sábado, 16 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 16 YA MWAKA-C

JUMATATU WIKI YA 16 YA MWAKA-C
Somo: Mik 6:1-4, 6-8
Zab: 50:5-6, 8-9, 16bc-17, 21, 23
Injili: Mt 12:38-42
Nukuu:
Kwa maana nalikupandisha kutoka nchi ya Misri, na kukukomboa utoke katika nyumba ya utumwa, nami naliwapeleka Musa, na Haruni, na Miriamu, watangulie mbele yako,” Mik 6:4 

Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” Mik 6:8

Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona,” Mt 12:39

 “Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani,” Mt 12:42 

TAFAKARI:Tenda haki, na kupenda rehema, na enenda kwa unyenyekevu.”

Wapendwa wana wa Mungu, kwa upendeleo wa ajabu Mungu alioufanya kwetu, yaani kwa kutuumba kwa sura na mfano wake, hatuna budi kuwa watu wa haki na kupenda rehema, na kuenenda kwa unyenyekevu kama shukrani kwa Mungu kwa tendo hili la ajabu. Ni kwa upendeleo huu Mungu haachi kwamwe kukupigania licha ya uasi wako na njia zako mbaya. Naye Mungu asema, Kwa maana nalikupandisha kutoka nchi ya Misri, na kukukomboa utoke katika nyumba ya utumwa, nami naliwapeleka Musa, na Haruni, na Miriamu, watangulie mbele yako,” Mik 6:4. Mungu apenda kila mmoja wetu awe huru, na katika uhuru huo achague ni nani anayetaka kumtumikia. Ni ndani ya uchaguzi huu ulio huru tunapojihukumu sisi wenyewe. Siku ya mwisho, yaani, katika ukuhumu ile, Mungu atafanya hakikisho tu la hukumu ambalo kwa kadiri tunavyoishi ndivyo tujihumivyo kwa uhuru ule tuliokuwa nao. Na hii ndiyo maana ya maneno haya;Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” Mik 6:8. Huu ndio wito wetu wa kila siku kama wafuasi wake Kristo na wale wote wenye hofu ya Mungu.

Matumaini yetu mbele za Mungu hayapaswi kusukumwa na ishara kama ndiyo msingi wa kumwamini Mungu. Ishara au miujiza itusaidie kukoleza Imani yetu na wala sio msingi wa imani yetu. Yesu anatoa angalizo na kusema, “kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona,” Mt 12:39. Ndugu yangu, hakuna ishara zaidi ya Yesu mwenyewe ambaye ndiye yote katika yote. Fumbo zima la wokovu wetu limekamilishwa kwa kumwilishwa neno, Yoh 1:14. Hivyo basi hakuna ishara kubwa zaidi ya hii. Naye Yesu anasema, Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani,” Mt 12:42. Bwana wetu Yesu Kristo ndiyo kila kitu kwetu. Je, bado waitafuta njia? Yesu ndiye njia. Je, bado wautafuta ukweli? Yesu ndiye ukweli. Je, wautafuta uzima? Yesu ndiye uzima wa kweli. Ngoja nikujuze!

Naye Yesu anasema, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Yesu Kristo ni njia kama ulivyo Mlango pekee wa kuufikia uzima wa milele. Na njia aliyoichagua Yesu ni Msalaba. Kwa kuibeba misalaba yetu na kuchukuliana kindugu katika misalaba yetu na ya wenzetu kwa uaminifu na hofu ya Mungu tunakutana naye Kristo katika hali na mazingira hayo. Yesu Kristo ni kweli halisi. Kweli hii tunakutana nayo katika neno lake hasa pale tunapokuwa tayari kulisikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno, kulishirikisha neno, na mwisho kuwa shahidi wa neno.

Na Yesu Kristo ni uzima halisi. Kristo ni uzima halisi tunaposhiriki Ekaristi Takatifu katika mastahili yake. Yesu anatuambia, “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe” Yoh 6:35. Ni katika kula chakula hiki-mwili na damu yake,  Yesu anahaidi mambo mawili makuu: Moja, ni ufufuko siku ya mwisho. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:54. Na katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Kristo hukaa ndani yetu. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake,” Yoh 6:56. Hata hivyo Mtume Paulo anatupa angalizo la chakula hiki cha uzima. Naye anasema, Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana,” 1Kor 11:27. Yatupasa kuijongea Meza ya Bwana tukiwa na mastahili ya kufanya hivyo-usafi wa mwili na roho, yaani, pasipo hatia yoyote. Zaidi ya hapo ni kuikufuru Meza ya Bwana.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa kupitia Sakramenti ya kitubio tunapatanishwa tena na Kristo kutoka katika hatia zote. Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu,” Isa 1:18. Hakuna sababu ya kufa moyo pale ambapo mambo huenda ndivyo sivyo. Mungu aliye Upendo na Huruma uanza upya nasi pale tunapokuwa tayari kufanya hivyo. Hivyo ndani na katika Kristo hakuna sababu ya kuwa na hofu. Tumwamini Kristo na tuziamini kazi zake na hasa kupitia Masakramenti yake. Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi,” Yoh 14:1.

Ndani na Katika Kristo kunautulivu wa kweli, naye kesha tuandalia makao ya milele. Duniani hapa ndugu yangu tunapita tu. Ulimwenguni hapa ni sehemu ya maandalizi ya huo umilele. Mbinguni ndipo kwenye nafasi ya kila mmoja wetu, na ndiyo makao ya milele. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali,” Yoh 14:2. Lengo la Kristo ni kumpata kila mmoja wetu. Hili ndilo pia lengo msingi la Kanisa. Lilipo Kanisa katika maana ya Mwili wa Kristo nasi tukiwa viungo hai vyake, Kanisa huwa Sakramenti ya Wokovu kwa sababu Kristo yu hai mahali hapo. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo,” Yoh 14:3. Ndungu yangu, je, hu kiungo hai cha mwili wa Kristo, yaani Kanisa?

Tumsifu Yesu Kristo!

Akajibu, akawaambia, Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona,” Mt 12:39


Tusali:- Ee Yesu, Wewe watosha. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario