Sikukuu ya
MTAKATIFU MATHIYA Mtume
14/5
Somo:
Mdo 1:15-17, 20-26
Zab:
113:1-2, 3-4, 5-6, 7-8
Injili:
Yoh 15:9-17
Nukuu:
“Basi
katika watu waliofuatana nasi wakati wote Bwana Yesu alipokuwa akiingia na
kutoka kwetu, kuanza tangu ubatizo wa Yohana, hata siku ile
alipochukuliwa kwetu kwenda juu, inapasa mmoja wao awe shahidi wa kufufuka
kwake pamoja nasi,” Mdo 1:21-22
“Kisha
wakaomba, wakasema, Wewe, Bwana, ujuaye mioyo ya watu wote, tuonyeshe ni nani
uliyemchagua katika hawa wawili, ashike mahali katika huduma hii na
utume huu, alioukosa Yuda, aende zake mahali pake mwenyewe,” Mdo 1:24-25
“Wakawapigia
kura; kura ikamwangukia Mathiya; naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na
mmoja,” Mdo 1:26
“Kama
vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo,”
Yoh 15:9
“Mkizishika
amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za
Baba yangu na kukaa katika pendo lake,” Yoh 15:10
“Amri
yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” Yoh 15:12
“Hakuna
aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya
rafiki,” Yoh 15:13
“Siwaiti
tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi
nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu,” Yoh
15:15
“Si
ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka
mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote
mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Yoh 15:16
TAFAKARI: “Amri
yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” Yoh 15:12
Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa
anaadhimisha Sikukuu ya Mtume Mathiya. Tukumbuke kwamba Mitume waliochaguliwa
na Yesu walikuwa kumi na mbili, na kufanya lile kundi lililokuwa karibu sana na
Yesu, yaani Thenashara-kumi na wawili. Baada ya Yuda Iskariote kumsaliti Yesu
na kujinyonga kundi hili la Mitume likawa na upungufu wa mmoja. “Yesu
akawajibu, Je! Mimi sikuwachagua ninyi Thenashara, na mmoja wenu ni shetani?”
Yoh 6:70. Hivvo Mitume kwa umoja wao wanao waliona ni vyema kumchagua mmoja
mwenye sifa zifuatazo; “Basi
katika watu waliofuatana nasi wakati wote Bwana Yesu alipokuwa akiingia na
kutoka kwetu, kuanza tangu ubatizo wa Yohana, hata siku ile alipochukuliwa
kwetu kwenda juu, inapasa mmoja wao awe shahidi wa kufufuka kwake pamoja nasi,”
Mdo 1:21-22
Baada ya vigezo na masharti kuzingatiwa
kwa kina, walipatikana watu wawili, yaani, Barsaba na Mathiya. Hatua ya pili
kabla ya kufanya uchaguzi, waliwaweka katika maombi kwa kuwakabidhi kwa Bwana
Yesu Kristo awapatie yule atakaye fuata nyayo zake kimamilifu. Hivyo, “wakaomba,
wakasema, Wewe, Bwana, ujuaye mioyo ya watu wote, tuonyeshe ni nani
uliyemchagua katika hawa wawili, ashike mahali katika huduma hii na
utume huu, alioukosa Yuda, aende zake mahali pake mwenyewe,” Mdo 1:24-25.
Baada ya hatua hii ya
maombi, ilifuata hatua ya tatu yaani kupiga kura. “Wakawapigia kura;
kura ikamwangukia Mathiya; naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na
mmoja,” Mdo 1:26. Mathiya akachukua ile nafasi iliyokuwa wazi baada ya kifo cha
kujinyonga cha Yuda Iskariote,
aliyemsaliti Bwana wetu Yesu Kristo. Tangu nyakati hizo, Kanisa limekuwa
likifuata taratibu hizi hasa pale ambapo mmoja wa maaskofu kufariki, au
kustaafu, au kutokana na hitaji la mchungaji mkuu, yaani Askofu.
Wapendwa, mambo haya
yote Mama Kanisa anayafanya ili kuendeleza na kuuishi ule upendo aliyotuachia
Kristo. Upendo kwetu sisi wafuasi wake Kristo ni Amri. Mkristo bila upendo ni
kichokoo fulani hivi. Kama mchungwa unavyojulikana kwa matunda yake, hivyo
hivyo nasi kama wafuasi wake Kristo yatupasa daima kujulikana kwa upendo wetu
na jirani zetu. “Amri yangu ndiyo hii,
Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” Yoh 15:12. Kupenda huku kunaendana na kuishi katika kweli na
haki. Ukipenda kweli utaishi katika kweli, na kweli hiyo itakufanya utende haki
kwa wali unaoishi nao.
Kuishi katika hali hii ya upendo, ukweli
na haki, ndicho kitakachotutambulisha mbele za watu na hasa wale wasiomjua
Kristo. Leo sisi kama wafuasi wa Kristo tunasisitizwa sana kuishi ushuhuda wa
‘ukimya’ ambao unajidhihirisha zaidi kwa upendo, ukweli na haki. Ni ukweli
usiotia shaka kwamba wapo watu ambao leo hawataki kusikia kabisa neo ‘Yesu,’
‘Kristo,’ ‘Katoliki.’ Nasi hatuna sababu ya kuwalazimisha kuyasikia. Ila
tunaweza kuwafanya kuyaelewa maneno hayo tunapotoa ushuhuda wetu wa ukimya kwa
kupendana sisi kwa sisi, kuwapenda, kuwa wakweli, na kuwa watu wa haki kama
alivyo Kristo mwenyewe. Huku ndiko kuzishika amri za Kristo, na kumtambulisha kwa
wale wasiomjua na kumpenda au kutokutaka kumsikia. “Mkizishika amri zangu,
mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na
kukaa katika pendo lake,” Yoh 15:10
Wapendwa wana wa Mungu,
kukaa katika pendo la Kristo ni kuhesabiwa haki na Kristo mwenyewe. Kristo
hapendi kuwa mchoyo wa upendo huu na ukaribu aliokuwa nao na Baba Mungu. Kipimo
kile kile alichopendwa na Mungu Baba, ndicho kipimo hicho hicho anachotupenda
sisi. “Kama vile Baba alivyonipenda mimi,
nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo,” Yoh 15:9. Mfumo huu wa upendo,
makuzi na kukomaa kwake ni kujitoa sadaka kila siku. Kujitoa sadaka kwa ajili
ya upendo na kutambua upendo aliotupenda Kristo kama shukrani ya wokovu wetu.
Kielelezo cha upendo sadaka ni Kristo mwenyewe. “Hakuna
aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya
rafiki,” Yoh 15:13. Hapa ndipo tunapoona sababu ya kuumbwa wetu, na malengo ya
kuwa katika ulimwengu huu.
Ndugu yangu, haukuumbwa
kwa bahati mbaya, na usiyekuwa na malengo hapa duniani. Hapa hapa duniani kwa
misioni maalumu ambayo yakupasa kuitimiza kadiri ya vipaji na wito aliokujalia
Mungu. Kama utajua hupo hapa kwa misioni fulani unayotakiwa kuitimiza kila
unapojaliwa pumzi, huwezi kuchezea Muda wako hata kidogo. Hii ndiyo sababu
kubwa ya sisi kuitwa na Yesu marafiki zake. Ni marafiki zake kwa sababu anataka
muda wote kutumegea siri ya yale yaliyojificha ndani mwetu, maishani mwetu, na
kule tunakotamani kupajua na kufika. Hivyo Yesu anatuambia, “Siwaiti
tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi
nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu,” Yoh
15:15. Ni fuaraha kubwa sana kuwa marafiki wa Yesu. Tumethaminiwa sana kupewa
nafasi hiyo bure.
Uteuzi huu wa kuwa
marafiki wake Yesu unaonyesha ni kwa namna gani Yesu achoki kutufikiria.
Unapoelewa ukweli huu, huwezi hata mara moja kujisikia kutengwa na Yesu. Huwezi
hata mara moja kujisikia mpweke au kutokuwa na msaada pale unapokumbana na
matatizo. Hata kwenye matatizo hayo Kristo yupo. Lengo lake kubwa ni kukupata
na siyo kukupoteza. Tunaposafiri naye katika vilindi hivi vya matatizo na
mateso bila kukengeuka, utujaza neema na baraka kuyashinda matatizo na mateso
hayo. Katika hali hii, Mungu hatuondolei uhuru wetu wa kutokuamua na kufanya
vingine. Anatutaka tuwe huru na si watumwa. Tumfuate kwa uhuru wetu na kweli.
Anatutaka tuwe hivyo muda wote kwa sababu aliona hivyo kabla yetu. Hivyo Yesu
anasema, “Si ninyi mlionichagua mimi, bali
ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda
yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,”
Yoh 15:16
Wapendwa wana wa Mungu,
tukijua kiini hiki cha upendo wa Kristo ndani yetu, tutajua maana halisi ya
wajibu wetu kama wafuasi wake. Kama najua napendwa na Kristo kama Yeye
alivyopendwa na Baba Mungu, hivyo nami ili nizae matunda katika upendo huu wa
Kristo na Mungu Baba yanipasa kupenda bila kipimo. Je, nianzie wapi zoezi hili?
Anza hapo ulipo!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Si
ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka
mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote
mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Yoh 15:16
Tusali:
Ee Yesu, tuwashie moyo wa upendo wako, nasi tupendane kama ulivyotupenda. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario