IJUMAA
WIKI YA 15 YA MWAKA-C
Somo: Isa 38:1-6, 21-22, 7-8
Zab: 38: 10, 11, 12abcd, 16
Injili: Mt 12:1-8
Nukuu:
“Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana
utakufa, wala hutapona,” Isa 38:1b
“Mimi
nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku
zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami
nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji
huu,” Isa 38:5-6
“Akawaambia,
Hamkusoma alivyotenda Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wenziwe? jinsi alivyoingia katika nyumba ya
Mungu, akaila mikate ile ya wonyesho, ambayo si halali kwake kuila wala kwa
wale wenziwe, ila kwa makuhani peke yao?” Mt 12:3-4
“Lakini kama
mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu
wasio na hatia,” Mt 12:7
“Kwa
maana Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato,” Mt 12:8
TAFAKARI: “Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.”
Wapendwa wana wa Mungu, tunapoongelea ufunua
wa wazi na wa kweli wa Mungu, kigoto chake au hitimisho lake ni ‘Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu,’ Yoh
1:14. Tendo hili limebebwa katika upendo wa kweli wa Mungu, na dhumuni na
malengo ya uumbaji wake. “Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu;
ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa,
aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine,” Isa 45:18.
Ndugu yangu unayesafiri nami sasa katika tafakari hii, upendo huu wa Mungu
ikiwa ni pamoja na nia na kusudi lake, haukufifishwa licha ya maanguko ya
mwanadamu. Na huu ndiyo uthibitisho wa upendo wa Mungu kwetu kwamba, “kwa
maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila
mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele,” Yoh 3:16. Ni kwa upendo
wake Mungu na siyo mastahili yetu kwamba Mungu alituumba kwa sura na mfano wake
mwenyewe, Mwa 1:27. Hivyo wokovu wetu katika mantiki hii ilikuwa ni swala la
wakati tu kwa upande wetu. Mungu hakufungwa na hajafungwa na wakati kwa nyakati
zote zote kwa sababu yeye ni alfa na omega, Ufu 1:8; 21:6; 22:13. Hakika, ‘Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato,’ Mt 12:8
Ni
katika maana hiyo ya Mungu kutokufungwa na wakati, na ilipompendeza na
kusadifu, alisema ‘sasa inatosha na nitafanya kitu na kutimiza lengo langu.’
Hivyo, “Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu
nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana,
aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu,” Ebr 1:1-2.
Tendo hili la ajabu na la Kimungu linamwinua mwanadamu katika maana ya
kumshirikisha, yaani, Mungu kuchukua umbo la mwanadamu ili kuwezesha na kufikia
kile kilicho cha Kimungu. Hii ndiyo maana halisi ya Neno kufanyika mwili na
kukaa mwetu. Mtume Paulo anaelezea kweli hii kwa maneno haya: “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu
alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini
ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4:4-5. Ni upendo
gani huu wa ajabu wa Mungu ambao mimi na wewe tukae kimya bila kumshukuru
Mungu? Kwa maana nyingine tendo hili la Mungu lamaanisha hivi; ‘Mungu aliye
tajiri wa kila kitu amekubali kujishusha ili mimi na wewe tuwe tajiri kwa
umasikini wake.’ Hakika Mungu anakupenda na ananipenda sanaaaaaaa! Katika kweli
hii ya Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Mungu katika umasikini wake ili
tuwe matajiri, Mtume Paulo anasema, “maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo,
jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba
ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Ndugu yangu una sababu
yoyote ya kujiona mnyonge ilihali unapumua pumzi ya Mungu bila tozo lolote?
Ndugu yangu, ni katika hali na mazingira hayo
niliyoyasema kama utangulizi wa tafakari yetu ya leo, Nabii Isaya ana
mwakilisha Mungu mbele ya Mfalme Hezekia katika hali yake ya kufa. Katika hali
hii, Nabii Isaya anaenda kwa Mfalme Hezekia na kumwambia, “Tengeneza mambo ya
nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona,” Isa 38:1b. Ndugu yangu, kufa ni lazima, ila kuzaliwa siyo
lazima. Kama kufa ni lazima, umejiandaaje na tukio hili la lazima? Kwa kutambua
kweli hii juu ya maisha na kifo ambacho ni lazima, Mfalme Hezekia anakiri haya
mbele ya Mungu, “Ee Bwana, kumbuka
haya, nakusihi, kwamba nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo
mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana,” Isa
38:3. Hatuna sababu ya kuwa na hofu na mashaka mbele ya Mungu kama twaenenda
mbele zake Mungu katika kweli na haki. Pasipo shaka yoyote, Mungu anamjibu
Mfalme Hezekia kwa kinywa cha Nabii Isaya; “Mimi
nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku
zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami
nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji
huu,” Isa 38:5-6. Na maneno haya ya Mungu
yalithibitishwa kwa ishara hii, “Na
watwae mkate wa tini, wakauweke juu ya jipu, naye atapona,” Isa 38:21. Hakika
Mungu ni mwaminifu nyakati zote! Hivyo
kama Mungu ni mwaminifu nyakati zote, huo ndio mwito wetu mbele ya Mungu,
yaani, kuwa waaminifu kwake, Mt 5:48. Na kwa mantiki hiyo, yote tuyafanyayo
lazima yawe na uhusiano na Mungu.
Wapendwa
wana wa Mungu, Mungu hapendi sadaka zetu zisizo na uhusiano wa maisha yetu na
thamani mbele zake. Mungu wetu hupenda rehema na neema anazotujalia pale
tunapoziishi kuliko kile tumtoleacho kama sadaka. Yote tumtoleayo ni mali yake,
Zab 24:1. Vyote vipo chini ya mamlaka yake. Hivyo Yesu anasema, “Lakini kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala
si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia,” Mt 12:7. Wapendwa wana wa Mungu,
bila shaka kutokana na mila na desturi zetu, wakati fulani tulilazimika kufanya
mitambiko na hata kutolea sadaka za kuteketezwa zisizo na uhusiano na imani
yetu. Kwa kufanya hivi tunapoteza dira na mwelekeo wa Kimungu katika maisha
yetu. Je, naweza kuwa huru hata kama naishi katika mila na desturi hizi? Jibu
ni HAPANA! “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana
atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu.
Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24
Tumsifu
Yesu Kristo.
“Tengeneza mambo
ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona,” Isa 38:1b
Tusali:-Ee Yesu ujuaye
siri ya maisha yangu, nasema asante kwa sababu kwangu wewe watosha. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario