viernes, 20 de mayo de 2016

TAFAKARI: SHEREHE YA UTATU MTAKATIFU MWAKA-C

SHEREHE YA UTATU MTAKATIFU-C
Somo: Mit 8:22-31
Zab: 8:3-8 (K) 1
Somo II: Rum 5:1-5
Injili: Yoh 16:12-15
Nukuu:
Ndipo nilipokuwa pamoja naye, kama stadi wa kazi; Nikawa furaha yake kila siku; Nikifurahi daima mbele zake,” Mit 8:30 

Nikiifurahia dunia inayokaliwa na watu; Na furaha yangu ilikuwa pamoja na wanadamu,” Mit 8:31 

Basi tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika imani, na mwe na amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya imani kuifikia neema hii ambayo mnasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu,” Rum 5:1-2 

na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini; na tumaini halitahayarishi; kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi,” Rum 5:4b-5 

Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake,” Yoh 16:13

Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasheni habari,” Yoh 16:15 

TAFAKARI: Tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika imani, tu na amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, na Roho Mtakatifu tuliyepewa. Huu ndiyo Utatu Mtakatifu na umoja usiogawanyika.”

Wapendwa wana wa Mungu leo Mama Kanisa anasheherekea Sikukuu ya Utatu Mtakatifu. Jumapili iliyopita Mama Kanisa alisheherekea Sikukuu ya Pentekoste kama siku rasmi ya kuzaliwa kwake, yaani Kanisa. Sherehe ya Pentekoste, yaani kuvuviwa kwa Roho Mtakatifu kwa Kanisa na Waamini wake kunalifanya Kanisa kuwa chombo na Sakramenti ya Wokovu katika umoja usiogawanyika, yaani Mungu Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu. Na ndiyo maana agizo msingi la Yesu na kwa Kanisa baada ya Pentekoste ni kuuinjilisha ulimwengu wote, na kuwabatiza kwa Jina la Baba, na la Bwana, na la Roho Mtakatifu wale wote watakao upokea wokovu huo.

Leo kwa namna ya pekee tunaalikwa kuzama ndani zaidi juu ya Utatu Mtakatifu na Umoja huu usiogawanyika. Mpendwa tunayesafiri sote katika tafakari hii, ya kupasa kuelewa ukweli huu kwamba, Ukristo na tukienda ndani zaidi Ukatoliki kwetu, siyo tokeo la ugunduzi wa akili ya mwanadamu au wanadamu, bali ni dini ‘funuliwa’ na Mungu mwenyewe kwa watu wake na aliopendezwa nao. Hivyo ni zawadi ya Mungu mwenyewe aliyopenda kuwashirikisha watu wake. Ufunuo huu wa Mungu kwa watu wake umejidhihirisha kwa matukio mbalimbali katika historia nzima ya wokovu wa mwanadamu, yaani, Uuumbaji, Ukomboaji, na Utakatifuzwaji wa kile kilichoumbwa na kukombolewa. Hapa ndipo tunapoweza kuona Utatu huu Mtakatifu na Umoja huu usiogawanyika. Hivyo mwanadamu huyu aliye huru na bila kushurutishwa anao wajibu wa kuitikia ufunuo huu. Mwitikio huu wenye lengo la kuelewa siri na fumbo hili la ufunuo wa Mungu kwa watu wake ndiyo tunayoiita Teología-‘tahuidi ambayo imegawanyika katika matawi tofauti.’ Hata hivyo leo siyo lengo langu kuyaongelea mgawanyiko huo kiteologia.

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu yote matatu ya leo yanatutafakarisha na kutuwezesha kwa kiasi fulani kuuona Utatu huo Mtakatifu. Ni kuuona katika maana ya kutafakari, na siyo kuujua katika maana ya uhasili wake kwa sababu ni Fumbo. Utatu Mtakatifu ungekuwa ni ‘tatizo’ basi tungekuwa na jibu lake. Kwa vile Utatu Mtakatifu ni ‘fumbo’ hatuna jibu lake katika ukamilifu wake. Tunachojaribu kufanya ni kuueleza katika maana ya kuzama katika tafakari ya fumbo hilo. Na katika kuzama huko ndipo tunapozidi kufunuliwa siri hiyo. Ni Utatu Mtakatifu katika maana ya nafsi tatu: Mungu Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu. Ni umoja usiogawanyika katika maana Mungu ni mmoja. Tofauti ipo tu katika utendaji. Hata hivyo katika utendaji wa moja ya nafsi hizi tatu za Mungu, siyo kwamba katika tenda yake (nafsi moja)  hizo nafsi nyingine hazipo. La hasha!

Somo la kwanza linatupa jibu la utendaji huu katika kuifunua wazi nafsi moja, na wakati huo huo nyingine zikiwa katika utendaji uleule. Ndipo nilipokuwa pamoja naye, kama stadi wa kazi; Nikawa furaha yake kila siku; Nikifurahi daima mbele zake,” Mit 8:30. Ni wazi kazi ya uumbaji na inavyojionyesha imefanywa na Mungu-nafsi ya kwanza ya Mungu, ila hapo hapo nafsi ya pili ya Mungu, yaani Mungu Mwana kushiriki kwa kiasi kikubwa sana. Mwinjili Yohana anatuambia ukweli huu kwa kusema, Vyote vilifanyika kwa huyo (Mwana); wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Maneno “ndipo niliokuwa pamoja naye,” katika nukuu kutoka somo la kwanza yanaturudisha kwenye uhasili wa Neno kabla ya kumwilishwa na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Mwinjili Yohana katika hili anasema, Hapo mwanzo kulikuwako Neno (Mwana), naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu,” Yoh 1:1. Huu ni uthibitisho wa umoja usiogawanyika katika utendaji.

Neno, yaani Mwana nafsi ya pili ya Mungu, kufanyika mwili na kukaa kwetu ni tokeo la upendo usio na kipimo wa Mungu kwetu sisi wanadamu. Hii ndiyo furaha ya Mungu kama tulivyosikia kutoka somo letu la kwanza, kwamba, Nikiifurahia dunia inayokaliwa na watu; Na furaha yangu ilikuwa pamoja na wanadamu,” Mit 8:31. Mungu hakuwahi kutuacha hata mara moja tangu alipokusudia kutushirikisha furaha yake katika uumbaji wake. Furaha ya Mungu na mshikamano huu kwa viumbe vyake ulijidhihirisha kupitia nafsi ya pili ya Mungu, yaani Neno lile lililomwilishwa na kukaa kwetu-Yesu Kristo. Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele,” Yoh 3:16. Kumwamini Mwana wa Mungu si tokeo la akili na nguvu zetu, wala tokeo la kina kama sehemu ya tafakuri yetu. Kumwelewa Mwana wa Mungu tunawezeshwa na nafsi ya tatu ya Mungu-Roho Mtakatifu. Roho huyu Mtakatifu ni tunda la upendo wa Mungu Baba na Mwana. Hivyo Mtume Paulo anatuambia, “wala hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu,” 1Kor 12:3b. Roho huyu Mtakatifu anakazi ya kutuweka pamoja katika umoja aliyotuombea Mwana kabla ya kujongea kikombe kile cha mateso Yoh 17:11b, na kulitakatifuza Kanisa lake, yaani, wabatizwa wote.

Wapendwa wana wa Mungu, wewe na mimi leo tunauishi Utatu huu Mtakatifu na umoja usiogawanyika tunapoambatana pasipo kujipoteza katika malimwengu tukiwa ndani ya Utatu huu kila mmoja kadiri alivyoitwa kutumika hapa duniani kama viumbe shirikishwa katika uumbaji wa pili na Mungu-“co-creators of God.” Hivyo wito na maisha yako unayoyaishi kwa uaminifu ni kwa namna hiyo hiyo unashiriki fumbo hili Takatifu katika (kuumba, kikombo, na kutakatifuza malimwengu). Hapa ndipo twawezwa kuhesabiwa haki katika imani hiyo. Hivyo Basi tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika imani, na mwe na amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya imani kuifikia neema hii ambayo mnasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu,” Rum 5:1-2. Na kuishi Imani hii katika kweli, tumaini na haki, tunawezeshwa na Roho Mtakatifu tuliyepewa. Na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini; na tumaini halitahayarishi; kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi,” Rum 5:4b-5. Je, ninalo la kujivunia au kuona fahari juu ya kufunuliwa siri na fumbo hili la Utatu Mtakatifu na umoja usiogawanyika? Sina!

Ndugu yangu, sina cha kuona fahari isipokuwa jambo hili tu: “nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14. Kwa kupitia Msalaba huu Mtakatifu mimi na wewe leo tupo huru na kuhesabiwa haki kama wana na warithi wa Ufalme wa Mungu. Na kwa kutambua ukweli huu na kushikamana nao ndivyo hivyo hivyo Roho Mtakatifu utufunulia kweli yote ya mambo yale aliyotufundisha Kristo Yesu ikiwa ni pamoja na siri ya maisha ya umilele.  Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake,” Yoh 16:13. Hapa pia tunaona umoja usiogawanyika wa Utatu Mtakatifu. Kwa maana Yesu anasema, Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasheni habari,” Yoh 16:15. Usifiwe Utatu Mtakatifu na Umoja usiogawanyika. Amina. 

Wapendwa wana wa Mungu niwaache na mfano huu tunaoujua wote, CHAI. Bila shaka licha ya sukari kuwa bidhaa Ghali na adimu kwa sana, sote tuipendayo chai twaendelea kuisaka sukari kwa gharama yoyote ile. Kuipata chai kama kinywaji na kiburudisho yakupasa kuwa na vitu vitatu: Maji moto, Majani chai “Mchaichai,” na Sukari. Ukikosa kimoja wapo hapo, hautakuwa na “kinywaji-chai.” Na vyote vikiwa pamoja na kufanya “kinywaji chai,” kwa macho ya kibinadamu hutoweza kubainisha kipi ni kipi. Usifiwe Utatu Mtakatifu na Umoja usiogawanyika. Amina
Tumsifu Yesu Kristo

Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasheni habari,” Yoh 16:15


Tusali:-Ee Yesu uliye Mwokozi wetu, Roho Mtakatifu umoja na mtakatifuzaji wetu, na Mungu Muumba wetu, twakiri katika Mungu mmoja na nafsi Tatu. Tuwezeshe daima kwani ni furaha yetu viumbe vyako kuwa katika Umoja huo daima na milele. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario