miércoles, 18 de mayo de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 7 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI YA 7 YA MWAKA-C
Somo: Yak 5:9-12
Zab: 103:1-2, 3-4, 8-9, 11-12
Injili: Mk 10:1-12 
Nukuu:
Ndugu, msinung'unikiane, msije mkahukumiwa. Angalieni, mwamuzi amesimama mbele ya milango,” Yak 5:9 

Lakini zaidi ya yote, ndugu zangu, msiape, wala kwa mbingu wala kwa nchi; wala kwa kiapo kinginecho chote; bali ndiyo yenu na iwe ndiyo, na siyo yenu iwe siyo, msije mkaangukia hukumu,” Yak 5:12

Lakini tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke,” Mk 10:6 

Kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja,” Mk 10:7-8 

Basi alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe,” Mk 10:9 

Akawaambia, Kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake;  na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini,” Mk 10:11-12 

TAFAKARI: “Tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke.”

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna hata mmoja kati yetu ambaye yupo katika ulimwengu huu kwa bahati mbaya. Ni kwa maana hiyo hiyo kwamba hakuna kati yetu aliyejipangia kuwa kama alivyo; kijinsia, kuchagua azaliwe na wazazi wa aina gani, kabila gani, au taifa gani. Tupo kama tulivyo kwa makusudi yake Mungu kwa sababu anampango mzuri na kila mmoja wetu. Je, una sababu yoyote ya kumlaumu Mungu au kumkosoa Mungu kwa kile ulicho? Angalizo: Ndugu, msinung'unikiane, msije mkahukumiwa. Angalieni, mwamuzi amesimama mbele ya milango,” Yak 5:9. Leo kutokana na matumizi mabaya ya neno ‘uhuru,’ tumefikia hatua ya kukosoa kila kitu ambacho kimsingi ni kwenda kinyume kabisa na kusudio la uumbaji wetu.

Kwa mfano swala la jinsia Maandiko Matakatifu yanatufundisha kwamba, tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke,” Mk 10:6. Leo walio wanaume wanataka kuwa wanawake na walio wanawake wanataka kuwa wanaume kwa kisingizio cha kutumia uhuru wao. Baadhi ya nchi za ulaya wazazi hawana tena mamlaka ya kuamua juu ya watoto wao. Mtoto akifikia umri ufaao kisheria ujiamulia jinsia aipendayo. Je, tunaenda kinyume na mpango wa Mungu? Maandiko Matakatifu yanatuambia, Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba,” Mwa 1:27. Hii ghiliba na kasumba ya kujibadili na kuwa kitu kingine inatoka wapi? Kwa nini tunashindwa kujipokea?

Kumkosoa Mungu katika suala la uumbaji wake ni sawa na kuhasi na kuikataa ile ‘ndiyo’ iliyomo ndani mwetu. Ukosoaji huu utupelekea kuishi maisha yasiyo na malengo na mwisho wa siku tunageuka kuwa vituko.Lakini zaidi ya yote, ndugu zangu, msiape, wala kwa mbingu wala kwa nchi; wala kwa kiapo kinginecho chote; bali ndiyo yenu na iwe ndiyo, na siyo yenu iwe siyo, msije mkaangukia hukumu,” Yak 5:12. Je, unayekwenda kinyume na matakwa ya Mungu ndiyo yako ipo wapi?

Wapendwa wana wa Mungu, kwa upendo wake juu yetu Mungu hakuishia tu kumuumba Adamu, bali aliona inafaa Adamu akawa na mwenza wake na kuifanya familia kama shina na msingi wa maisha kumwelekea Yeye mwenyewe kama ulivyo ule Utatu Mtakatifu wa umoja usiogawanyika, yaani, Mungu Mmoja na nafsi tatu; Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu. Tukirudi kwenye kusudi na hitaji la uwepo wa familia, ni kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja,” Mk 10:7-8. Familia itatoka wapi kama tutafuata matamanio yetu na tamaa zetu kwa kisingizio cha uhuru usio na mipaka?

Ndugu zangu, alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe,” Mk 10:9. Leo mwanadamu amejitwalia mamlaka yasiyo yake na kujaribu kuuvaa umungu ambao pamoja na umungu huo wa kijivika, kifo hakijaacha kumwaibisha. Hata hivyo kwa kiburi chake mwanadamu huyu hapendi kujirudi na kuwa kile kilicho kusudi la Mungu juu yake. Kusudi la Mungu la kumfanya mtu mme na mtu mke kuwa kitu kimoja ni kuufunua upendo wake kwetu, mshikamano wake, na ukaribu wake wetu usiokoma. Ni jukumu na wajibu wetu kuudhihirisha upendo huo wa kweli kati yetu.  Hilo pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu,” Rum 12:9-10. Tunapokosa upendo huu na umoja huu na hasa katika funganishi la Sakramenti ya Ndoa na kujishikamanisha na mwingine nje ya ndoa husika, muonekano huo hauna jina lingine zaidi ya ‘uzinifu.’ Hivyo, kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake;  na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini,” Mk 10:11-12. Ndugu yangu, ukubali mpango wa Mungu ndani yako. Mungu anasababu kubwa ya kukuumba kama ulivyo. 

Tumsifu Yesu Kristo!

Basi alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe,” Mk 10:9


Tusali:-Ee Yesu Mwema, tufungamanishe siku zote na kusudi la Mungu katika maisha yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario