akisema, “Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli,” Mt 10:5-6. Yesu analifanya hili kwa Thenashara wote ili hali akijua mmoja wao atamsaliti.  Hivyo, Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye kumsaliti,” Mt 10:4. Je, twaweza kuushinda uovu kwa kuzidi kutenda lililo jema na hata kuendelea kuona uzuri kwa wenzetu hata kama tumegundua njama na hila zao? Katika jambo hili bila shaka Yesu anatukumbusha thamani ya mtu na utu wake. Mt. Agustino anasema hivi: “usimchukie mtu, bali zichukie tabia zake mbaya.”

Mwisho kauli mbiu yetu: jana, leo, na kesho na iwe kuhubiri kusiko kikomo kwamba ufalme wa mbinguni umekaribia. Tunalisema hili iliwa ndiyo kauli mbiu ya Kanisa kama sakramenti ya wokovu wetu. Tunalihubiri hili kwa wengine tukijua kwamba ndani yetu na nafsini mwetu twauona na kuuonja ufalme huo wau pendo, haki, amani, upole, unyenyekevu, huruma na msamaha. Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 10:7

Tumsifu Yesu Kristo!

Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina,” Mt 10:1


Tusali:- Ee Yesu Mwema, tujalie nguvu na neema ya kushinda uovu kwa wema. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario