martes, 26 de julio de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 17 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI  YA 17 YA MWAKA-C
Somo: Yer 18:1-6
Zab: 146:1b-2, 3-4, 5-6
Injili: Mt 13:47-53
Nukuu:
 “Na chombo kile, alichokuwa akikifinyanga, kilipoharibika mkononi mwake yule mfinyanzi, alikifanyiza tena kuwa chombo kingine, kama alivyoona vema yule mfinyanzi kukifanya,” Yer 18:4

Ee nyumba ya Israeli, je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulivyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli,” Yer 18:6 

Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya samaki wa kila namna,” Mt 13:47

 “Akawaambia, Kwa sababu hiyo, kila mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni amefanana na mtu mwenye nyumba atoaye katika hazina yake vitu vipya na vya kale,” Mt 13:52 

TAFAKARI: “Mungu yupo tayari kuanza upya nawe. Ni utayari wako tu.”

Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka kuna wakati unafika nakujiona hufai mbele ya Mungu, na hasa pale unapoitazama historia yako iliyo mbaya. Kama binadamu wakati mwingine tunajiangalia katika maana ya kujihukumu kwa sababu hatuna tumaini tena katika maisha. Mungu wetu aliye Upendo na Huruma tazama yake kwetu ni ile yenye kubeba uhasili wake, yaani, Upendo na Huruma. Mungu daima yupo tayari kuanza upya nasi tunapojirudi na kuacha njia zetu mbaya. Kumbe hapa yategemea utayari wangu, na kuona upendo na huruma hii ya Mungu isiyo na mipaka.

Taswira hii ya Mungu aliye Upendo na Huruma inajidhihirisha kwa Nabii Yeremia kwa mfano wa nyumba ya mfinyanzi, aliye kuwa akifanya kazi yake kwa magurudumu, Yer 18:2. Mungu katika mfano huu anapenda kuufunua upendo na huruma yake. Haijalishi historia yako mbaya wala kuanguka kwako, bali utayari wako wa kuamka na kuanza upya na Mungu. Naye Mungu anamwambia Yeremia, Ondoka, ukashuke mpaka nyumba ya mfinyanzi, na huko nitakusikizisha maneno yangu,” Yer 18:2. Na hivi ndivyo Yeremia alivyoona akifanya yule Mfinyanzi;Na chombo kile, alichokuwa akikifinyanga, kilipoharibika mkononi mwake yule mfinyanzi, alikifanyiza tena kuwa chombo kingine, kama alivyoona vema yule mfinyanzi kukifanya,” Yer 18:4. Ndugu yangu, hivi ndivyo Mungu huyabadili maisha yako pale unampomrejea. Na katika tendo hili, Mungu anaufunua upendo na huruma yake na kusema akitumia kinywa cha Nabii Yeremia, Ee nyumba ya Israeli, je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulivyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli,” Yer 18:6. Hakuna limshindalo Mungu kama tutakuwa tayari kumrejea katika hali ya toba na majuto ya kweli. Mungu hawezi kuumba jiwe kubwa kiasi kwamba Yeye mwenyewe akashindwa kulibeba.

Mungu wetu huyu ambaye ni Huruma na hukumu yake ni ya haki, hayupo katika hali ya kutuvizia tunapotenda kosa au dhambi na kutuadhibu. La hasha! Mungu wetu ambaye taswira na uhalisia wake ni UPENDO NA HURUMA, utuvumilia hadi mwisho akiwa na matumaini makubwa kubadilika kwetu kutoka katika njia mbaya na kumrudia yeye. Hivyo, licha ya anguko la wazazi wetu wa kwanza, Mungu hakuondoa uhuru ndani yetu wa kumrudia baada ya kutambua mienendo yetu mibaya. Ni kwa uhuru huo huo twaweza kurudi kwake au kuendelea katika hali ya uasi na dhambi.

Ndugu yangu, kuishi katika kweli na haki ya Mungu ni kuishi katika ufalme wake. Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya samaki wa kila namna; hata lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa,” Mt 13:47-48. Hivyo ni katika kweli na haki hii tunapokutana na hukumu ya haki ya Mungu. Mungu hutupa hali na uwezekano wa kuziacha njia zetu mbaya na kumrudia ili mwisho wa siku tusipate nafasi yoyote ya kumtupia lawama. Mungu anaheshimu sana uhuru wa kila mmoja wetu, kwa sababu ndiye Yeye aliyetuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Mungu hapendi kutuburuza kama nyapara gerezani.

Elimu ya ufalme wa Mbinguni ni kujifunza kweli na haki ya Mungu. Ni katika kweli tunakuwa huru, Yoh 8:32, na ni katika kutimiza mapenzi ya Mungu kadiri ya maagizo yake tunahesabiwa haki. Tunapotimiza jambo hili kwa ufasaha wake, twatwaliwa haki ya mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni. Naye Yesu anasema, Kwa sababu hiyo, kila mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni amefanana na mtu mwenye nyumba atoaye katika hazina yake vitu vipya na vya kale,” Mt 13:52. Huku ndiko kuwa wapya katika Kristo na ndani ya Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulivyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli,” Yer 18:6b

Tusali:-Ee Mungu uliye Upendo na Huruma yetu, tuongoze daima katika kweli na haki. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario