domingo, 17 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 16 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 16 YA MWAKA-C
Somo: Mik 7:14-15, 18-20
Zab: 85:2-4, 5-6, 7-8
Injili: Mt 12:46-50
Nukuu:
Alipokuwa katika kusema na makutano, tazama, mama yake na ndugu zake walikuwa wakisimama nje, wataka kusema naye,” Mt 12:46 

Akajibu, akamwambia yule aliyempasha habari, Mama yangu ni nani? Na ndugu zangu ni akina nani?” Mt 12:48

Kwa maana ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu,” Mt 12:50

Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia?” Mik 7:18a

“Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema,” Mik 7:18b

TAFAKARI: Ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.”

Wapendwa wana wana Mungu, Somo la kwanza, kutoka kitabu cha Nabii Mika linatuelezea uhasili wa Mungu. Mungu kwa asili ni Upendo, Huruma, na Msamaha. Ni Mungu anayetutakia mema muda wote sisi viumbe na wana wake. Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia?” Mik 7:18a. Ni Mungu anayejifunua kwetu kupitia historia na vile alivyoviumba. Ni Mungu ambaye yupo na alikuwepo na atakuwepo milele yote.

 Kwa upande wetu,  tunayokazi moja tu, yaani kumtafuta kwa maana anapatika. Nabii Isaya anatuambia hivi, “Mtafuteni Bwana, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu baribu; Mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa.” Isa 55:6-7

Ndugu yangu, kumwasi Mungu ni tendo ambalo lipo chini ya uwezo wetu. Kumrudia Mungu ni tendo la toba na kufanya maamuzi ya msingi kabisa. Mungu “hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema,” Mik 7:18b. Unapofanya maamuzi haya ni wazi itakulazimu  kuachilia mengi ambayo kwayo yalikupa furaha na hata kujulikana na kujikweza. Ila tukitambua umuhimu wa umilele wa maisha yetu, hatuna budi kuachilia yote haya ambayo ni ya kupita na ya muda mfupi. Mungu atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya baharí,” Mik 7:19 

Ufanyapo toba ya kweli na kumrudia Mungu, anakupokea kama tulivyo. Mungu katika mapokezi haya hatazamani historia yako iliyo mbaya. Mungu huanza mradi mpya nawe na kukufanya mpya tena katika yale mazuri anayokufikiria. “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11. Ndugu yangu, kwa nini hubadiliki? Waitaji malaika washuke na kukuambia jambo hili? Kwa nini unakuwa kero kwa ndugu na jirani zako? Kwa nini unakuwa kero kwa wanajumuiya wako na viongozi wako? Je, unapenda kuishi hivyo hadi lini?

Ndugu yangu elewa jambo hili; sote tumefanywa wana na ndugu kwa upendo wa Mungu kwa njia ya Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo. Na hapa ndipo tunapoiona asili ya Mungu, yaani, Upendo, Huruma, na Msamaha. Maandika Matakatifu yanatufundisha hivi: Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Kwa tendo hili la upendo wa Mungu kwa kumtoa mwanaye Yesu Kristo, leo hii sote tumefanywa ndugu katika Kristo. Hivyo Yesu haoni haya kuwaambia wazazi wake ukweli huu. Akajibu, akamwambia yule aliyempasha habari, Mama yangu ni nani? Na ndugu zangu ni akina nani? Akawanyoshea mkono wanafunzi wake, akasema, Tazama, Mama yangu na ndugu zangu! Kwa maana ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu. ” Mt 12:48-50

Kuyafanya mapenzi ya Mungu ni kutambua ukweli huu wa kumwilishwa Bwana wetu Yesu Kristo. Mungu ambaye alikuwa mbali sana na viumbe vyake sasa yupo karibu, yaani: Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi,” Mt 1:23. Huyu ndiye Mungu anayetuunganisha na kuwa watoto wake bila kujali familia zetu, koo zetu na kabila zetu. Yeyote yule mwenye kujinadi kwa koo au kabila lake na kujiona bora kuliko wengine, na huku akijiita mfuasi wa Kristo na Mkristo, bado hayajitambua.

Tumsifu Yesu Kristo

“Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema,” Mik 7:18b


Tusali:- Ee Mungu, twasema asante kwa kutupenda kama tulivyo, na upo tayari kutusamehe. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario