JUMATANO WIKI YA 17 YA MWAKA-C
Somo:
Yer 15:10, 16-21
Zab: 59:2-3, 4-5a, 10-11, 17
Injili:
Mt 13:44-45
Nukuu:
“Maneno
yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na
shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Bwana, Mungu wa
majeshi,” Yer 15:16
“Kwa
sababu hiyo Bwana asema hivi, Ukirudi, ndipo mimi nitakapokurejeza, upate
kusimama mbele zangu; nawe ukitoa kilicho cha thamani katika kilicho kibovu,
utakuwa kama kinywa changu; nao watakurudia wewe, bali hutawarudia wao,” Yer
15:19
“Tena ufalme wa
mbinguni umefanana na hazina iliyositirika katika shamba; ambayo mtu alipoiona,
aliificha; na kwa furaha yake akaenda akauza alivyo navyo vyote, akalinunua
shamba lile,” Mt 13:44
“Tena
ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri,” Mt 13:45.
TAFAKARI:
“Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na
maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa
kwa jina lako, Ee Bwana, Mungu wa majeshi.”
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, ujasiri wa Nabii Yeremia umejengwa katika neno la Mungu. Ujasiri huu
siyo tukio litokealo mara moja, bali lina hatua zake, na kila hatua huanzisha
hatua nyingine. Kwa maana nyingine, kila hatua mpya huwa tokea la hatua
iliyotangulia. Hivyo kwa ufupi ujasiri wa Nabii Yeremia unaonekana katika haya
ayasemayo, “Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako
yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina
lako, Ee Bwana, Mungu wa majeshi,” Yer 15:16. Ni
muhimu kutambua mabadiliko ndani yako yenye mwelekeo wa kweli na haki ya
Kimungu. Hii ni hatua ya kwanza katika Neno la Mungu. “Ole
wangu, mama yangu, kwa kuwa umenizaa mtu wa kuteta, na mtu wa kushindana na
dunia yote! Mimi sikukopesha kwa riba, wala watu hawakunikopesha kwa riba;
lakini kila mmoja wao hunilaani,” Yer 15:10.
Na
sasa tuzame ndani ya ujasiri ule wa Nabii Yeremia kama tokeo la neno la Mungu
lililo yabadilisha maisha yake. “Maneno yako yalionekana,” inamaanisha,
‘kulisikia neno. Kulisikia neno ni hatua ya
utofautishaji wa jumbe tuzisikiazo na kuchota maana, na tumaini la kweli la
kule tuendapo tusipokujua. “Sikuketi
katika mkutano wao wanaojifurahisha, wala sikufurahi, naliketi peke yangu kwa
sababu ya mkono wako; kwa maana umenijaza ghadhabu,” Yer 15:17. Hi ni hatua ya
upembuzi wa kile tukisikiacho.
“Nami
nikayala,” inamaanisha, ‘kulipokea neno,’ kwani
huwezi kufanya hivyo kama hujalisikia neno. Kuyala maneno ya Mungu ni ‘neno la
Mungu kama mwanga huanza kulifukuza giza ndani yetu na kuangaza nuru ile ya
Mungu ambao ndio uhai na uzima halisi. Hivyo Mtume Petro katika hili anasema, “Nasi
tuna lile neno la unabii lililo imara zaidi, ambalo, mkiliangalia, kama taa
ing'aayo mahali penye giza, mwafanya vyema, mpaka kutakapopambazuka, na nyota
ya asubuhi kuzuka mioyoni mwenu,” 2Pet 1:19
“Na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu,”
kunamaanisha ‘kulitafakari neno.’ Na unaweza tu kulitafakari neno kama
‘umelipokea neno’ hilo. Neno hili husababisha mitikisiko ndani ya nafsi yako. Hapa ndipo unapotambua kwamba, “mbona maumivu yangu ni ya daima, na jeraha yangu haina dawa,
inakataa kuponywa? Je! Yamkini wewe utakuwa kwangu kama kijito kidanganyacho,
na kama maji yasiyodumu?” Yer 15:18. Kumbe
tunapozama katika tafakari ya neno la Mungu ambalo ndilo uzima ndani yetu,
tunaanza kutambua ndani yetu mambo hayako salama.
Tunatambua yapo mambo
ya kurekebisha ili neno liendelee kuwa uzima na uhai ndani yetu. Tunatambua pia
vyanzo vya mashaka na wasiwasi wetu ambavyo kwa kiasi fulani ndiyo sababu ya
kutokuwa na furaha. Hapa ndipo ninatambua nguvu na udhaifu wangu. Hapa ndipo
ninapoanza safari mpya na kuelekea kule liliko tumaini la kweli. Hapa ndipo
tunapomwamsha roho yule ndani yetu tukitambua mwili wetu ni hekalu la Roho
Mtakatifu. “Mkijua neno hili
kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama
apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya
mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho
Mtakatifu,” 2Pet 1:20-21
Hapa ndipo ninapotambua bila Mungu mimi si
lolote wala chochote. “Kwa
sababu hiyo Bwana asema hivi, Ukirudi, ndipo mimi nitakapokurejeza, upate
kusimama mbele zangu; nawe ukitoa kilicho cha thamani katika kilicho kibovu,
utakuwa kama kinywa changu; nao watakurudia wewe, bali hutawarudia wao,” Yer
15:19
“Shangwe ya moyo wangu,” yamaanisha, ‘utayari
ule wa kulishirikisha neno la Mungu kwa wengine, na furaha ya Mungu iliyopo ndani yangu. Furaha
ni kama kikohozi huwezi kukizuia. Unaweza kushirikisha furaha hii kama tunda la
tafakari ya kina. Hivyo ushirikishwaji wa neno la Mungu kwa wengine ni tokeo la
tafakari ya kina. “Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu
hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe,
ili nikuokoe, na kukuponya, asema Bwana,” Yer 15:20. Kulishirikisha neno la
Mungu kwa wengine ni tokea la kulitafakari neno la Mungu vyema ambalo wakati
huu limeyabadili maisha yako. Hivyo tunalishirikisha neno la Mungu
tunavyokomazwa na neno hilo na kuwa sehemu ya neno hilo kama ulivyo uhusiano wa
maji na samaki. Bila maji hakuna uhai wa samaki. Hii ndiyo furaha
tuishirikishayo kwa wengine. Uhai na uzima huu tuupatao mara baada ya kuzama
katika tafakari ya kina, na kushirikisha uhai na uzima huo kwa wengine, ndiyo
sababu ya ujasiri wetu na kuwa tayari kuwa mashahidi na washuhuda wa neno bila
woga.
“Maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Bwana, Mungu
wa majeshi,” maneno haya yamaanisha ‘kuwa shahidi na shuhuda wa neno la Mungu
hata ikibidi kufa.’ Hatua hii haitazami nafsi na ubinafsi wako, bali kweli na
uzima ule wa neno ndani yetu, 2Pet 1:20-21. Kuwa shahidi wa neno bila woga ni kutambua nafasi ya Mungu
katika maisha yako, na kumwachia Mungu usukani wa maisha yako. Ni kuamini
pasipo shaka maneno haya ya Mungu kwamba, “Nami nitakuokoa na mkono wa watu wabaya, nami
nitakukomboa katika mkono wao wenye kutisha,” Yer 15:21.
Na hii ndiyo maana halisi ya maneno haya
ya Yesu kuhusu ufalme wa mbinguni, yaani,
“Tena ufalme wa mbinguni umefanana na hazina
iliyositirika katika shamba; ambayo mtu alipoiona, aliificha; na kwa furaha
yake akaenda akauza alivyo navyo vyote, akalinunua shamba lile,” Mt 13:44. Hapa hatuna woga tena kwa sababu neno la Mungu
lina mizizi imara ndani yetu na kutufanya sehema ya uimara na uhai huo. Hii
ndiyo lulu ndani ya maisha yetu. Hakuna wakutunyang’anya kwani ndiyo uzima
ndani yetu. “Tena ufalme wa mbinguni
umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri,” Mt 13:45. Je, ni nani aliye tayari kuipoteza
lulu hii nzuri ndani ya maisha yake? Kuipata lulu hii, na iwe sehemu ya thamani
ya urithi wako, yaani, uzima na uhai ule niutamanio, sina budi kuzipitia hatua
hizi tano muhimu, yaani; kusikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno,
kulishirikisha neno, na kwisho kuwa sehemu ya neno hilo kama shahidi na
shuhuda.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nami
nitakuokoa na mkono wa watu wabaya, nami nitakukomboa katika mkono wao wenye
kutisha,” Yer 15:21
Tusali:-Ee Yesu Mwema,
tuimarisha katika neno lako siku zote na tufanye mashahidi na mashuhuda wa neno
hili katika kweli na haki. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario