viernes, 29 de abril de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 6 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 6 YA PASAKA YA MWAKA-C

Somo I: Mdo 15:1-2, 22-29
Zab: 67:1-5, 7 (K) 3
Somo II: Ufu 21:10-14, 22-23
Injili: Yoh 14:23-29
Nukuu:
Wakashuka watu waliotoka Uyahudi wakawafundisha wale ndugu ya kwamba, Msipotahiriwa kama desturi ya Musa hamwezi kuokoka,” Mdo 15:1

 “Kwa maana ilimpendeza Roho Mtakatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima,” Mdo 15:28

Nami sikuona hekalu ndani yake; kwa maana Bwana Mungu Mwenyezi na Mwana-Kondoo, ndio hekalu lake,” Ufu 21:22 

Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, kwa maana utukufu wa Mungu huutia nuru, na taa yake ni Mwana-Kondoo,” Ufu 21:23 

 “Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia,” Yoh 14:26

Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga,” Yoh 14:27

 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini,” Yoh 14:29 

TAFAKARI: “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini.”

Wapendwa wana wa Mungu, Leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya sita ya mwaka “C” wa Kanisa. Tafakari yetu ya leo inalenga kwa kiasi kikubwa tukio lile la Pentekoste, na hasa ahadi ile aliyotuhaidia Bwana wetu Yesu Kristo kwamba, ‘huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.’ Leo anatukumbusha ahadi hiyo tunapotafakari neno hili: “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini,” Yoh 14:29. Roho huyu Mtakatifu ndiye aliyeliongoza “Kanisa la mwanzo” kwenye changamoto mbalimbali, na hasa swala zima la kupokelewa na kushiriki huduma za kikanisa kwa wale ambao hawakuwa Wayahudi. Ni Roho huyu pia aliyewawezesha Mitume kufanikisha Mtaguso ule wa Yerusalemu. Na Roho huyu Mtakatifu ndiye anayeliwezesha Kanisa kupanuka na kuenea kila kona ya dunia hadi leo. Hata hivyo kwa kupanuka huku na kuenea kila kona kwa Kanisa hili la mwanzo, lilikumbwa na kasumba ya ubaguzi uliolenga mila na desturi za Kiyahudi. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, tendo la kutahiriwa kwa wayahudi lilibeba tafsiri mbalimbali kwa kadiri walivyoishi na kufanya maagano yao na Mungu.

Kama tulivyoona katika tafakari ya masomo kwa wiki nzima hii iliyokwisha, kwa mara ya kwanza katika historia yao-Wayahudi, tendo hili la kutahiriwa lilibeba maana ya usafi na kwa yule aliyetaka kuoa lilichukua maana ya “Bwana harusi wa damu.” Ndipo Sipora akashika jiwe gumu na kuikata govi ya zunga la mwanawe, na kuibwaga miguuni pake akasema. Hakika wewe u bwana arusi wa damu kwangu mimi. Basi akamwacha. Ndipo huyo mkewe akanena, U bwana arusi wa damu wewe, kwa ajili ya kutahiri” Kut 4:25-26.  Kutahiri kulimaanisha pia agano kati yao na Mungu hasa kwa tendo la Mungu kuwatoa utumwani Misri, na hapa wanatairiwa kwa mara ya pili. “Wakati huo Bwana akamwambia Yoshua, Haya, jifanyie visu vya mawe ya gumegume, watahiri tena wana wa Israeli mara ya pili. Basi Yoshua akajifanyia visu vya mawe ya gumegume, akawatahiri wana wa Israeli huko Gibea-haaralothi. Na sababu ya Yoshua kutahiri ni hii; watu wote waliotoka Misri, waliokuwa waume, hao watu waume wote waendao vitani walikufa katika bara njiani, baada ya wao kutoka Misri,” Yos 5:2-4. Kutahiriwa pia kulimaanisha kushika torati kikamilifu. Basi ikiwa yeye asiyetahiriwa huyashika maagizo ya torati, je! Kutokutahiriwa kwake hakutahesabiwa kuwa kutahiriwa?  Rum 2:26. Pamoja na sababu nyingine zote tulizokwisha kuziona, hii ya mwisho ndiyo iliyotumika kama kigezo cha alisiye Myahudi kupokelewa katika jumuiya hii ya Wakristo wa kwanza ambayo kwa kiasi kikubwa walikuwa Wayahudi. Hapa tunaambiwa, Wakashuka watu waliotoka Uyahudi wakawafundisha wale ndugu ya kwamba, Msipotahiriwa kama desturi ya Musa hamwezi kuokoka,” Mdo 15:1

Mambo haya ya nje hayakupaswa na hayapaswi kuwa sababu ya kutokuishi upendo wa Kristo katika Kanisa. Hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3:11. Maandiko Matakatifu, hasa Habari Njema ya Bwana wetu Yesu Kristo kama ilivyoandikwa na Mwinjili Yohana inasema ukweli huu wa Kristo, kwamba,  Uzima wetu, na uhai wetu kiroho ni katika Kristo Yesu aliye mzabibu nasi matawi yake. Kuishi katika ukweli huu ni kuzaa matunda, yaani kuwa watu wa  upendo, haki na amani kama Kristo mwenyewe. Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa,” Yoh 15:2.

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, “sisi sote tuna mastahili sawa mbele ya Kristo, yeye ndiye aliyetuchagua bila mastahili yetu ili tuzae matunda ya kudumu.” Yakiwa haya ndiyo majumuisho ya Mtaguso wa Yerusalemu, Kristo anatupenda kama tulivyo na kutuhesabia haki mbele zake na mbele ya Mungu Baba bila kujali familia tulizozaliwa, koo tulizotoka, kabila tulizotoka, na hata mataifa tuliyotoka. Hakika, ingekuwa haya niliyoyataja kuwa kigezo cha kuwa Mkristo na hata kuwa Mtumishi katika Kanisa lake KRISTO, bila shaka ingekuwa ndoto leo mimi au wewe kuwa kama nilivyo ndani na katika KRISTO. Ni katika msingi huu nilioutaja (Kristo ametuchagua bila ya mastahili yetu), Mtaguso wa Yerusalema wanaafikiana vyema kuhusu swala la watu wa mataifa waliolipokea neno na kuunda ujumuiya ya Kikristo. Ukristo wetu hautokani na hayo matabaka niliyoyasema hapo juu. Ukristo wetu unatokana na kuhesabiwa haki na Kristo mwenyewe, kulikotokana na kutupenda upeo, Yoh 13:1. Hivyo Mtaguso wa Yerusalemu unatoa tamko lifuatalo, sisi tumeona vema, hali tumepatana kwa moyo mmoja, kuwachagua watu na kuwapeleka kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo,” Mdo 15:25. Mtume Paulo na Barnaba wanachaguliwa kwa vigezo vya maisha yao kupeleka ujume huu kwa wale waliolipokea neno. Ni watu waliohatirisha maisha yao kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo,” Mdo 15:26.

Hata hivyo Yuda na Sila ndio watakaosema kwa vinywa vyao juu ya ujembe huo. Basi tumewatuma Yuda na Sila, watakaowaambia wenyewe maneno yayo hayo kwa vinywa vyao,” Mdo 15:27. Yuda na Sila bila shaka ni watu waliokuwa karibu sana na jumuiya hiyo mpya ya Antiokia. Uwakilishi huu ni njia mojawapo ya kuboresha ukaribu wao na jumuiya ya Yerusalemu, na kuanza kuishirikisha jumuiya hii mpya ya Antiokia yale yote yamuhusuyo Kristo. Ukaribu na umoja huu si wakubebeshana mizigo, bali ni fursa ya kuyatafakari makuu ya Mungu na upendo wake kwa kila mmoja aliyeridhia upendo na umoja huo wa Kristo. Roho Mtakatifu ndiye mleta umoja huo. Kwa maana ilimpendeza Roho Mtakatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima,” Mdo 15:28.
Hivyo basi, ili kuendelea na umoja huu na upendo huu ndani na katika Kristo, iliwapasa kujitenga na yale ambayo hayakuwa na mwelekeo wa Kimungu. Ni ukweli kwamba kama tunataka kuishi katika Kristo, yatupasa kujikana wenyewe na kumfuata. Yatupasa kuacha yale ya zamani na kuyachuchumilia yale yampendezayo Kristo. Hivyo basi, jumuiya hii mpya ya Antiokia, inapaswa kufanya haya yafuatayo; yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati. Mkijizuia na hayo, mtafanya vema. Wasalamu,” Mdo 15:29. Tunapoachana na makandokando haya ya maisha ndipo tunapokuwa karibu na upendo wa Kristo na kutimiza mapenzi yake. Huu ndio upendo anaotutaka Kristo tuuishi kama familia yenye hofu ya Mungu na kuwajibika. Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” Yoh 15:12. Ndugu yangu, jambo hili si rahisi! Mimi na wewe leo tupo hiki tulicho kama tokeo la historia yetu tangu kuzaliwa, makuzi yetu ambayo yameathiriwa na mila na desturi zetu, ufahamu wetu ambao umeathiriwa pia na mfumo mzima wa elimu tuliokuwa nao. Katika mazingira hayo ya makuzi, lengo ni kuuona ukweli kama ulivyo, na siyo kuuona ukweli kama tulivyo. Hapa ndipo penye tofauti kubwa ya kusoma na kuelimika. Wote walioelimika wamesoma, ila siyo wote waliosoma wameelimika. Hapa kusoma simaanishi kwenda darasani kama ilivyo ada, bali kuyaelewa vizuri mazingira yanayokuzunguka, ambayo kwa kiasi kukubwa si lazima kwenda darasani kadiri ya mfumo unavyotutaka. Hivyo kwa mazingira ya Kanisa la mwanzo, na changamoto iliyowakabili, Mtaguso ule uliwalazimu kuyaona yote katika upendo wa Kristo na hatma ya upendo huo ambao ni kifo kile cha Msalaba.

Ndugu yangu, kuukubali ubinadamu wetu ni pamoja na kujitambua na kuzishika amri za Mungu kwani twataka kuongozwa na Mungu na kuwa watoto wa Mungu. Hivyo Yesu anasema, Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake,” Yoh 14:21. Nani asiyependa kutambuliwa na Mungu? Embu fikiri yote uyafanyayo leo kadiri ya wito wako mwisho wa siku yanakosa kibali mbele ya Mungu. Kumpenda Mungu ni kushika amri zake. Kristo kesha tuambia ni amri ipi iliyo kubwa kuliko zote. Je, neno UPENDO ni geni kwako? Yesu anasema, Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:24. Hata Bwana wetu Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani hakujifanyia mambo yake kadiri atakavyo. Alikuwa makini sana kutimiza mapenzi ya yule alimpeleka yaani Mungu Baba. Swali la kujiuliza mara zote ni hili, je, hapa nilipo na kadiri ya agano au maagano yangu kimaisha ninayafanya mapenzi ya Mungu? Kama jibu ni hapana, Je, nimejiandaaje kujibu swali hili siku ya mwisho?

 Ndugu yangu, mpango wa Mungu kwetu na hasa swala zima la maisha ya umilele limeratibishwa vizuri sana. Nafasi uliyokuwa nayo leo na “mawezekano yake kimaisha,” hayapo kwa bahati mbaya kwako au kwa upendeleo. Yote haya yanasababu kubwa kuhusu maisha yako ya sasa na wale wanaokuzunguka, na hatma  yake, yaani, umilele. Hata hivyo, kwa kutusaidia, Yesu Kristo anatukumbusha jambo muhimu sana ndugu zangu. Naye anasema, Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia,” Yoh 14:26. Hivi kama tumefundishwa yote na kukumbushwa yote tunayosababu ya kushindwa mtihani ulio mbele yetu? Ni katika maana hii Yesu anatuambia mwisho wa kiama jambo hili litatokea kwa hakika. “Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje,” Lk 13:28. Neno hili “kusaga meno” limesemwa mara sita katika Habari Njema ya Bwana wetu Yesu Kristo kama iliyoandikwa na Mwinjili Matayo, mara moja kama ilivyoaandikwa na Mwinjili Marko na mara moja kama ilivyoandikwa na Mwinjili Luka. Maana yake ni kwamba hakutakuwa na nafasi ya kujitetea kwani nafasi ya kufanya vema ni leo na sasa. Kristo Yesu angali hapa duniani aliweka yote sawa na kusema bila kupindisha neno, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Yesu Kristo ni njia kama ulivyo Mlango pekee wa kuufikia uzima wa milele. Na njia aliyoichagua Yesu ni Msalaba. Kwa kuibeba misalaba yetu na kuchukuliana kindugu katika misalaba ya wenzetu kwa uaminifu na hofu ya Mungu, tunakutana naye Kristo katika hali na mazingira hayo. Yesu Kristo ni kweli halisi. Kweli hii tunakutana nayo katika neno lake hasa pale tunapokuwa tayari kulisikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno, kulishirikisha neno, na mwisho kuwa shahidi wa neno.

Na Yesu Kristo ni uzima halisi. Kristo ni uzima halisi tunaposhiriki Ekaristi Takatifu katika mastahili yake. Yesu anatuambia, “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe” Yoh 6:35. Ni katika kula chakula hiki-mwili na damu yake,  Yesu anahaidi mambo mawili makuu: Moja, ni ufufuko siku ya mwisho. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:54. Na katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Kristo hukaa ndani yetu. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake,” Yoh 6:56. Hata hivyo Mtume Paulo anatupa angalizo la chakula hiki cha uzima. Naye anasema, Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana,” 1Kor 11:27. Yatupasa kuijongea Meza ya Bwana tukiwa na mastahili ya kufanya hivyo-usafi wa mwili na roho, yaani, pasipo hatia yoyote. Zaidi ya hapo ni kuikufuru Meza ya Bwana.

Kuliishi kiaminifu fundisho hili zito la Kristo, Yoh 14:6, kunatusaidia kuzama ndani ya ule ufunuo wa Yohana na kuona uzuri wa maisha ya umilele kadiri ya somo letu la pili leo. Naye anasema, Nami sikuona hekalu ndani yake; kwa maana Bwana Mungu Mwenyezi na Mwana-Kondoo, ndio hekalu lake,” Ufu 21:22. Maana yake ni nini?

Basi mpendwa katika Kristo kwa kuelewa zaidi juu ya neno hilo la Ufunuo 21:22, nikuache na mfano huu:-Bila shaka wengi wetu tuna mawazo ya “kuwa TENA kile tulicho leo na sasa baada ya maisha haya hapa duniani.” Mathalani, kama mimi leo Mama Kanisa kanihesabia haki ya kuwa mtumishi wake na muhudumu kama ‘Baba Paroko au Askofu,’ kwenye maisha baada ya kifo-umilele, hakutakuwa tena na wajibu huo kama Paroko au Askofu kwa sababu huko hakutakuwa na “mwonekano,” “muundo,” “mfumo” tena wa kiparokia au kijimbo. Nawe ndugu yangu unayeishi leo Sakramenti yako ya ndoa ni kukumbushe maneno haya ya Yesu; Naye anasema Wana wa ulimwengu huu huoa na kuolewa; lakini, wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule kufufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi; wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo,” Lk 20:34-36. Je, maneno haya ya Yesu na yale ya ufunuo wa Yohana 21:22, yanasema chochote katika maisha yako leo? 

Wapendwa wana wa Mungu, bila kujali mtindo wa maisha tunaoishi leo kila mmoja kadiri ya wito wake, sote katika maisha ya umilele tutajulikana kwa cheo chetu tu, yaani, utakatifu wako. Na mahali pa kuutafuta utakatifu huo ni hapa hapa duniani kwa muda huu mfupi tuliokuwa nao. Hivyo, haijalishi mimi ni nani leo, ila kila siku yanipasa niyaone maisha yangu katika mtazamo wa Kimungu, yaani: Maisha ya duniani ni jaribu, Maisha ya duniani ni dhamana, na Maisha ni jukumu la muda mfupi. Utukufu wa Mungu ambao ni UTAKATIFU WAKE ni mwanga na nuru ya kutosha katika maisha hayo ya umilele. Utakatifu wa kila mmoja wetu ambacho ndicho cheo chetu, ni ile hali halisi tutakayokuwa nayo wakati tulipoumbwa, yaani, ‘sura na mfano wake Mungu,’ Mwa 1:27. Hivyo, “wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo,” 1Yoh 3:2. Kumwona Mwana-Kondoo huyu, Yesu Kristo kama alivyo kwawezekana tu katika hali ya utakatifu wako. Kwa sababu,  Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, kwa maana utukufu wa Mungu huutia nuru, na taa yake ni Mwana-Kondoo,” Ufu 21:23. Je, bado taa yangu inawaka, yaani, UTAKATIFU wangu? Je, ile sura na mfano wa Mungu ndani yangu bado inang’aa, au ishafifishwa na mali yangu halali, yaani, dhambi zangu? Tafakari!

Tumsifu Yesu Kristo! 

Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia,” Yoh 14:26


Tusali:-Ee Yesu, uliye Mwana-Kondoo na taa halisi ya Mungu, niwezeshe kila siku kutoififisha ile sura na mfano wa Mungu ndani yangu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario