JUMATATU
WIKI YA 6 YA PASAKA
Somo:
Mdo 16:11-15
Zab:
149: 1b-2, 3-4, 5-6a, 9b
Injili:
Yoh 15:26-16:4
Nukuu:
“Mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya
zambarau, mwenyeji wa Thiatira, mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake
ulifunguliwa na Bwana, ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo,” Mdo 16:14
“Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba yake, akatusihi,
akisema, Kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni nyumbani mwangu
mkakae. Akatushurutisha,” Mdo 16:15
“Lakini
ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli
atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia,” Yoh 15:26
“Watawatenga
na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea
Mungu ibada,” Yoh 16:2
“Lakini
nimewaambia hayo, ili makusudi saa ile itakapokuja myakumbuke ya kuwa mimi
naliwaambia. Sikuwaambia hayo tangu mwanzo, kwa sababu nalikuwapo pamoja
nanyi,” Yoh 16:4
TAFAKARI:
“Uwepo wako kama Mkristo hai ni kutangaza vita dhidi ya uovu na shetani.”
Wapendwa wana wa Mungu,
jana yaani dominika ya sita ya Pasaka tumeanza wiki ya sita ya Pasaka, na baada
ya dominika ya Kupaa kwake Bwana wetu Yesu Kristo, tutasherekea Sikukuu ya
Pentekoste. Ni tukio kubwa sana Kikanisa tunapompokea Roho Mtakatifu
tuliyeahidiwa na Bwana wetu Yesu Kristo. Pamoja na Karama zake na Mapawa yake
katika Kanisa, Roho Mtakatifu hufanya kazi
kubwa sana ya kutufanya kitu kimoja ndani na katika Kristo. Sifa mojawapo
kubwa ya Roho Mtakatifu ni kutufanya wamoja, ikiwa ndiyo sala kuu ya Yesu
Kristo kabla ya mateso na kifo chake, aliposali, “Na
kwa ajili yao najiweka wakfu mwenyewe, ili na hao watakaswe katika kweli. Wala si hao tu ninaowaombea; lakini na
wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao.
Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao
nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe
uliyenituma. Nami utukufu ule
ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja,” Yoh 17:19-22.
Bila umoja huu, na mwongozo wa Roho Mtakatifu, maisha yetu kama Wakristo yapo
hatarini kabisa. Hivyo, leo natulitafakari neno hili, “Uwepo wetu kama Wakristo
hai ni kutangaza vita dhidi ya uovu na shetani.” Vita hivi vinaushindi pale tu
tunapoishi na Kristo na kuongozwa na Roho Mtakatifu ambaye anatufunulia yote
tusiyoyajua bado na kutufundisha njia sahihi ya kufuata.
Roho huyu Mtakatifu
tunapewa pale tunapoyapokea Sakramenti yake Matakatifu, naye hutujaza neema na
kutufanya kuwa wapya. Haya yote hufanyika kwetu si kwa juhudi zetu, wala kazi
zetu, bali kwa mastahili yake Mungu mwenyewe. Hivyo, “si kwa sababu ya matendo
ya haki tuliyotenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa
pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu; ambaye alitumwagia kwa wingi, kwa njia
ya Yesu Kristo Mwokozi wetu; ili tukihesabiwa haki kwa neema yake, tupate
kufanywa warithi wa uzima wa milele, kama lilivyo tumaini letu.” Tit 3:5-7.
Ni roho huyu kwa namna
ya pekee huwaongoza walioridhiwa naye kuisha maisha yanayompendeza Mungu kama
ilivyotokea kwa mwanamke yule, Lidia wa Filipi. Na mambo yalikuwa hivi, “Mwanamke
mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira,
mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze
maneno yaliyonenwa na Paulo,” Mdo 16:14. Mtume Paulo alitumika vizuri kwa
jumuiya hii iliyoko Filipi, na hivyo anaacha kitu cha kuigwa. Ukweli ni kwamba,
tunapoisha hapa duniani mwisho wa siku ya maisha yetu moja ya mambo haya mawili
lazima litokee; kuwa MUHENGA au LIHOKA! Muhenga ni mtu yule anayeacha kitu cha
kuigwa na wengine baada ya maisha yake, kama mchango katika jamii hiyo
aliyoisha na kutoa maisha yake kama ushuhuda wa kiroho ma kimaadili. Lihoka ni
mtu yule ambaye hakuacha chochote kama somo la kuigwa, na watu kujifunza kiroho
na kimaadili. Hivyo mtu huyu anakuwa roho mbaya/ovu kwa jamii ile aliyoiacha,
“bad spirit!” Kwa ushuhuda huu wa Mtume Paulo uko Filipi, anabakia kuwa
Muhenga. Ndugu yangu, jambo hili linasema nini kuhusu utume wako na wito wako
hapo ulipo?
Wapendwa,
nimeanza kwa kusema moja ya kazi kubwa ya Roho Mtakatifu ni kutufanya wamoja.
Hivyo Roho huyu hakumpendelea tu Lidia kufanya kama alivyofanya baada ya
kumpokea kupitia Sakramenti ya ubatizo, ila nyumba yake yote walijazwa neema ya
Mungu, na kuishi katika hofu hiyo ya Mungu, na kuleta taswiri nzima ya uwepo wa
Roho Mtakatifu. Hivyo, “Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba
yake, akatusihi, akisema, Kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni
nyumbani mwangu mkakae. Akatushurutisha,” Mdo 16:15. Shurutisho hili wanalopata
Mtume Paulo na mwenzake Barnaba, ni shurutisho la upendo uliotukuka. Yeyote
anayeongozwa na Roho wa Bwana hakwishi kuwa na upendo wa kujitoa kwa wengine.
Roho huyu huwa sehemu ya kwanza katika kuanzisha joto hilo la upendo kwa
jirani, Roho huyu humwezesha mtu husika kujitoa bila kujibakiza, na mwisho Roho
huyu humfanya mtu huyo kuwa na huruma.
Hakika
kwa matendo haya ya Roho Mtakatifu kwa Mkristo ni sababu tosha ya kuwa na vita
vya kudumu dhidi ya uovu, na hasa yule mwovu shetani. Katika hili Yesu
anatuambia, “Watawatenga na
masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea
Mungu ibada,” Yoh 16:2. Matendo hayo mema yafanywayo kwa nguvu ya Roho
Mtakatifu kwetu, ni Ibada tosha ya Mungu, kwani Mungu ni MWEMA. Hivyo mwovu
shetani katika uovu wake, hatafurahiwa na jambo hili. Hata katika hali hii Yesu
anatutumia Msaidizi wa kutufanya kubaki katika upendo na wema huu wa Kimungu. “Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka
kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia,” Yoh 15:26.
Roho huyu licha ya kutushuhudia kweli ya Kristo katika maisha yetu,
anatufunulia yale yaliyo nje ya uwezo wetu wa Kibinadamu. Hivyo tendo hili
linamfanya Mungu wetu kuitwa Mungu, na Waajabu muda wote kwa wale wenye hofu
juu yake.
Wapendwa wana wa Mungu,
Yesu anatuambia haya yote ili itakapofika saa ile, yaani wakati ule wa
kujaribiwa kwetu, na wakati ule wa kuutoa ushuhuda wetu mbele ya watu juu ya
Kristo, tujue kwamba hatupo wenyewe, bali yupo nasi na haachi kutupigania.
Hivyo, “nimewaambia hayo, ili makusudi saa ile itakapokuja
myakumbuke ya kuwa mimi naliwaambia. Sikuwaambia hayo tangu mwanzo, kwa sababu
nalikuwapo pamoja nanyi,” Yoh 16:4. Hali hii inatukumbusha msimamo wetu kiimani
hasa pale tunapokumbana na sintofahamu kwenye maisha yetu. Mkristo aliyeiva
katika imani hii, mara zote Mganga yake Mkuu ni Kristo. Ndugu yangu, mara ngapi
umemsaliti mganga huyu Mkuu Yesu Kristo na kwenda kwa akina “nsonganzingwe”?
Embu tazama kifua chako, kiuno chako, shingo yako, paja lako la uso na sehemu
nyingine ujuazo zilivyo chanjwa na kukufanya kama umevaa mkanda wa Rambo! Usicheke! “Jesus is the master key.” Mrushusu naye
atatenda. Amina
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka
kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia,” Yoh 15:26
Tusali:-Ee Yesu, usinitoe katika kweli hii; wewe tu baki kwangu kuwa Njia, Kweli
na Uzima. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario