JUMATATU
WIKI YA 8 YA MWAKA-C
Somo:
1Pet 1:3-9
Zab:
111:1-2, 5-6, 10c
Injili:
Mk 10:17-27
Nukuu:
“Ahimidiwe
Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa
mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo
katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu,
usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu,” 1 Pet 1:3:4
“ili
kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu
ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na
utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo,” 1Pet 1:7
“Yesu akamkazia
macho, akampenda, akamwambia, Umepungukiwa na neno moja. Enenda, ukauze ulivyo
navyo vyote, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo
unifuate,” Mk 10:21
“Yesu akawakazia
macho, akasema, Kwa wanadamu haiwezekani, bali kwa Mungu sivyo; maana yote
yawezekana kwa Mungu,” Mk 10:27
TAFAKARI:
“Akakunja uso kwa neno hilo, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na
mali nyingi.”
Wapendwa wana wa Mungu,
ikiwa wewe ni Mkristo uliye hai ni vyema ukafahamu thamani ya Ukristo wako,
yaani umekombolewa kwa Damu ya thamani kubwa sana, yaani Mwana-kondoo, Yesu
Kristo. “Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha
au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba
zenu;bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa,
yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19. Hivyo maisha yako na yangu hapa duniani
tunapaswa kuyasalimisha yote na kwa asilimia zote kwa Yesu Kristo Mwana wa
Mungu aliye hai. Tendo hili la kujisalimisha ndiko kuabudu kwenyewe kuliko hai
na kwenye kumpendeza Mungu.
Kujiita Wakristo bili
Kristo ni kupotea muda kabisa kwa sababu kwa kufanya hivyo maisha hayo hayana
njia, kweli, uzima (tungali hapa duniani) na ufufuo (maisha ya uzima wa
milele), Yoh 14:6. Hivyo ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii,
tungali hapa duniani wakuhimidiwa ni Mungu, na kwa njia ya pekee na ufunuo
uliokamilika kwa Yeye aliyemwilishwa (Neno), Bwana wetu Yesu Kristo. Kwa Kristo
Yesu kuna Njia, Kweli, Uzima, na Ufufuo wa wafu. Kwake Yesu na kupitia kwake
tunaheshabiwa haki na Mungu kwa wana na warithi wa ufalme wake Mungu. Na kwa
namna hiyo, “Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye
kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa
kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi
usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu,”
1 Pet 1:3:4. Ndugu yangu, tumaini yenye uzima lipo kwa Kristo Yesu, na siyo kwa
kile tulicho au yale tunayoyamiliki hapa duniani. Tungali hapa duniani tu
waangalizi wa muda mfupi kwa yale tunayoyamiliki. Kwayo (tunayoyamiliki) kama
yalivyo hayana umilele ingawa tuliyakuta na tutayaacha.
Hivyo wapendwa katika
Kristo, yatupasa mimi na wewe kuyashinda majaribu tukiwa na ufahamu kwamba
‘maisha ni jaribu,’ na kulishinda jaribu ndipo kunakotupatia Imani yenye
thamani kupita yote tuwezayo kuwa nayo. Vita vyetu vya kiimani kama
anavyotufundisha Mtume Petro ni kulishinda jaribu “ili kwamba
kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo,
ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na
heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo,” 1Pet 1:7. Tokeo la kubebwa na
ulimwengu wa vitu ni anguko kubwa la ‘uzuni.’ Furaha ya kweli ipo pale
tunapoyasalimisha yote kwa Kristo Yesu. Kristo awe tegemeo na msukumu wa yote
tuyafanyayo, na tumuone kwa wengine yale yote tuyafanyayo katika jamii
tunayoishi. Lengo hapa siyo tu kuzishika au kuzifahamu amri za Mungu kama ndege
yule ‘kasuku,’ bali amri hizo za Mungu zimulike uhai uliopo ndani yetu binafsi
na wale wote tuliowekwa dhamana kwao ikiwa ni pamoja na wale wenye uhitaji wa pekee.
Ndugu yangu bila shaka,
hii ndiyo sababu ya Yesu leo kwenye Injili kumuuliza yule Mtu aliyetaka kujua
afanye nini ili aweze kuurithi ufalme wa Mungu. Yesu anamuuliza, “Wazijua amri, Usiue, Usizini, Usiibe,
Usishuhudie uongo, Usidanganye, Waheshimu baba yako na mama yako,” Mk 10:19.
Kwa moyo wa ukunyufu na furaha Mtu yule anamjibu Yesu, “Mwalimu,
haya yote nimeyashika tangu utoto wangu,” Mk 10:20. Jibu hili linamfurahisha
sana Yesu. Ila Bwana wetu Yesu Kristo hakuishia hapa tu. Yesu anakutaka wewe na
mimi tufanye zaidi kwa ya yale ya kawaida (katika kupenda, kutenda, na hata
kukopesha, Lk 6:32-34) kwani hayo hata wenye dhambi huyafanya. Hivyo
“Yesu akamkazia macho, akampenda,
akamwambia, Umepungukiwa na neno moja. Enenda, ukauze ulivyo navyo vyote, uwape
maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate,” Mk 10:21. Hapa
ndipo penye utata na tatizo kubwa kwangu na kwako. Wengi wetu ni vigumu sana
kujibadua katika ulimwengu wa vitu. Tupo tayari kufa na tai shingoni kuliko
kuviachia vitu na kuwa huru; kifikra, kitendaji, na kihuduma, ili kuwa huru
kufanya tu yale yaliyo ndani yetu kadiri ya mpango wa Mungu. Kwa kufanya hayo
na kujishikilia kwa hayo hakuna fadhila ndani yake. “Bali
wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na
thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni
mwema kwa wasiomshukuru, na waovu,
na ndani yake hakuna fadhila,” Lk 6:35.
Hitaji hili la pili,
yaani, ‘kufanya zaidi’ ili kujipatia fadhila linakuwa anguko na uzuni mkubwa
kwa mtu yule aliyekuwa na hamasa kubwa sana ya kuurithi ufalme wa Mungu. “Walakini yeye akakunja uso kwa neno hilo,
akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi,” Mk 10:22. Ndoto na furaha yake ya kuujua na kuurithi
ufalme wa Mungu anakubali iyeyuke kwa sababu ya ulimwengu wa vitu. Ndugu yangu, leo hata ungekuwa na utajiri wa
aina gani kuna mambo hutoweza kuyapata kwa utajiri wako huo hata kama bado
tungali hapa duniani. Ngoja nikujuze machache; kwa utajiri na fedha ulizonazo
waweza kuwa na marafiki wengi ila siyo wa kweli na watakatifu. Kwa fedha na
mali ulizonazo waweza kujenga nyumba nzuri, ukawa na kitanda kizuri cha dhahabu
(na chenye nakshi zote), ila huwezi kuununua uzingizi. Kwa fedha na mali
ulizonazo leo hapa duniani unaweza kwenda kokote upendapo ila Mbinguni ni swala
la kuhesabiwa haki na mastahili ya Mungu Mwenyewe.
Ndugu yangu, kwa fedha na mali ulizonazo
leo waweza kununua chakula kizuri na chenye gharama, kichwaji kizuri na chenye
gharama, ila hutoweza kununua hamu ya chakula hicho. Kwa fedha na mali
ulizonazo waweza kuwanunua watu na kuwahonga watu, ili utimize hazma yako ya
kuwa kile utakacho, ila hutoweza kumnunua Mungu wala kumrubuni. Mwisho wa siku
Mungu atakudhihirishia kile kilichokuwa haki yako mbele ya watu wake
uliowarubuni. Ayubu aliyepatwa na majanga makubwa katika maisha yake, na
kupoteza yote aliyokuwa nayo, anatuambia hivi kuhusu mali na utajiri; “Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi
tena huko uchi vilevile; Bwana alitoa, na Bwana ametwaa; jina la Bwana na
libarikiwe,” Ayu 1:21. Utajiri wake na mali alizokuwa nazo haikuwa sababu ya
kumkufuru Mungu hata pale ilipoondolewa yote pasipo yeye-Ayubu, kwenda kinyume
na matakwa ya Mungu. Maandiko Matakatifu
yanatuambia, “Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala
hakumwazia Mungu kwa upumbavu,” Ayu 1:22. Kwa nini basi mimi na wewe
twaulinganisha au kuufananisha uhai wetu na mali tulizonazo na kumkufuru Mungu?
Mali tunazoongelea hapa ni zote ikiwa pia zile zisizoshikika kama vipaji
alivyokupa Mungu. Mbona basi twavimba vichwa na kujisahau pale tunapofanikiwa
kutokana na zawadi aliyotupa Mungu ikiwa ni pamoja na ufahamu wa kiwango cha
juu? Ndugu yangu, hayo yote si mali yako. Umekopeshwa au kupewa kwa muda tu, na
ukiwa navyo ni kwa faida ya wengine. Huku ndiko kushirikishana utajiri wa Mungu
na Utukufu wake. Mali yako halali ni dhambi zako.
Hivyo
ni vigumu sana, tena sana, kuingia katika Ufalme wa Mungu tukishikamana na
kulandana na vitu na katika fursa hiyo kutokumpa Mungu nafasi na mastahili
yake.
“Yesu akatazama kotekote, akawaambia
wanafunzi wake, Jinsi itakavyokuwa shida wenye mali kuingia katika ufalme wa
Mungu!” Mk 10:23. Kushikamana huko na vitu hakutupi heri yoyote, na badala yake
ni anguko kubwa. Ndugu yangu, ni wale tu walio masikini wa roho (wenye nafasi
ya Mungu ndani ya mioyo yao, Mt 5:3, na wasiokata tamaa wanapoudhiwa kwa
kutenda haki kwa wote, Mt 5:10, ndio watakaourithi Ufalme wa Mbinguni. Na kwa
sababu hiyo, kama washikamana na ulimwengu huu wa vitu na kutokumpa Mungu
nafasi, “Ni rahisi ngamia kupenya katika
tundu ya sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu,” Mk 10:25.
Fundisho hili lenye kweli yote linakuwa mshangao mkubwa kwa wanafunzi wa Yesu,
yaani, wale Thenashara. “Yesu akawakazia macho, akasema, Kwa wanadamu
haiwezekani, bali kwa Mungu sivyo; maana yote yawezekana kwa Mungu,” Mk 10:27.
Hivyo, ukijiachia kwa Mungu bila kujibakiza yote hufanyika kwako kadiri ya
mapenzi yake Mungu na hitaji lako na wale wanaokuzunguka.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa wanadamu haiwezekani, bali kwa
Mungu sivyo; maana yote yawezekana kwa Mungu,” Mk 10:27
Tusali:-Ee
Yesu, kwa Upendo wako tujalie Neema na Hekima ya kufahamu yale tunayohitaji ili
kwa namna hiyo hiyo tuweze kufahamu hitaji au mahitaji ya wengine, na sote kwa
pamoja tuweze kuurithi Ufalme wako wa Mbinguni.
No hay comentarios:
Publicar un comentario