lunes, 23 de mayo de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 8 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 8 YA MWAKA-C
Somo: 1Pet 1:10-16
Zab: 98:1, 2-3ab, 3cd-4
Injili: Mk 10:28-31
Nukuu:
Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo,” 1Pet 1:13

 “kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu,” 1Pet 1:16

“Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele,” Mk 10:29-30 

Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho; na wa mwisho watakuwa wa kwanza,” Mk 10:31. 

TAFAKARI: “Kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.”

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na ukweli kwamba tupo hapa duniani kwa muda mfupi, je, inatosha kuridhika na hali hiyo na kutokufanya chochote? La hasha! Uchache wa muda wetu hapa duniani unasema zaidi kuhusu thamani ya maisha yetu, na kila mmoja kadiri ya wito wake. Kumbe licha ya mahali hapa-duniani kuwa ni sehemu pekee ya maandalizi ya maisha yale ya umilele, muonekano huo unatukumbusha kwamba maisha ni dhamana. Maisha ni dhamana tukiutazama ‘Utakatifu’ ambao ndio kikomo cha zawadi hii ya uhai tuliopewa na Mungu. Furaha ya Mungu ni sisi kuwa Watakatifu kama Yeye alivyo Mtakatifu, kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu,” 1Pet 1:16. Hivyo tungali tunaishi leo na sasa na katika uchache wa miaka yetu hapa duniani, tuelewe maisha ni dhamana tukiutazama ule utakatifu na umilele wa maisha mara baada ya maisha ya hapa duniani.

Utakatifu tunaoutamani unatukumbusha na kutuwajibisha kupungua kila siku ili Kristo aongezeke katika maisha yetu bila kupoteza au kusahau kile ulichoitwa kufanya hapa duniani katika uchache wa miaka hiyo. Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo,” 1Pet 1:13. Utakatifu huu tunaoutamani unatutaka na kutuwajibisha kuvishinda vilema vyetu kila siku kwa kulenga ukamilifu. Licha ya udhaifu tulionao kama wanadamu kamwe tusijifananishe na udhaifu huo kwa sababu Mungu kwa kutuumba kwa sura na mfano wake anatuwazia mambo makubwa kila siku. Na kwa sababu hiyo, Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu,” 1Pet 1:14. Mungu hakutuumba na kutuacha tujiendee wenyewe kama mwendo wa saa ya mshale. Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11. Tumaini hilo la siku za mwisho ni hili: kama yeye aliyewaita alivyo Mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote,” 1Pet 1:15, ili tuweze kuurithi uzima wa milele. Hakuna maisha ya umilele pasipo ‘Utakatifu’ kwa sababu alipo Mungu Mtakatifu katika makao yake ndipo ulipo Utakatifu kwa sababu yeye ni Mtakatifu. Je, utawezaje kuwa na Mungu Mtakatifu katika makao yake bila wewe kuwa Mtakatifu?

Wapendwa wana wa Mungu, safari ya kuelekea taji lile la ‘utakatifu’ inatutaka sadaka iliyo hai na yenye kumpendeza Mungu. Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana,” Rum 12:1. Sadaka hii kama sehemu ya maisha yako kila siku itoe pasipo manung’uniko, marejesho, na wala malinganisho. Sadaka yako iwe ya thamani na ya pekee kwa Mungu kama shukrani kwa sadaka ile ya Yesu Kristo pale Msalabani yenye thamani kubwa kupita sadaka zote. Hakika niutazamapo Msalaba na kuutafakari nagundua nimekombolewa na kununuliwa kwa thamani kubwa sana! “Wala ninyi si mali yenu wenyewe; maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu,” 1Kor 6:19b-20.

Bwana wetu Yesu Kristo anakutaka wewe na mimi tusifanye marejesho, au malinganisho, na wala manung’uniko utoapo sadaka ya maisha yako kwake na kwa Injili, yaani, Habari Njema ya Wokovu wetu. “Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele,” Mk 10:29-30. Yesu Kristo kama alivyomwondolea mashaka Petro ndivyo hivyo hivyo anavyokuondolea mashaka wewe na mimi tutoapo sadaka ya maisha yetu kwa ajili yake na Injili. Hivyo licha ya kuyapata haya ya leo na sasa kadiri ya hitaji letu,  tuna hakika ya uzima wa milele ndani na katika Kristo.

Ndugu yangu, kujitoa sadaka ya maisha yako kwa ajili ya Kristo na Injili kwahitaji fadhila ya unyenyekevu. Hapa ndipo kwenye kushushwa na Kristo pale unapojipandisha mwenyewe na pasipo haki, na kupandishwa na Kristo pale unapojishusha kwa kumpa nafasi Kristo ndani ya maisha yako. Kwa maana hiyo, wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho; na wa mwisho watakuwa wa kwanza,” Mk 10:31. Hii ndiyo changamoto kubwa katika maisha yetu ya kiroho.

Ukimruhusu Yesu Kristo ndani ya maisha yako uwe tayari kuyapokea yote kama alivyoyapokea Kristo hadi kuwambwa pale Msalabani. Utatemewa mate, utachekwa, watakushangaa, utakejeliwa, utazushiwa, utashangiliwa, utaonewa huruma, na mwisho utawambwa kama utimilifu wa sadaka ya maisha yako kwa Kristo na Injili. Haya ndiyo maisha ya utauwa.  Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa,” 2Tim 3:12. Kwa maana nyingine hii ndiyo heri ile ya kuishi umasikini wa roho, Mt 5:3, kwa kumpa Yesu Kristo nafasi ndani ya maisha yako, na mwisho wa siku kuupata Ufalme wa Mbinguni. Ni kama asemavyo Mtume Paulo kwamba,  “Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote,” 1Kor 15:19. Ni umasikini kwa kupungua ili Kristo Yesu apate nafasi ndani ya maisha yako, nawe uwe na furaha isiyo na kipimo. Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna awaondoleaye,” Yoh 16:22. Wapendwa nani kama Yesu Kristo? Hakuna!

TumsifuYesu Kristo!

Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho; na wa mwisho watakuwa wa kwanza,” Mk 10:31.


Tusali:-Ee Yesu Mwana wa Mungu uliye hai, nifundishe kutii hata pale penye shaka katika kutii, kama ulivyotii Wewe pasipo shaka hadi mwisho kwa kutukomboa sisi na ulimwengu nzima. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario