sábado, 28 de mayo de 2016

TAFAKARI: SHEREHE YA MWILI NA DAMU YA BWANA WETU YESU KRISTO

SHEREHE YA MWILI NA DAMU TAKATIFU YA BWANA WETU YESU KRISTO-C
Somo: Mwa 14:18-20
Zab: 110:1-4 (K) 4
Somo II: 1Kor 11:23-26
Injili: Lk 9:11-17
Nukuu:
Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye juu sana,” Mwa 14:18 

 “Ahimidiwe Mungu Aliye juu sana, aliyewatia adui zako mikononi mwako. Abramu akampa fungu la kumi la vitu vyote,” Mwa 14:20 

naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu,” 1Kor 11:24 

Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu,” 1Kor 11:25

Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo,” 1Kor 11:26 

 “Akawaambia, Wapeni ninyi chakula. Wakasema, Hatuna kitu zaidi ya mikate mitano na samaki wawili, tusipokwenda tukawanunulie watu hawa wote vyakula,” Lk 9:13 

 “Wakala, wakashiba wote; na katika vile vipande vilivyowabakia walikusanya vikapu kumi na viwili,” Lk 9:17 

TAFAKARI: “Wapeni ninyi chakula.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha sherehe ya Mwili na Damu Takatifu ya Bwana wetu Yesu Kristo. Hiki ndicho kiini na uwepo halisi wa Kristo katikati yetu. Kwa uwepo wa Mwili na Damu ya Yesu, mimi na wewe tulio wafuasi wake waaminifu tunaunganishwa na kufungamanishwa na Upendo huu wa ajabu wa Bwana wetu Yesu Kristo. Sasa, basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti,” Rum 8:1-2. Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo ni chakula na Uzima wetu. Hii ndiyo Sakrameti Kuu ya Ekaristi Takatifu. Sherehe hii ya leo inaturudisha nyuma na kutafakari kwa undani siku ile ya Alhamisi Kuu ambayo ndiyo iliyokuwa siku rasmi kwa kusimikwa Sakramenti hii ya Ekaristi Takatifu.

Kwa maumbo haya ya Mkate na Divai, Mwili na Damu ya Yesu, Yesu Kristo ni uzima halisi. Kristo ni uzima halisi tunaposhiriki Ekaristi Takatifu katika mastahili yake. Yesu anatuambia, “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe” Yoh 6:35. Ni katika kula chakula hiki-mwili na damu yake,  Yesu anahaidi mambo mawili makuu: Moja, ni ufufuko siku ya mwisho. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:54. Na katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Kristo hukaa ndani yetu. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake,” Yoh 6:56. Hata hivyo Mtume Paulo anatupa angalizo la chakula hiki cha uzima. Naye anasema, Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana,” 1Kor 11:27. Yatupasa kuijongea Meza ya Bwana tukiwa na mastahili ya kufanya hivyo-usafi wa mwili na roho, yaani, pasipo hatia yoyote. Zaidi ya hapo ni kuikufuru Meza ya Bwana.

Wapendwa katika Kristo, jibu la Yesu kwa wanafunzi wake, “Wapeni ninyi chakula, Yoh 9:13,” kwenye Injili ya leo pale wanafunzi wake walipomwendea ili awaage makutano nao wapate muda wa kujitafutia chakula, liliakisi kile kilicho tokea siku ile ya Alhamisi Kuu, yaani wajibu (Mkleri) na kiini cha Sakramenti ya Daraja Takatifu. Hivyo ili kuwe na mwendelezo wa chakula hicho-Ekaristi Takatifu, Yesu aliisimika rasmi Sakramenti ya Daraja Takatifu siku hiyo ya Alhamisi Kuu na kuwaonyesha kiini chake, yaani, kuwa watumishi na kutumika vilivyo kwa upendo wa kimungu, kwa tendo lile la kuwaosha miguu wanafunzi wake. Yesu kwa jibu lake hili anaonyesha utashi wake ikiwa na kukubali kwamba kwa hitaji hilo walilokuwa nalo wanastahili chakula. Pili, anawataka kwanza Mitume wake watoe kile walichokuwa nacho na kukishirikisha kwa upendo.

Leo Mama Kanisa anaposheherekea Sikukuu hii ya Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo, tunakumbushwa pia wajibu na kiini cha Sakramenti ya Daraja Takatifu, vile vile bila kusahau ushiriki wetu katika ukuhani wa kawaida kwa kila Mbatizwa kwa Sakramenti ile ya Ubatizo (kupakwa mafuta Matakatifu ya Krisma, na kuunganishwa na taifa lake Mungu, kuendelea kuwa kiungo cha Kristo, kuhani, nabii na mfalme, hadi uzima wa milele Mbinguni). Kwa mantiki hiyo, Kanisa kama mwili wa Kristo uliojengwa na Wabatizwa wote, na Kanisa kama Sakramenti ya Wokovu, linawajibu wa kuwalisha chakula waamini wake, wale wote wenye hofu ya Mungu, na wale ambao bado hawajamjua Kristo.

Jamii inayotuzunguka licha ya itikadi zao za kidini, siasa, utamaduni na desturi, wana njaa ya mwili na roho. Kama Kanisa linalosafiri-Kanisa la hija, lililosheni watakatifu na wadhambi, ni wakati wa kutafakari kwa makini zile heri nane kama zilivyoandikwa na Mwinjili Mathayo 5:3-11, na kwa namna ya pekee mstari ule wa sita na tisa. “Heri wenye njaa na kiu ya haki; Maana hao watashibishwa. Heri wapatanishi; Maana hao wataitwa wana wa Mungu,” Mt 5:6,9. Jamii yetu ya leo ina njaa na kiu ya haki. Mtu katika ukamilifu wake ni mwili na roho. Mtu huyatamani yaliyo ya roho kama haya ya kimwili yapo sehemu yake na katika umaana wake. Hivyo, mtu na utu wake lazima uheshimiwe na kupewa stahili zake. Haki ya mtu kama tokeo la kuwajibika kwake lazima ilindwe na kutetewa kwa nguvu zote bila kupepesa macho. Ni kazi ya kila Mbatizwa kama Kanisa, na Kanisa kama Chombo na Sakramenti ya Wokovu, ‘kuwapa chakula’ katika maana ya kuamsha dhamiri zilizo lala, kuzijenga dhamiri zilizoharibiwa na kudumaa, na kuzifufua dhamiri zile zilizokwisha kufa, ile duniani hapa tunapoishi pale mahali salama kama sehemu pekee ya kujiandaa kwa maisha ya umilele.

Kila kukicha ulimwengu huu wa leo unapoteza usalama wake kwa sababu tu wapo watu wachache kwa ubinafsi wao (uroho wa madaraka) wanatumia vibaya uhuru na madaraka yao na kuzalisha machafuko. Katika eneo hili kila Mbatizwa anaalikwa kuulisha ulimwengu kuanzia pale alipo kwa kuwa mpatanishi. Kabla ya yote yakupasa kujipatanisha nafsi yako mwenyewe, wewe na jirani yako, wewe na mazingira yako, na wewe na Mungu. Upatanisho huu utuepusha na dhambi ya kijamii. Kwa kuishi na kufanya hivyo tunautendea haki ukuhani wetu wa kawaida, na unabii wetu. Nafasi uliyonayo leo kama Mkristo ni taa na nuru pale ulipo. Kristo ni kielelezo cha Nuru halisi kwetu licha ya kwamba walio wake, yaani, mimi na wewe kila siku tunamkataa. “Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua,” Yoh 1:10. Hivyo ndiyo maana ukuhani wa Kristo unafananishwa na ule wa Melkizedeki Mfalme wa Salemu. Historia yake haijulikani sana zaidi ya kile alichokifanya kama kuhani na Mfalme. Kumbe kwa muono huo mimi na wewe tunashirikishwa ukuhani wa Kristo bila kujali historia zetu wala makabila yetu. Sote tunaitwa kuhudumu na kuwa wahudumu ndani na katika Kristo. Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye juu sana,” Mwa 14:18. Kwa nafasi yake kama kuhani anamlisha Abramu kwa kumbariki. Akambariki, akasema, Abramu na abarikiwe na Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi,” Mwa 14:19. Na mwisho kwa uwepo wa Abramu anamsifu Mungu na kuwa mpatanishi kati ya Abram una maaduni zake kwa kuitafuta amani. Ahimidiwe Mungu Aliye juu sana, aliyewatia adui zako mikononi mwako. Abramu akampa fungu la kumi la vitu vyote,” Mwa 14:20.

Leo Kanisa linaposheherekea Sikukuu hii ya Mwili na Damu Takatifu ya Bwana wetu Yesu Kristo, tunakumbushwa kuwa wakarimu. Yakupasa kuwa mkarimu ukitambua thamani ya kukombelewa kwako. Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19. Kwa kutambua thamani hiyo, niwe mkarimu kuanzia pale nilipo ikiwa ni kwa wote wanaonizunguka. Niwe mkarimu na kujitoa katika Kanisa kwa vipaji vyangu na mali alizonijalia Mungu ili shughuli zake za kimisionari zisonge mbele na Kristo afikiwe kwa wate wote wenye njaa na kiu ya haki. Hivyo nikumbuke kuishi katika kiasi na kuwajali wengine.

Niepuke mara zote matumizi mabaya ya mali na kutapanya kile kilichozidi au baki baada ya kupata hitaji langu. Wakala, wakashiba wote; na katika vile vipande vilivyowabakia walikusanya vikapu kumi na viwili,” Lk 9:17. Vikapu kumi na viwili, ni idadi ile ya jumla ya makabila yale kumi na mbili ya Wayahudi, yaani wana wa Yakobo. “Basi hao wana wa Yakobo walikuwa kumi na wawili. Wana wa Lea ni Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, na Simeoni, na Lawi, na Yuda, na Isakari, na Zabuloni. Wana wa Raheli, ni Yusufu na Benyamini. Wana wa Bilha, kijakazi wa Raheli, ni Dani na Naftali. Wana wa Zilpa, kijakazi wa Lea, ni Gadi na Asheri. Hawa ndio wana wa Yakobo aliozaliwa katika Padan-aramu,”  Mwa 35:22b-26. Kumbe tukiwa wakarimu na kushirikishana kwa upendo yale tuliyojaliwa kwa ukarimu na Mungu, hakuna atakayekosa.

Tujifunze kutoka mshumaa. Mshumaa upiga vita giza (njaa na kiu ya haki), na wakati huo huo kutoa bila kujibakiza (kuepuka ubinafsi, uroho wa madaraka, kujilimbikizia na kuwa sababu ya machafuko). Kumbe mimi na wewe haitoshi kulalamika tu bila kufanya chochote ili hali twaweza kubadili hali pale ulipo na kwa nafasi uliyo nayo. Kama si umeme uwe mshumaa, na kama si ushumaa ule kijinga cha moto. Hakuna sababu ya kupiga kelele chumbani kuna giza tororo ilhali umeushika mshumaa. Washa mshumaa huo, na ingia chumbani. Kuwa nuru na mwanga pale ulipo. “Wapeni ninyi chakula.”

Tumsifu Yesu Kristo!

Wakala, wakashiba wote; na katika vile vipande vilivyowabakia walikusanya vikapu kumi na viwili,” Lk 9:17


Tusali:-Ee Yesu, nifundishe ukarimu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario