domingo, 8 de mayo de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 7 YA PASAKA

JUMATATU WIKI YA 7 YA PASAKA
Somo: Mdo 19:1-8
Zab: 68:2-3ab, 4-5acd, 6-7ab
Injili: Yoh 16:29-33
Nukuu:
Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu,” Mdo 19:4

Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri,” Mdo 19:6

Basi wanafunzi wake wakasema, Tazama, sasa wasema waziwazi, wala huneni mithali yo yote,” Yoh 16:29

Tazama, saa yaja, naam, imekwisha kuja, ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami,” Yoh 16:32

Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu,” Yoh 16:33

TAFAKARI: “Kuongozwa na Roho Mtakatifu.”

Wapendwa wana wa Mungu, Roho Mtakatifu hakuwahi kuliacha Kanisa lake tangu zama hizo. Roho Mtakatifu amekuwa kielelezo cha yale yote tuyafanyayo kuliendeleza na kulijenga Kanisa la Kristo pale ambapo Kristo hajajulikana. Roho Mtakatifu amekuwa muhimili mahiri kabisa kuliongoza na kulitakasa Kanisa nyakati za matatizo na migogoro iliyoibuka kwa sababu mbalimbali katika historia ya Kanisa. Roho Mtakatifu aliwaongoza vyema Mitume, Mababa wa Kanisa, na katika shughuli za kimisionari, maamuzi mbalimbali na mafundisho sahihi yaliyokuwa yakifanyika katika mitaguso mbalimbali katika historia ya Kanisa.

Leo kwa namna ya pekee tunasukumwa na neno hili katika tafakari yetu; “kuongozwa na Roho Mtakatifu.” Kuongozwa na Roho Mtakatifu ni kuomba mapaji yake saba ambayo kwayo kwa kuyaishi ni utimilifu wa yale aliyokusudia Mungu kwetu, na ukamilifu wa yale tunayoyatamani katika uzima wa milele. Mapaji hayo ni kama ifuatavyo; Hekima, Akili, Ushauri, Nguvu Elimu, Ibada na Uchaji. Mapaji haya yote yanalenga kumfahamu Mungu, na kuishi katika kweli yake. Tukimfahamu Mungu na kuishi katika kweli yake, maisha yetu hapa duniani yanapata malengo yake halisi, yaani kuelekea uzima wa milele.

Ni kwa sababu hii, Mtume Paulo anawauliza Waefeso, kama walipokea Roho Mtakatifu walipoamini, na walibatizwa ubatizo gani. Maswali haya mawili yana maana sana. Kama tunaimani bila kumpokea Roho Mtakatifu tunaupungufu wa mapaji yake ambayo ndiyo kielelezo sahihi cha kumjua Mungu na kuishi katika kweli yake. Kwa maana hiyo, kama hili halipo, basi hata malengo ya maisha yetu hapa duniani yanakosa mwelekeo sahihi. Jibu la Waefeso ni kwamba hawajawahi kusikia kuhusu Roho Mtakatifu, na ubatizo walioupata ulikuwa wa Yohane Mbatizaji.

Mtume Paulo anatoa ufafanuzi wa ubatizo huo wa Yohane kwa kusema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu,” Mdo 19:4. Ubatizo huu ulikuwa maandalizi ya kumtambulisha na kumwamini yule atakaye kuja baada ya Yohane, ambaye ni Yesu Kristo. Yesu Kristo ndiye ufunuo halisi wa Mungu Baba, na kwa maana hiyo, Yesu anasema, Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasheni habari,” Yoh 16:15. Jambo hili ndilo analojaribu kulisema Yohane, kwamba ukamilifu wa tendo analolifanya yaani ubatizo huo wa toba litakamilishwa na Yesu Mwenyewe.

Mtume Paulo analikamilisha lile lililokamilishwa na Kristo kwa Sakramenti hii ya Ubatizo kwa kuwawekea mikono juu yao. Hivyo, “alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri,” Mdo 19:6. Tunaona baada ya Roho Mtakatifu kuwa ndani yao, mapaji yake yanajionyesha mara kwa kuanza kunena kwa lugha na kutabiri. Haya ni matunda ya Roho Mtakatifu kwa wale aliowaridhia.

Ni ukweli usio shaka kwamba Mitume hawakufahamu ukweli aliokuwa akiuongelea Yesu alipokuwa akisema ‘Bado kitambo kidogo nanyi hamnioni; na tena bado kitambo kidogo nanyi mtaniona,’Yoh 16:16.  Kwa sasa Mitume wanaufahamu ukweli aliokuwa akiusema Yesu. Basi wanafunzi wake wakasema, Tazama, sasa wasema waziwazi, wala huneni mithali yo yote,” Yoh 16:29. Roho huyu Mtakatifu ndiye atakayetufunulia yale tusiyojajua. Tazama, saa yaja, naam, imekwisha kuja, ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami,” Yoh 16:32. Roho Mtakatifu ndiye mfariji wetu, kwani Kristo kesha ushinda ulimwengu. Ulimwengu huu tutapata matatizo ila Roho Mtakatifu atatufunulia yale yaliyojificha. Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu,” Yoh 16:33. Wapendwa, tumwombe Roho Mtakatifu na kutushushia mapaji yake saba ili tuzaliwe upya ndani yake.

Tumsifu Yesu Kristo!

Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri,” Mdo 19:6


Tusali:- Ee Roho Mtakatifku, utushushie mapaji yako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario