domingo, 15 de mayo de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 7 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 7 YA MWAKA-C
Somo: Yak 4:1-10
Zab: 55:7-8, 9-10a, 10b-11a, 23
Injili: Mk 9:29-36
Nukuu:
Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi!” Yak 4:2 

Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3 

Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu,” Yak 4:4

Lakini hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema, Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu,” Yak 4:6 

Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia,” Yak 4:7 

Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili,” Yak 4:8 

Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu,” Yak 4:9 

 “Kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akawaambia, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka,” Mk 9:31 

 “Akaketi chini, akawaita wale Thenashara akawaambia, Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote,” Mk 9:35 

TAFAKARI: “Hofu ya Mungu, maisha ya sala na maombi.”

Wapendwa wana wa Mungu, kufanikiwa katika maisha yanayoongozwa na malengo, ni kuishi maisha yanayosukumwa au kuongozwa wakati wowote na hofu ya Mungu, sala na maombi. Maisha yenye mtazamo huu kwa ujumla wake utufikisha kwenye kusudio la maisha ya kiroho. Kuongozwa au kusukumwa na hofu ya Mungu uturejesha kwenye kusudio la uumbaji wetu, na hali yetu halisi, yaani, ubinadamu wetu. Hofu hii ya Mungu umulika na kutukumbusha kila mara kusudi la kuumbwa kwetu, yaani, tumjue Mungu, Kumb 6:5, tumpende Mungu na majirani zetu, Mt 22:29, kumtumikia Mungu na wale tuliopewa dhamana juu yao, Gal 5:13, na mwisho tuupate uzima wa milele. Hii ni hatua ya mwisho kama asemavyo Mtume Paulo katika kuvipiga vita vile vya imani hapa dunia, yaani, “mkiisha kuwekwa huru, na kuwa mbali na dhambi, na kufanywa watumwa wa Mungu, mnayo faida yenu, ndiyo kutakaswa, na mwisho wake ni uzima wa milele,” Rum 2:22. Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, hayo ndiyo maisha yanayoongozwa au kusukumwa na hofu ya Mungu.

Ndugu yangu, hatutaweza kuifikia hali hiyo kama tutabebwa na wimbi la dunia tunaloishi leo kama litakavyo. Tunaishi katika ulimwengu wa ushindani, na wakati mwingine pasipo washindani au washindaniwa. Ni ulimwengu wa vitu, na utafutaji wa  vitu kila siku hata kama havina tija leo na kwa sasa. Mtindo na mtazamo huu wa maisha huaribu na upoteza lengo na sababu ya kuumbwa kwetu. Hofu ya Mungu hutoweka, na maisha ya sala na maombi hukosa ladha yake, kama Mtume Yakobo asemavyo, Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi!” Yak 4:2. Maisha yenye msukumo huu kamwe mbele ya safari hayana ushindi. Ni kushindwa tu! Ni maisha yaliyokosa malengo. Na ndiyo maana kama asemavyo Mtume Yakobo, hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3. Tunaomba vibaya na kuvitumia vibaya kwa sababu maisha yamepoteza shabaha yake, yaani uzima wa milele. Ni maisha bila hitimisho ambalo kwa uhakika lipo, yaani, maisha ya umilele.

Ndugu yangu, ni kweli pasipo shaka kabisa kwamba usipo thamini umilele kama hitimisho la maisha yako, nguvu na akili zako zote zitajikita kwa haya ya leo na kesho ambayo kwa uhakika kama yalivyo hayana umilele. Katika kweli hii Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako,” Mt 6:19-21. Ndugu yangu, chunguza kile kinachochukua muda wako mwingi hapa duniani na ujiulize kama kina uhusiano na umilele wako mara baada ya maisha haya hapa duniani.

Wapendwa wana wa Mungu, Yakobo Mtume anatupa karipio zito pale tunapokosa mwelekeo sahihi wa maisha ya hapa duniani, na uhusiano wake, yaani, maisha ya milele. Na kwa sababu hiyo anasema, enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu,” Yak 4:4. Ndugu yangu, tukiwa na uadui na Mungu kuna kushinda kweli vita hiyo? Hakika hakuna kushinda! Hivyo pamoja na raha na anasa zake mwisho wa siku hakuna faida yoyote. Basi kila mmoja na haihoji dhamiri yake kwa swali hili la Yesu kama anavyotuuliza, Kwa kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake?” Mk 8:36-37. Ndugu yangu, pasipo shaka sindano hiyo imekuingia vizuri. Tafakari!

Wapendwa wana wa Mungu, ili tufikie lengo la maisha ya kiroho twahitaji kuishi na kukumbatia muda wote fadhila ya unyenyekevu. Unyenyekevu uturudisha katika hali ya ubinadamu wetu pale tunapotaka kujiumba na kuvaa taswira nyingine kama tokeo la majivuno yetu, mafanikio yetu kimaisha, na hata ufahamu wetu. Ndugu yangu, chochote kile kitakachojiumba kama tokeo la kujikuza zaidi na kuipoteza ile hofu ya Mungu ndani yako, mwisho wake ni kupoteza dira ya hitimisho la maisha yako, yaani, umilele wake. Hofu hii ya Mungu, na kumtanguliza Mungu kwa kila jambo, hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema, Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu,” Yak 4:6. Ndugu zangu, tusipokuwa na hofu hii ya Mungu hatutaweza kumtii Mungu na wala kumkaribia kwa sababu Mungu hatakuwa na nafasi ndani ya moyo wako. Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia,” Yak 4:7. Na kwa namna hiyo hiyo Yakobo Mtume anatuambia,  mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili,” Yak 4:8. Hili litawezekana tu pale tutakapokuwa tayari kujinyenyekesha na kuiishi hofu ya Mungu. 

Wapendwa katika Kristo, maisha ya unyenyekevu na hofu ya Mungu hayatupeleki tu karibu na Mungu, bali utufanya kuwa tayari kutahabikiana katika hali zote za maisha na mahangaiko yake. Hivyo, huu ni mwaliko kwako na kwangu wa kufanya toba ya kweli na kumrudia Mungu. Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu,” Yak 4:9. Kujishusha huku ndiko kujidhili mbele za Mungu, naye atatukuza, Yak 4:10. Pasipo kujishusha ni vigumu kuyaona mahangaiko ya wengine na kuyabeba kama moja ya changamoto na misalaba yenye nuru ya Utukufu. Yesu anataka tulione jambo hili vizuri ikiwa yeye ndiye kielelezo chetu. Hivyo ni  “kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akawaambia, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka,” Mk 9:31. Hata hivyo Mwinjili Marko anatuambia hawakulifahamu neno lile kwa sababu walijawa na uoga na hivyo walishindwa kumuuliza Yesu, Mk 9:32

Ndugu yangu, kutokujishusha hakutatuandaa na kuwa tayari kutumika kwa ajili ya wengine. Je, kila mmoja wetu akiupenda ukubwa bila kutumika tutaepuka machafuko? Wanafunzi wa Yesu, yaani wale Thenashara, wanapatwa na ushindani huu wakiwa njiani wakipita katikati ya Galilaya na Yesu, Mk 9:34. Yesu anawaambia kiini cha ukubwa huo wanaoutamani. Akaketi chini, akawaita wale Thenashara akawaambia, Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote,” Mk 9:35. Ukubwa ni utumishi, na kutumika kweli kwa ajili ya wote pasipo kuweka mbele faida au maslahi binafsi. Huu ndio ule utumishi usio na faida kama anavyotuambia Yesu; “Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10. Hakika sote leo tuliopewa dhamana ya uongozi  katika nyanja mbalimbali katika Taifa letu- Tanzania, tungaliishi hofu hii ya Mungu na kweli katika hali ya kutumika, Kristo angeonekana kwa kila mtu.

Tusifu Yesu Kristo! 

Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote,” Mk 9:35b


Tusali: Ee Yesu Mwema, tujalie fadhila ya unyenyekevu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario