IJUMAA WIKI YA 8 YA MWAKA-C
Somo: 1Pet 4:7-13
Zab: 96:10, 11-12, 13
Injili: Mk 11:11-26
Nukuu:
“Lakini
mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala,”
1Pet 4:7
“Mtu akisema, na
aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na
Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza
una yeye hata milele na milele. Amina,” 1Pet 4:11
“Akaona
kwa mbali mtini wenye majani, akaenda ili labda aone kitu juu yake; na
alipoufikilia hakuona kitu ila majani; maana si wakati wa tini. Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda
kwako. Wanafunzi wake wakasikia,” Mk 11:13-14
“Kwa sababu hiyo
nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo
yatakuwa yenu,” Mk 11:24
“Nanyi,
kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu
aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu,” Mk 11:25
“Lakini
kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa
yenu,” Mk 11:26
TAFAKARI: “Mwaminini
Mungu. Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili
na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu.”
Wapendwa wana wa Mungu, licha ya kutokukamilika kwetu kama wanadamu,
Mungu ameweka ndani yetu uwezo wa kumtafuta na kumfikia kama tutamtafuta. Hali
na uwezo huu ndani yetu ni namna ile tuliyoumbwa kwa sura na mfano wake, Mwa
1:27. Hivyo kwa Imani na hali ya msukumo uliopo ndani yetu Mungu anapatikana
tunapomtafuta. “Mtafuteni Bwana, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu
baribu,” Isa 55:6. Ni kwa uwezo huu uliopo ndani yetu unatupa uwezekana wa
kumrudia Mungu kwa sala na toba naye uturehemu. Mungu kamwe hapendi tuangamie
katika uovu na ubaya wetu. Bado kuna nafasi ya kujenga tena mahusiano mazuri na
nafsi yako mweyewe, na binadamu mwenzako, na
Mungu, na mazingira unayoishi. “Mtu mbaya na aache njia yake, na mtu
asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa
Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa,” Isa 55:7. Huruma ya Mungu ipo wazi muda
wote. Ni mimi na wewe tu kuitafuta kwani haipo mbali.
Uwezo na hali hii iliyo ndani mwetu yenye kutuwezesha kufika pale
alipo Mungu kama tutamtafuta, inakukata kila mara uwe zaidi ya kile ambacho kwa
mazingira ya kawaida ungepaswa kuwa-“be productive and positive wherever and
whenever you are.” Muono huu wa kuwa zaidi ya kile ulicho kwa sababu ndani yako
upo uwezekano, ndicho kinachotokea kwa ule mtini ambao ulikuwa na majani ila
haukuwa na tini kwa sababu haukuwa wakati wake. Yesu alijua fika kabisa si
wakati wa tini, ila alienda kutazama kama tini zipo. Kwa mazingira ya kawaida
mara chache msimu wa matunda fulani, upo uwezekano wa kuyapata yale yanayowahi
kutoka kabla ya msimu husika kufikia. Ujio wa Yesu kwa watu wake, alitegemea kuwepo
na muono chanya. Kwa maana nyingine alitegemea wawe na Imani hata kama mambo
yote yalikuwa bado kufunuliwa kwao-wakati utakapotimia.
Adhabu iliyotolewa kwa
mti ule wa mtini ni kielelezo kwa Wayahudi ambao hawakuwa na Imani juu ya ujio
wa Mwana wa Mungu licha kwa mbali walitegemea mkombozi, na huu ndio ule uwepo
wa majani yale ya mtini. Adhabu hii pia yanihusu mimi na wewe pale
tunaposhindwa kuwa zaidi ya kile tulicho kwa sababu ndani yetu uwezekano
ushawekwa kwa kuumbwa kwetu kwa sura na mfano wake Mungu. Yesu “Akaona kwa mbali mtini wenye majani, akaenda ili labda
aone kitu juu yake; na alipoufikilia hakuona kitu ila majani; maana si wakati
wa tini. Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako. Wanafunzi
wake wakasikia,” Mk 11:13-14. Hii ndiyo nguvu inayosukuma imani yetu kwa
sababu uwezo huo tushawekewa tayari.
Kuchukizwa huku kwa Yesu kutokana na uhaba huu wa Imani unajionyesha
alipofika Hekaluni na kukuta ndivyo sivyo. “Akafundisha,
akasema, Je! Haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa
yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Mk 11:17. Kuifanya
nyumba ya Mungu-“Hekalu kuwa pango la wanyang’anyi kuna tafsiri ya nyumba kama
jengo, na nyumba kama mwili, yaani Hekalu la Roho Mtakatifu. Majengo haya yote (kama
nyumba au mwili) katika tafsiri yake yapaswa kupewa stahili yake, yaani,
“iliyotengwa kwa kazi ya Mungu tu: kusifu, kuabudu, kushukuru, kutolea sadaka. “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho
Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu
wenyewe; maana mlinunuliwa kwa
thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu,” 1Kor 6:19-20. Ndugu
yangu, Kristo kama kichwa na jiwe kuu la pembeni, sisi kwa Ubatizo wetu
tumeunganishwa naye na kuwa Hekalu Takatifu. “Mmejengwa
juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la
pembeni. Katika yeye jengo lote
linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana,” Efe
2:20-21. Hili ndilo Kanisa kama mwili wa Kristo, Kristo akiwa ndiye Kichwa nasi
viungo vya mwili huo. “Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha
kanisa; naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe
mtangulizi katika yote,” Kol 1:18. Je, waamini hilo?
Baada ya kuona mtini
ule umenyauka toka shinani, kwa mshtuko aliokuwa nao Petro, Yesu anamjibu, “Mwaminini Mungu,” Mk 11:22. Alichokifanya Yesu
ni kudhihirisha uwezo na nafasi yake na hasa kile alichokijia, yaani, kukuweka
huru wewe na mimi kutoka utumwa wa dhambi. Huu ndio ukombozi wa kweli. Hivyo
ukimwamini Mungu na huyu aliyetumwa na Mungu, yaani, Bwana wetu Yesu Kristo
pasipo shaka mengi na ya ajabu yatatendeka kwako kwa jina lake. “Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng'oka
ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo
asemayo yametukia, yatakuwa yake,” Mk 11:23. Imani ujengwa na kuwa na nguvu
katika maisha ya sala na kujiachia pasipo shaka. Ni kusali au kuomba ukijua
ushakipata tayari hata kama kwa wakati ule bado. Hii ndiyo hali ya kuwa zaidi
ya kile ulicho. “Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo
mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu,” Mk 11:24. Tatizo
kubwa langu na lako tunaomba tukiwa na mashaka kama kweli Mungu anaweza
kutupatia kile tuombacho kutokana na mazingira tuliyo nayo. Tusimwendee Mungu
kwa majaribio. “Maana mawazo yangu si mawazo yetu, wala njia zenu si njia
zangu; asema Bwana,” Isa 55:8. Mungu wetu hajaribiwi kwa sababu ukamilifu ni
asili yake.
Ila tusalipo yatupasa
tusiwa katika hali ya hatia. “Nanyi, kila
msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye
mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu,” Mk 11:25. Mfano: Tusalipo sala ya
‘Baba Yetu,’ sharti la
kuipata huruma ya Mungu na msamaha wake, ni wewe kwanza kuwa tayari kusamehe.
Hii ndiyo maana ya maneno haya; “Basi
ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno
juu yako, iache
sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha
urudi uitoe sadaka yako,” Mt 5:23-24. Mungu aliye mkamilifu na Mtakatifu
hafananishwi na uchafu. Tuyasuluhishe kwanza mapungufu yetu nipo tumjongee
katika sala na maombi. “Lakini kama
ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu,”
Mk 11:26. Je, bado umewekeza katika kutokusamehe? Mradi huo hautakuwa na faida
zaidi ya hasara, tena kubwa ajabu.
Wapendwa wana wa Mungu,
yeyote yule anayewekeza katika kusamehe anajua kuishi katika malengo na kuyaona
maisha katika mtazamo wa kimungu, yaani, maisha kama jaribu, dhamana, na jukumu
la muda mfupi. Maisha kama jukumu la muda mfupi ni kutambua kwamba, “mwisho
wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala,” 1Pet 4:7.
Tunda la sala zetu liimarishe upendo kati yetu. Na kupendana kwetu kutuzamishe
zaidi katika sala. Na penye sala na upendo wa kweli dhambi haina nafasi. Hivyo,
“Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi
katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi,” 1Pet 4:8. Sala na upendo wa kweli utukuza kimwili na kiroho
na kwa namna hiyo hiyo tunawezeshwa kuvifahamu vipaji na karama zetu Mungu
alizotujalia kwa ajili yetu na jumuiya ile tunayoishi. Ndugu yangu, “kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama,
itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu,”
1Pet 4:10. Mungu hakukupa kamara uliyonayo kwa kujifaidisha nafsi yako. Mungu
amekupa karama hiyo akiwa na kusudi la huduma na kukamilishana ili kuwa na
umoja katika utofauti ambao ndio Utukufu na uzuri wa Mungu.
Wapendwa katika Kristo, uwezo huu Mungu
aliouweka ndani yetu, “kumtafuta na kumfikia,” licha ya hali yetu ya
kutokukamilika kama wanadamu, ndiyo inayotuweka karibu zaidi na Mungu. Hivyo, “Mtu akisema, na aseme
kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu;
ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye
hata milele na milele. Amina,” 1Pet 4:11. Ndugu yangu, wewe si bahati mbaya na
kamwe usijidharau.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini
mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala,”
1Pet 4:7
Tusali:-Ee Bwana wangu Yesu Kristo, nikumbushe
kila siku niamkapo kwamba muda wangu wa kuishi hapa duniani unakwisha, hivyo
niwe zaidi ya kile kilichokuwa jana. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario