JUMATANO WIKI YA 9 YA MWAKA-C
Somo: 2Tim 1:1-3, 6-12
Zab: 123:1b-2ab, 2cdef
Injili: Mk 12:18-27
Nukuu:
“Namshukuru
Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile
nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana,” 2Tim 1:3
“Basi
usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake,
bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya
Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo
yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo
tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele,” 2Tim 1:8-9
“Kisha Masadukayo, watu wasemao ya kwamba hakuna kiyama,
wakamwendea, wakamwuliza na kusema, Mwalimu,
Musa alituandikia ya kwamba ndugu ya mtu akifa, akamwacha mkewe wala hana
mtoto, ndugu yake amtwae yule mkewe akampatie ndugu yake mzao,” Mk 12:18-19
“Kwa
maana watakapofufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika
walioko mbinguni,” Mk 12:25
TAFAKARI: “Kuna furaha ya kweli na heshima kuifia ‘kweli na haki’ kwa wajinga
ili waijue kweli na haki, kuliko kufa kama mfalme kwa pongezi na makofi ya
wapumbavu wadhanio kuijua ‘kweli na haki ilhali hawaijui na wao wenyewe
hawajijui.’”
Wapendwa wana wa Mungu, leo kuwa Mkristo kwa kubatizwa tu haitoshi. Leo
kuwa Mkristo kwakuitaji kuwa mpiganaji halisi wa Kristo kama Mfalme wa haki,
kweli, upendo, unyenyekevu, huruma, msamaha, na uwazi. Ulimwengu uliojaa
dhuluma, ufisadi, na matendo ya uvunjifu wa haki za binadamu, hauwezi kamwe
kuukubali Ufalme wa Yesu Kristo kama nilivyosema. Leo tulio wengi, yaani
Wakristo, tumewekwa katika kikaangio cha kukubaliana na mtazamo huo (dhuluma,
ufisadi, na uvunjifu wa haki za binadamu) au kuukataa kwa gharama kubwa sana
hata kuutoa uhai wako. Hakika njia iliyo rahisi na isiyo na mawaa ni kuusaliti
Ukristo (kumkana Kristo) wako kwa gharama nafuu kama alivyofanya Yuda Eskariote
kwa vipande thelathini vya fedha. Ndiyo maana leo wale tuliotegemea waseme na
kuukemea uovu wapo kimya, na wale waliojaliwa ufahamu wa kupembua mema na
mabaya wamekuwa wasaliti wa iliyo kweli na haki.
Ndugu yangu unayesafari nami katika tafakari hii, kuwa Mkristo leo ni
changamoto kubwa sana, kama ilivyokuwa kwake Yesu Kristo kuutangaza Ufalme
wa Mungu kwa Wayahudi kwa kauli mbiu
yake ile, yaani, “Wakati
umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili,” Mk 1:15.
Jamii ya Yesu wakati ule ilikuwa kama ndoto kuupokea ujumbe huu-kutubu na
kuiamini Injili. Je, katika hali hii, Yesu alirudi nyuma katika hili kwa vigezo
vya kutokukubalika? La hasha!
Kwa
kuushindilia msumari wa moto katika kusisitiza na kumaanisha asemacho, Yesu
aliwapa wapinzani wake silabasi ya utendaji wake kwa miaka ile mitatu. Naye
anasema juu ya utendaji wake kama ifuatavyo na itakavyokuwa: “Roho wa Bwana yu juu
yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma
kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha
huru waliosetwa, Na kutangaza
mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Silabasi hii ndiyo iliyokuwa hatma ya
kifo chake kila cha aibu, yaani, kifo cha Msalaba. Msukumo wa kifo hiki ni
Upendo na furaha ya kweli katika haki, kwa kujua kile akifiacho siyo kitu cha
kubumba bali ndio ukweli wenyewe. Yesu anakuwambia wewe na mimi, “Hakuna aliye na upendo
mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Bwana wetu Yesu Kristo amelifanya
hili, nasi kama wafuasi wake ni changamoto kubwa kwetu leo. Hakika Kristo
amekupenda wewe na mimi upeo, na kwa sababu hiyo alikuwa tayari na yupo tayari
hadi sasa kufa kwa ajili yako na mimi. “Basi,
kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika,
atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake katika
ulimwengu, aliwapenda upeo,” Yoh 13:1. Kwa
nini basi Mkristo mwenzangu unakuwa na imani ya mwono wa chura? Hivi leo
nikikuuliza uniambia ukweli kuhusu Chura ‘kama amesimama au kachuchumaa waweze
nipa jibu sahihi? Kigugumizi hiki cha kujua mkao wa Chura, ndicho kigugumizi
juu ya imani ya Wakristo wengi wa leo.
Wapendwa wana wa
Mungu, yote niliyoyasema ni kukuandaa ili uzame vizuri katika tafakari ya leo na
kadiri ya masomo yake. Mtume Paulo licha ya changamoto alizozikuta baada ya
kuongoka kwake, hakuwa tayari kubadilishwa na mtazamo wa wakati wake na
kujivika koti la uovu. Haki na kweli ndani na katika Kristo Yesu ilibaki kuwa
msingi wa imani yake. Hivyo Barua yake ya pili kwa Timotheo anapenda wafahamu,
na tufahamu kiini na msimamo wa imani yake. Naye anasema, “Namshukuru
Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile
nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana,” 2Tim 1:3.
Anaye kumbukwa hapa bila shaka ni Timotheo mwenyewe aliye mfano halisi wa kweli
na haki katika jumuiya yake. Leo mambo hayako hivyo hata kidogo. Baadhi yetu
kama viongozi wa dini, na wenye kuijua iliyo kweli, na hata kama hatuiamini kwa
kupitia utaratibu uliowekwa kwa taasisi husika kama hatua ya kuhesabiwa haki ya
kuwa kile ulicho, tumekuwa waogeleaji wa kufuata mawimbi ya maji bila kujali
ustadi wa kuogelea kwetu tukitazama ng’ambo ile na iliyo salama tunayotamani
wote kuifikia. Hapa ndipo penye chimbuko la unafiki. Hapa ndipo kwa makusudi
makubwa kabisa katika fikiri, amua na tenda yetu, wafuasi wetu hutushangaa kwa
kwenda kinyume kabisa cha matazamio ya kweli ile tunayoihubiri na matamanio
yake. Hapa ndipo tunapoonekana si tu vituko, bali watu tusiokuwa na maono na
uelewa wa kile tukisemacho, na mwisho kuutabiri unabii tusioujua ili tuenende
na mawimbi ya nyakati zetu tusiyoyajua.
Mkristo mwenzangu,
niyasemayo siyo mageni mbele ya macho yako. Manabii hawa wa kubumba hawaoni
shaka wala haya hata kidogo leo kusema Edgar ndiye “chaguo lile la Mungu” leo
kwa watu wa Mungu. Je, kwa nini wanasema kama wasemavyo? Je, wanajua kile
walicho na yale waliyoyalia kiapo kwa ajili ya taifa la Mungu? Kwa nini basi
wanadanganyika kiasi hicho? Je, wanaifahamu karama ya Mungu ndani ya maisha na
utume wao? Mtume Paulo anamwambia Timotheo hivi, “Kwa sababu hiyo
nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono
yangu,” 2Tim 1:6. Kutokuchoka maana yake, usitafute urahisi wa jambo na kuutafsiri
vinginevyo na karama uliyonayo kwa kuyaona mawimbi ya muda tu katika wakati
wako. Kwa maana nyingine, palipo na giza tusema giza, na tufanye kadiri iwezekanapo
kuuleta mwanga, na palipo mwanga tusema mwanga na uutetee mwanga huo ili udumu.
Kwa nin basi katika hali hii twaingiwa na woga? Kwa nini tunakufa gazi pasipo ganzi? “Maana
Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,”
2Tim 1:7. Katika mazingira ya utata kama huu tufanye nini?
Wapendwa wana wa Mungu,
katika mazingira na utata kama huo yatupasa kusimama katika kweli, hata kama nikibaki mwenyewe. Yesu Kristo kwa
kutambua ugumu huu anakuambia wewe na mimi leo kwamba, “tena
mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa
huru kweli kweli.” Yoh 8:32, 36. Mwana anatuweka huru, unapokuwa tayari
kujiachia katika minyororo ya upumbavu kwa kuwa tayari kujifunza na
kumsikiliza. Hii ndiyo habari njema ya wokovu, yaani, kulisikia neno, kulipokea
neno, kulitafakari neno, kulishirikisha neno, na kuwa shuhuda ya neno hilo kwa
maisha yako ya kila siku. “Basi
usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake,
bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya
Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo
yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo
tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele,” 2Tim 1:8-9. Je, hili lasema lolote
juu ya maisha yako kama Mkristo leo?
Leo mimi kama mfuasi wa
Kristo na muhudumu wake wa karibu, habari njema ya wokovu, yapaswa kuwa kipaua
mbele changu. Na habari njema ya wokovu kwa ufupi kabisa ni kulishinda giza
(dhambi) kwa kuukumbatia mwanga (utakatifu). Kwa habari hii njema ya wokovu, “inadhihirishwa
kwa kufunuliwa kwake Mwokozi wetu Kristo Yesu; aliyebatili mauti, na kuufunua
uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili; ambayo kwa ajili ya hiyo
naliwekwa niwe mhubiri na mtume na mwalimu,” 2Tim 1:10-11. Leo mimi kama mfuasi
wa Kristo, na kwa upekee kama mhudumu wa karibu (Mkleri), bila kuijua habari
njema, na kusoma alama za nyakati kadiri ya habari njema ile, ufuasi wangu na
ukaribu wangu hautakuwa na mguso wowote kati ya kile nilicho na ushuhuda ule
nipasao kuutoa. Nitabaki kuwa tukio kama utaratibu wa kawaida bila historia
kama sehemu ya mang’amuzi. Ndugu yangu, unakuwa historia kama sehemu ya mang’amuzi
unapoyachukulia yale yaliyotokea katika maisha yako, ukitazama kule unapokutamani
kama hitimisho la kila kitu. Hapa tumaini lipo hata kama linachelewa au
kucheleweshwa. Hapa ndipo mateso kama matukio katika maisha ya kila siku
yanapata maana kama asemavyo Mtume Paulo, kwamba, “Kwa sababu hiyo
nimepatikana na mateso haya, wala sitahayari; kwa maana namjua yeye
niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana
kwake hata siku ile,” 2Tim 1:12. Hapa siku ‘ile’ ya maanisha ‘uzima ule wa
milele’ tunao utamani.
Ndugu yangu,
kutokuyaona maisha katika mtazamo huu wa umilele, ni tatizo kubwa sana leo, na
hasa katika jamii yetu ya Tanzania ambayo kwa kiasi kikubwa tunaishi katika
ulimwengu wa kufikirika na usiowezekana. Leo wengi tumeaminishwa uongo, na
tumeupokea uongo huo kuwa ndiyo kweli. Hili ndilo analojaribu kulibadili Yesu
katika akili za watu kwa nyakati zake zile na mazingira yake, na hasa kuhusa swala
la kiyama. “Kisha Masadukayo, watu wasemao ya kwamba hakuna
kiyama, wakamwendea, wakamwuliza na kusema, Mwalimu,
Musa alituandikia ya kwamba ndugu ya mtu akifa, akamwacha mkewe wala hana
mtoto, ndugu yake amtwae yule mkewe akampatie ndugu yake mzao,” Mk 12:18-19.
Yesu Kristo haoni haya kusema lililo kweli na haki hata kama jambo hili
limeaminika kuwa kweli ilhali kweli haipo ndani yake. Kristo anatutaka
tutofautishe maisha tunayoishi leo na sasa, na maisha yale tutakayoishi mara
baada ya kifo chetu. Maisha ya ufufuko,
yaani, maisha baada ya kifo, ni tofauti kabisa, kwa sababu tutakuwa na miili
tofauti na hitaji tofauti. Miili tutakayokuwa nayo ni miili iliyotakatifuzwa,’
na isiyo shikiliwa au zuiliwa na ‘muda na nafasi.’ Ni miili iliyo huru kwa kila
jambo na katika kweli na haki, na yote katika utukufu wa Mungu.
Na kwa
namna hiyo Yesu anasema, “watakapofufuka
katika wafu, hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika walioko mbinguni,”
Mk 12:25. Tunaoa au kuolewa kwa sababu tupo chini ya shikamanizi la muda na
nafasi. Ndugu yangu, katika egesho au kipimo muda na nafasi, hatuna chaguzi
nyingine zaidi ya kile kilichopo katika kipimo hicho. Kumbe maisha ya ufufuko
ni tofauti kabisa. Katika kweli hii Yesu anatutaka tujue hili, kwamba, “kwa
habari ya wafu ya kwamba wafufuliwa, hamjasoma katika kitabu cha Musa, Sura ya
Kijiti, jinsi Mungu alivyomwambia, akisema, Mimi ni Mungu wa Ibrahimu, na Mungu
wa Isaka, na Mungu wa Yakobo?” Mk 12:26. Huyu Mungu kwa lugha nyepesi ni Mungu
aliye hai, na hai kwa kila kitu. “Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Hivyo
mwapotea sana,” Mk 12:27. Tunapotea pale tunapomwona Mungu kama mfu kadiri ya
ubinadamu wetu. Mungu wetu ni mwanzo na mwisho, Alfa na Omega, Ufu 22:13.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Kwa
sababu hiyo nimepatikana na mateso haya, wala sitahayari; kwa maana namjua yeye
niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana
kwake hata siku ile,” 2Tim 1:12
Tusali:-Ee
Yesu, nijalie niwe kielelezo chako halisi popote pale nitakapokuwa, na iwe
sehemu ya ushuhuda wangu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario