martes, 17 de mayo de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 7 MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 7 YA MWAKA-C
Somo: Yak 4:13-17
Zab: 49:2-3, 6-7, 8-10, 11
Injili: Mk 9:37-39
Nukuu:
Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida,” Yak 4:13 

walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka,” Yak 4:14 

Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi,” Yak 4:15 

Lakini sasa mwajisifu katika majivuno yenu; kujisifu kote kwa namna hii ni kubaya,” Yak 4:16 

Basi yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi,” Yak 4:17

Yohana akamjibu, akamwambia, Mwalimu, tulimwona mtu akitoa pepo kwa jina lako, ambaye hafuatani nasi; tukamkataza, kwa sababu hafuatani nasi,” Mk 9:38 

Yesu akasema, Msimkataze, kwa kuwa hakuna mtu atakayefanya mwujiza kwa jina langu akaweza mara kuninenea mabaya; kwa sababu asiye kinyume chetu, yu upande wetu,” Mk 9:39-40 

TAFAKARI: “Yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi,”

Wapendwa wana wa Mungu, ni kweli ugonjwa wa Malaria na UKIMWI umekuwa tishio kubwa kwa afya na maendeleo katika Taifa letu la Tanzania kwa muda mrefu sasa. Maradhi haya yamekuwa huzuni na wakati mwingine sababu kubwa ya mahangaiko na mifarakano kifamilia, kiuko, na hata mahusiano ya karibu baina ya watu na ndugu. Pamoja na maradhi hayo niliyoyataja na mengine mengi tu yakiibuka kila kukicha, jamii yetu leo kama Watanzania imetikiswa na tunateketea kwa “Saratani unafiki.” Mtume Yakobo leo ameielezea kwa undani saratani hii unafiki. Ni hali ile ya kuujua ukweli/kweli lakini hutaki kufanya au kutenda kadiri ya kweli ile, na badala yake unafanya ndivyo sivyo ama kuwafurahisha watu, mtu (bosi wako), au itikadi fulani kadiri ya mfumo fulani usiopenda kweli na haki kwa sababu tu kulinda maslahi fulani tena ya wachache fulani tu.

Wapendwa wana wa Mungu na yeyote yule wenye hofu ya Mungu, unafiki huu kwa namna nyingine ni dhambi ya kijamii, yaani, “social sin.” Dhambi hii ndiyo ambayo Mtume Yakobo anasema, yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi,” Yak 4:17. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, nikuombe utazame hali halisi hapo ulipo (familia yako, jamii inayokuzunguka, kazini mwako, hali halisi na mazingira ya sasa ‘kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni, na kijami’) na ugonjwa huu hatari, yaani UNAFIKI. Je, wewe kama Baba au Mama katika familia yako, kiongozi wa serikari au dini wauona ukweli na kufanya kadiri ya kweli hiyo? Kama unaona na hufanyi dhamiri yako bado ipo hai? Na kama unaona kweli hiyo ila unafanya kinyume chake, je wamfurahisha nani? Je, wamjua unayetakiwa kumtumikia katika kweli na haki? Ndugu yangu, kama umepewa dhamana na umma wa watu na kwa nafasi hiyo unawaangamiza kwa maslahi niliyokwisha kuyasema hapo juu, muogope sana Mungu ukijua unawiwa deni kubwa kwa pumzi aliyokupa. Unafiki wa kiwango hiki huwezi kuwa na ujasiri wa kuyasema maneno haya mazito aliyoyatamka Mtume Paulo: “Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” Flp 4:12-13

Ndugu yangu, nafasi uliyo nayo, uwezekano ulio nao na dhamana uliyopewa ni kupigana kuliondoa giza la ujinga, chuki, umasikini wa watu na mazingira yao, uonevu na ukandamizaji wa hali za watu. Kwa namna nyingine hapo ulipo kuwa chumvi na mwanga kama Kristo Yesu anavyotusihi, kwamba, Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13. Tu chumvi katika jamii kwa kuuona ukweli, kuwa sehemu ya ukweli huo, na kuibadilisha hali ile isiyo ya kweli kwa kuleta ladha nzuri zaidi kama chumvi ifanyavyo. Tendo hili litakufanya uchanganyike na watu ili kuleta na kukoleza ladha hiyo, yaani, pale pasipo na haki, basi haki itendeke, pale pasipo na utu, basi utu uheshimiwe, pale palipo na ubaguzi, basi usawa uwepo, na pale palipo na chuki, basi upendo utawale. Huku ndiko kuona, kujua, kuguswa, kutenda, na kutetea kuliko kweli na haki kama alivyofanya na kutufundisha Bwana wetu Yesu Kristo. Na hili ndilo fumbo la “kuwa chumvi.” Hivyo chumvi ikikosa ‘uchumvi’ huu ni ‘kuputwa nje na kukanyagwa na watu,’ Mt 5:13b. Vita hii si rahisi. Gharama yake ni kubwa kama tusivyoweza kuutenganisha utukufu na msalaba. Hivyo yanipasa kuishinda hofu ili niwe mbali na unafiki na kutenda kweli na haki hata kama kwa kufanya hivyo itanibidi kutoa sadaka kubwa ya maisha yangu.

Wapendwa wana wa Mungu, tu mwanga kwa kuwa na kuishi maadili mema. Kila kazi au taaluma fulani ina maadili yake na miiko yake. Hivyo, kazi hiyo au taaluma hiyo ikipoteza nguvu yake ya kimaadili ni sawa kuendesha gari katika kiza kinene pasipokuwa na taa. Ni wazi katika hali hiyo lolote linaweza kutokea, na haliwezi kuwa jambo zuru katika usalama wako na chombo chako cha usafiri, yaani gari lako. Hivyo, Yesu anatuambia, Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote unao mwanga; lakini likiwa bovu, mwili wako nao una giza. Angalia basi, mwanga ulio ndani yako usije ukawa giza,” Lk 11:34-35. Mwaliko wa kuwa mwanga ni kutenda kimaadili katika uelekezi wa hofu ya Mungu ndani yetu. Tunakosa kuwa chumvi na mwanga tunapoikubali na kufifishwa na “Saratani unafiki.” Hapa ndipo penye chanzo na dhambi hii ya kijamii-“social sin.” Ndiyo maana kila kukichwa hatukosi kusikia habari za uovu uliokidhiri katika jamii yetu leo. Neno ‘kupiga dili, ufisadi, n.k,’ yanataka kuwa maneno ya kawaidi na sifa katika jamii. Wachache wetu kwa kuwezeshwa na mfumo tuliokuwa nao wamepata fursa ya kujineemesha na kuzikanyaka haki za walio wengi, masikini na wanyonge. Mitazamo na maisha ya wacheche hawa ni kama asemavyo Mtume Yakobo, Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida,” Yak 4:13. Kila kona ni ‘kupiga dili na harufu ya ufisadi.’ ‘Saratani unafiki’ inaangamiza Taifa la wana wa Mungu!

Jambo la kukumbuka kwa yeyote yule asiyependa kutenda lililo jema ilihali anajua, ajue kwamba maisha ya hapa duniani ni jukumu la muda mfupi. Kuishi na kutotambua ukweli huu ni kuishi bila kujua yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka,” Yak 4:14. Ndugu yangu, katika ulimwengu huu, mwanadamu hawezi kudumu milele katika fahari yake. Tupo kwa muda fulani tu, tena uliofichwa na Yule aliyetupa pumzi yaani Mungu. Jeuri yako na yangu inatoka wapi? Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi,” Yak 4:15. Tumekuwa watu wa kutamka maneno mazito utafikiri tu washauri wa Mungu! Kiburi chetu kinatoka wapi? Ndugu zangu,  Lakini sasa mwajisifu katika majivuno yenu; kujisifu kote kwa namna hii ni kubaya,” Yak 4:16. Tumwogope Mungu tukijua tu binadamu tu, na uhai wetu tumeazimwa kwa muda fulani tu. Ukweli ni ukweli tu hata ukisemwa na yule ambaye haendani na mitazamo yetu na itikadi zetu. Hiki ndicho anachokikemea Yesu kwa wanafunzi wake, na hasa pale Yohana anapotoa taarifa ya utume wao na kusema, “Mwalimu, tulimwona mtu akitoa pepo kwa jina lako, ambaye hafuatani nasi; tukamkataza, kwa sababu hafuatani nasi,” Mk 9:38. Hali hii ya “USISI” Yesu anaikemea kwa maelezo yafuatayo: Msimkataze, kwa kuwa hakuna mtu atakayefanya mwujiza kwa jina langu akaweza mara kuninenea mabaya; kwa sababu asiye kinyume chetu, yu upande wetu,” Mk 9:39-40. Kweli hubaki kuwa kweli hata ikisemwa au tendwa na yule au wale wasiofuata mitazamo na itikadi zetu. Je, tuyaonayo leo katika jamii yetu yanamulika fundisho hili la Yesu?

Tumsifu Yesu Kristo!

Yesu akasema, Msimkataze, kwa kuwa hakuna mtu atakayefanya mwujiza kwa jina langu akaweza mara kuninenea mabaya; kwa sababu asiye kinyume chetu, yu upande wetu,” Mk 9:39-40


Tusali: Ee Yesu, uliyesimama imara katika upendo, kweli, na haki hadi mwisho, tena mwisho katika kifo kile cha msalaba, nijalie neema na nguvu ya kuona, kujua, kuguswa, kutenda, na kutetea kuliko kweli na haki kama ulivyo ishi na kufia. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario