JUMAPILI YA 15 YA MWAKA-C
Somo
I: Kumb 30:10-14
Zab: 69:13, 16, 29-30, 32-33, 35-36,
Somo
II: Kol 1:15-20
Injili:
Lk 10:25-37
Nukuu:
“ukiwa
utaifuata sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa kuyashika maagizo yake, na amri zake
zilizoandikwa katika chuo hiki cha torati; ukimwelekea Bwana, Mungu wako, kwa
moyo wako wote, na kwa roho yako yote. Kwa
maana maagizo haya nikuagizayo leo, si mazito mno kwako, wala si mbali,” Kumb
30:10-11
"Kwa
kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi,
vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi,
au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake,” Kol 1:16
“Kwa kuwa katika yeye
ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote
na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa
ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni,” Kol 1:19-20
“Akajibu
akasema, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na
kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako,”
Lk 10:27
TAFAKARI:
“Fanya hivi nawe utaishi,” Lk 10:28b
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 15 ya mwaka “C” wa Kanisa. Mama Kanisa
leo anatutafakarisha juu ya matendo ya uzima. Ikiwa ilimpendeza Mungu kutuumba
kwa sura na mfano wake kama tokeo la pendo lake, Mungu wetu huyu aliye mwanzo
na mwisho, na mwenye kuishi milele yote, lengo la kuumbwa kwetu ni kuishi
milele. Kuishi kwetu leo na sasa katika ulimwengu huu kusukumwe na upendo. Na
‘fanya hivi nawe utaishi.’ Ni katika kupenda tunaishi kwa sababu tunajua lengo
la kuubwa kwetu katika maana ya kumpenda Mungu na jirani, Mt 22:37-39. Na
katika amri hivi mbili hutegemea torati yote na manabii, Mt 22:40. “Ukiwa utaifuata sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa
kuyashika maagizo yake, na amri zake zilizoandikwa katika chuo hiki cha torati;
ukimwelekea Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote. Kwa maana maagizo haya nikuagizayo
leo, si mazito mno kwako, wala si mbali,” Kumb 30:10-11.
Kuishi tena na tena ni
‘kupenda bila kipimo kama kipimo cha upendo,’ na ndivyo atufundishavyo
Mtakatifu Augustino wa Hippo. Kielelezo cha upendo huu ni Kristo mwenyewe. Naye
Yesu anasema, “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka
katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao
mengi,” Yoh 12:24. Kumbe nisipokuwa tayari kwa ‘upendo sadaka,’ ishi yangu
inaulakini mkubwa. Kristo kwa kutupenda upeo, Yoh 13:1,
aliutoa uhai wake ili mimi na wewe tuishi na kuhesabiwa haki kama wana wa Mungu
na warithi wa ufalme wake wa milele. “Kwa kuwa katika yeye
ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote
na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa
ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni,” Kol 1:19-20. Ndugu yangu,
huyu ndiye Kristo.
Wapendwa wana wa Mungu,
pamoja na mbwembwe zote za mwanadamu hapa duniani, ni wajibu wa kila mmoja wetu
kujiuliza swali hili la msingi alilouliza mwana-sheria mmoja wa Kiyahudi kwa
Yesu kuhusu uhai. Mwana-sheria huyu anamuuliza Yesu hivi; “Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa
milele?” Lk 10:25. Msingi wa swali hili haupo kwenye uhai tu wa leo na kesho,
bali uhai katika umilele wake. Tuelewe kwamba mwanadamu ameumbwa kuishi milele,
na hayo ndiyo makusudi ya Mungu katika uumbaji wa mwanadamu. Tatizo kubwa la
mwanadamu ni mbwembwe nyingi alizonazo akisahau kuwa muda aliopewa hapa duniani
hausimami kumsubiri. Mhubiri anatuwasa na kusema, “mwanadamu hadumu katika
heshima, bali amefanana na wanyama wapoteao,” Zab 49:12. Fahari ya mwanadamu ni
yule aliyemuumba, yaani Mungu wake. Mengine yote ni mbwembwe tu! “Mche Bwana, Mungu wako, umtumikie yeye; ambatana naye, na kuapa
kwa jina lake. Yeye ndiye fahari
yako, na yeye ndiye Mungu wako, aliyekutendea mambo haya makubwa, ya kutisha,
uliyoyaona kwa macho yako,” Kumb 10:20-21. Ndugu unayesafiri nami katika
tafakari hii, elewa kwamba utajiri wako, ufahamu wako (kiwango cha elimu ulicho
nacho), umaarufu wako, nk, bila Mungu ni bure kabisa.
Yesu
kabla ya kumjibu vizuri mwana-sheria yule wa kiyahudi alitaka kujua uelewa wake
wa Maandiko Matakatifu (Torati) yanasema nini kuhusu uhai wa Milele.
Mwana-sheria yule akamjibu kwa staha, “Mpende
Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako
zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako,” Lk 10:27. Yesu
anaridhika na jibu hili na amamwambia hivi; “Umejibu vema; fanya hivi nawe
utaishi,” Lk 10:28. Kuishi kwetu hapa duniani ambapo kunatupelekea kuishi
milele baada ya kifo, kama wanadamu kwatuwajibisha kufanya kwa weledi mkubwa
mambo makuu mawili.
Moja, mpende Mungu wako kwa moyo wako wote, roho yako yote,
na nguvu zako zote. Kwa maana nyingine ni kutumia vyote Mungu alivyokujalia ili
umpende na ubaki kumpenda daima. Afya yako njema, akili yako ya pekee, utajiri
wako, na umaarufu wako hapa nduniani isiwe sababu ya kujitenga na upendo huu wa
Mungu. Hayo Mungu aliyokujalia kwa namna ya pekee isiwe sababu ya kuwakejeli
wenzako ambao kwa mtazamo wako wa kibinadamu waona hawastahili mema yoyote
mbele ya uso wa Mungu. Ndugu yangu, hata yale tunayoyaona kwa macho yetu kama
udhaifu wa mtu na wengine, Mungu wakati mwingine utumia udhaifu huo
kutufundisha siri ya maisha na uhai tuliopewa na Mungu mwenyewe. Maisha na uhai tuliyonayo ni mali na zawadi yake
Mungu. Mimi na wewe tumepewa uhai huu na kuazimwa kwa muda tu hapa duniani kama
sababu ya kuutumia vyema uhai huu ili tuishi milele baada ya muda ambao kila
mmoja wetu kapewa kadiri ya mapenzi yake Mungu. “Maana siku zangu zinatoweka
kama moshi, Na mifupa yangu inateketea kama kinga,” Zab 102:3.
Pili, nimpende jirani yangu kama nafsi yangu. Jirani yangu
ni yeyote yule ninayekutana naye na wale wote wanaonizunguka, yaani, wahitaji
na wasio wahitaji. Jirani yangu ni kama kioo cha kujitazama ukamilifu wangu
mbele ya Mungu. Je, udhaifu wa jirani yangu unasema nini kuhusu maisha yangu
mimi niliyejiinua na kujiona safi na mwema kuliko wengine? Yesu, anakemea hali
hii kwa Mafarisayo na Waandishi, na kwetu pia. “Waandishi na
Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi,
yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo
yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi,” Mt 23:2-3. Mtazamo huu wa
ugeugeu na kujiinua mbele za Mungu pasipo mastahili yoyote ndio sababu ya mfano
wa Msamaria mwema. Wafarisayo ambao kwa kiasi kikubwa walijiinua na kuwa wepesi
kuwahukumu wengine, wanashindwa kuokoa uhai ambao ni mali na zawadi ya Mungu
kwa vile tu muhitaji huyu na mhusika huyu hakuwa Myahudi. Wakati mwingine
tunashindwa kusimama katika kweli kwa vile tu mhusika siyo kutoka familia yetu,
ukoo wetu, kabila letu, au kutoka Kanda yetu. Wenye mitazamo kama hii ilihali wanajiita
wafuasi wa Kristo, basi Kristo huyo huendelea kusulubiwa kwa matendo yao.
Kristo huyo siyo fahari ya maisha yao. Mimi na wewe kama wafuasi wa Kristo
hatuna kitu kingine cha kujivunia zaidi ya Msalaba wa Kristo. “Lakini mimi, hasha,
nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo,
ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14.
Je, tusikemee maovu? La hasha! Mkemeapo “Basi, wekeni mbali uovu wote na hila yote, na unafiki na husuda
na masingizio yote. Kwa sababu
ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia
kielelezo, mfuate nyayo zake. Yeye
alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi
kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye
mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa
mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa,”
1Pet 2:1, 21, 23-24. Je, nauona udhaifu wangu ninapoutazama udhaifu wa
mwingine?
Wapendwa
wana wa Mungu, Yesu anapomwambia mwana-sheria yule afanye tathimini kati ya
wale wayahudi na yule Msamaria aliyetoa msaada kwa mhitaji yule aliyepata
kipigo na wanyang’anyi, mwana-sheria anaelewa soma lile na kumjibu Yesu, “Ni huyo aliyemwonea huruma. Yesu akamwambia, Enenda
zako, nawe ukafanye vivyo hivyo,” Lk 10:37. Wapendwa katika Kristo, yatupasa
kusimama katika kweli na haki, hivyo tutende yote kwa upendo na huruma ya
kweli. Tusipolifanya jambo hilo basi tujiandae kusutwa na dhamiri zetu katika
umiele wote.
Wapendwa
wana wa Mungu, mamlaka aliyokuwa nayo Yesu ni vita dhidi ya uovu hapa duniani.
Ni ukweli usiopingika kwa kupitia jina lake tunapata uponyaji wa kweli. “Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini
nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama
uende,” Mdo 3:6. Mamlaka
ya Yesu yamejengwa chini ya mamlaka ya Mungu. Hivyo hakuna jambo lolote
alifanyalo Yesu Lisilo kuwa na uhusiano na Mungu, huku jambo lile likifunua
siri ya Mungu kila kukichwa. “Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na
vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi,
au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa
ajili yake,” Kol 1:16. Kwa nini basi nakuwa na mashaka juu ya utendaji wa
Kristo katika maisha yangu?
Wapendwa
katika Kristo, Yesu anapotoa mfano wa vazi kuukuu na jipya, na kwa upande
mwingine divai ya zamani na kiriba kipya anataka kutufundisha jambo hili; “kwanza
kabisa lazima tujue sababu na malengo ya maisha yetu hapa duniani. Hatupo hapa
duniani kwa bahati mbaya hata kidogo. Tupo katika ulimwengu huu kadiri ya
mpango wa Mungu ambao ni dhahiri na mathubuti. Hivyo lolote lile lililo jema
mbele ya Mungu huwiishwa na kufanya upya.
Ndugu
yangu, maisha ya hapa duniani ni safari. Na katika safari hiyo kila siku
tunapimwa kwa upendo. John na Maria walipendana sana tangu walipokutana kwa
mara ya kwanza Chuo Kikuu. Baada ya miaka mitatu walifika lengo la kuishi kama
mume na mke. Hivyo likizo ya mwaka ule wa mwisho wa masomo yao, John
aliafikiana na Maria kwenda kwao na kujitambulisha ikiwa ni pamoja na
kuzungumza swala zima la mahari.
Wiki moja
kabla, Maria alitangulia nyumbani ili kuweka mazingira vizuri juu ya ujio wa
John Mchuma wake. Safari ya kuelekea kijiji kwa Maria haikuwa rahisi kwa John
kutokana na usafiri kuwa wa shida na barabara kuwa mbovu. Hata hivyo kwa vile
alikwisha penda, John alijitahidi na kupata usafiri ingawa ulikuwa wa
kugombania sana. Baba mmoja mwenye umri wa mtu mzima aliyekuwa nyuma yake John
katika kurupushani ile ya kugombania usafiri, shati lake lilichanika kiasi
kwamba kifua na tumbo lake vilikuwa wazi.
John na
Baba yule walikaa pamoja kwenye basi lile ingawa hali ile ya Baba kuwa kifua
wazi ilimsikitisha sana John. Ndipo John alipolivua sueta lake na kumpa Mzee
yule ajisitiri. Mzee yule alifurahi sana na kumwambia John, “asante sana
mwanangu kwa kuusitiri mwili wa Baba yako. Ubarikiwa popote uendapo na
utakapokuwa.” Basi John ndipo alipoanza kumwelezea ugeni wake na huko
anapokwenda kwa lengo la kujitambulisha kwa mchumba wake aliyekuwa anaitwa
Maria Majaliwa. Kadiri ya maelezo yale, Mzee yule alimwambia, “usihofu
chochote. Mimi naifahamu vizuri sana familia hiyo na binti huyo. Usijali nitakufikisha
mguu kwa mguu.”
Walipofika
kituoni, wote wawili waliongozana kuelekea kwenye familia ile ya Maria. Jambo
la ajabu walipokaribia tu kwenye nyumba ile Maria na ndugu zake walifika kwa
furaha kumpokea Baba yule na John, na mizigo yao yote kwa pamoja kuiingiza
ndani. Hapa ndipo John aliposhtuka na kumuuliza, “kumbe Baba wewe ndiye Mzee
Majaliwa Baba ya mchumba wangu Maria?” Naye akajibu, “ndiyo kijana wangu. Na
kwa ukarimu na upendo wako kwangu leo, sina shaka na ishi ya binti yangu nawe.
Baraka zangu zote nawapa, na yote yaliyo ndani ya mioyo yetu yawe kama Mungu
apendavyo.” Hakika ilikuwa furaha sana.
Ndugu
yangu, upendo wa kweli ni pale tunapomwona Kristo kwa kila tunayekutana naye
bila kujali historia yake, hali yake, familia yake, kufahamiana kwetu, na hata
kabila lake.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Mpende Bwana
Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote,
na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako,” Lk 10:27
Tusali:-Ee Yesu wangu mwema,
nifanye nuru na mwanga wako popote pale nitakapokuwa. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario