domingo, 10 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 15 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 15 YA MWAKA-C
Somo: Isa 7:1-9
Zab: 48:2-3a, 3b-4, 5-6, 7-8
 Injili: Mt 11:20-24
Nukuu:
Basi Bwana akamwambia Isaya, Haya, toka, umlaki Ahazi, wewe na Shear-yashubu mwana wako, huko mwisho wa mfereji wa birika la juu, katika njia kuu ya uwanja wa dobi; ukamwambie, Angalia, ukatulie; usiogope wala usife moyo, kwa sababu ya mikia hii miwili ya vinga hivi vitokavyo moshi; kwa sababu ya hasira kali ya Resini na Shamu, na mwana wa Remalia,” Isa 11:3-4 

“Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu,” Mt 11:21

Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe,” Mt 11:24 

TAFAKARI:Itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe.” 

Wapendwa wana wa Mungu, wahenge wanasema, ‘sikio la kufa halisikii dawa.’ Moja ya njia ya kukua kiroho na kimwili ni kuuona uhalisia wa mambo kama ulivyo. Mtazamo huu upo hata kwenye maisha ya kawaida ya kila siku. Ushabiki wa mambo unapozidi ukweli wa mambo, kifuatacho ni kupiga jaramba la maendeleo pale pale ulipo huku ukijifariji kwa upumbavu. Na heri aliye mjinga kwani upo uwezekano wa kujifunza na kuelewa kuliko kuwa mpumbavu usiye tayari kujifunza kwa sababu wajifariji kujua usichokijua.

Jamii yoyote ile inayoghubikwa na upumbavu itaichukuwa muda mrefu sana kuifikia kweli. Hata pamoja na giza hili, Mungu hachoki kusimama katika kweli na haki kwa watu wake. Wapo kati yetu wausimamiao ukweli na hata kuchukiwa na kundi hili kubwa la wapumbavu. Nabii Isaya ni mmoja ya watu hayo waisimamiayo kweli. Naye anamwambia Mfalme Ahazi, “usiogope wala usife moyo,” Isa 11:4a. Lililo kweli na libaki kama lilivyo na lisimamie hadi mwisho.

Mara zote tunapopambana na kweli, au kujikwamua kwenye shida fulani, mawazo pingamizi hayakosekani. Ugumu huu wakati mwingine husababishwa na kutokuwa na ufahamu wa kutosha wa jambo lile. Jambo hili ndilo analolisema Yesu anapoitazama miji ile iliyokithiri kwa uovu. “Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu,” Mt 11:21. Ni mara ngapi tunaambiwa ukweli wa mambo lakini mara zote tunabakia na ushabiki usiokuwa na tija yoyote? Kwa nini hatupendi kuona ukweli kama ulivyo na badala yake tunaupindisha? Katika jambo hili, Yesu anatupa angalizo na kusema, Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe,” Mt 11:24.

Wapendwa, hawatashuka malaika kutoka mbinguni na kutuambia mambo haya zaidi ya watu wenye uelewa tunaoishi nao kila siku kutuambia kweli hiyo. Mungu utumia watu wake kulisemea lile lililo ovu. Watu wenye maadili mema na mwono chanya, walisemapo jambo yatupasa kusikia na kulipembua kwa kina. Je, yote yasemwayo kuhusu maisha yako, hali yako, na Taifa lako hayana ukweli? Je, unaridhika na hali hii? Umechukua hatua yo yote?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida!” Isa 11:21a


Tusali:-Ee Mungu tupe nguvu ya kusimama katika kweli na haki

No hay comentarios:

Publicar un comentario