JUMATANO
WIKI YA 8 YA MWAKA-C
Somo:
1Pet 1:18-25
Zab:
148:12-13, 14-15, 19-20
Injili:
Mk 10:32-45
Nukuu:
“Nanyi
mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu;
mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa
damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya
Kristo,” 1Pet 1:18-19
“Bali Neno la Bwana hudumu
hata milele. Na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu,” 1Pet 1:25
“Kikombe
ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa
kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa
tayari,” Mk 10:39b-40
“Kwa maana Mwana
wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia
ya wengi,” Mk 10:45
TAFAKARI:
“Hamjui mnaloliomba.”
Wapendwa wana wa Mungu,
matamanio yanayosukumwa na hali ya ubinafsi wetu mwisho wake hayana heri kwako
wewe uyatamaniyo na wala kwa wale wanaokuzunguka. Kumbe leo na kwa namna ya
pekee Injili, inatualika kutafakari kwa undani kuhusu yale tunayoyatamani au
kuyapata. Ni vyema kujibu maswali yafuatayo kwa uelewa; Je, unafahamu vizuri
unachokitamani? Je, wafahamu vizuri wajibu wa kile ukitamanicho? Nini hasa lengo ya hicho ukitamanicho? Je, hicho
ukitamanicho na baada ya kuwajibika kwako kwacho kitakupatia utakatifu na
kuupata uzima ule wa milele?
Kwa kutokufahamu
vizuri kile wakitamanicho, wana wa
Zebedayo, Yakobo na Yohana, wanajichagulia sehemu za kuketi, mmoja mkono wa
kuume wa Yesu, na mwingine mkono wa kushoto wa Yesu, katika utukufu wake. Mitume hawa hawakuwa na muda wa
kutafakari fumbo lile la kifo alilokuwa anawasimulia Bwana wetu Yesu Kristo,
yaani, “Mwana wa Adamu atatiwa mikononi mwa
wakuu wa makuhani na waandishi, nao watamhukumu afe, watamtia mikononi mwa
Mataifa, nao watamdhihaki, na
kumtemea mate, na kumpiga mijeledi, na kumwua; na baada ya siku tatu
atafufuka,” Mk 10:33b-34. Walijitazama
wenyewe na nafsi zao tu. Kutokana na tamaa hiyo, walikuwa tayari kutoa majibu
mepesi kwa maswali magumu aliyowauliza Yesu. Kwa vile walithibitisha kuwa wapo
tayari kukinywea kikombe kila cha mateso, Yesu anawataka wazame zaidi kwa kile
wakitamanicho kwa kuwaambia, “Kikombe
ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa
kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa
tayari,” Mk 10:39b-40. Kumbe kukaa na Yesu katika Utukufu wake siyo swala la
kujitwalia tu, au kupeana kwa kujuana au kwa urafiki kama tuonavyo katika
malaka za kibinadamu, bali licha ya gharama zake, Mk 10:39b, ni swala la
kuhesabiwa haki, Mk 10:40.
Pamoja na ugumu huo, Yesu anatutaka
tutofautishe namna yetu ya kutenda na kuishi ili tulenge fumbo lile la kifo
chake cha Msalaba ambapo ndipo ulipotundikwa wokovu wetu na kumpatia Kristo
Utukufu wake, nasi kuhesabiwa haki ya kuwa wana wa Mungu bila ya mastahili yetu
binafsi. “Nanyi mfahamu kwamba
mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka
katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya
thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,”
1Pet 1:18-19. Damu hii yenye thamani kubwa iwe chachu na kielelezo cha imani
yetu na kumwamini Mungu. Ni kwa Damu hii ya Mwana-kondoo huyu aliye na hila,
Yesu Kristo, “ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu,
aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata imani yenu na tumaini lenu liwe
kwa Mungu,” 1Pet 1:21. Hivyo tenda na ishi yetu isukumwe kwa kuthamini
kukombolewa kwetu huku kuliko kwa thamani kubwa ajabu.
Kristo Yesu hali akijua
hulka yetu wanadamu anatukumbusha kuepuka kutawala wengine kwa mabavu kama
asemavyo, “Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala
kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha,” Mk 10:42. Kristo hataki hilo litokee
kwa Mitume na wafuasi wake. Kinyume chake tutangulize mbele ‘kutumika vyema’ na
siyo ‘kutumikiwa wala kuogopwa.’ “Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa,
bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mk 10:45. Maana yake
nini?
Wapendwa wana wa Mungu,
Kristo anatutaka tuelewa kuwa utumishi ni kujitoa kwa watu kwa upendo na
kuwapenda. Huwezi kuwatumikia watu vizuri kama huwapendi. Na ukifanya hivyo
(kuwatumikia ukiwa huwapendi) basi nyuma yake kuna ubinafsi mkubwa na
kujitazama wewe tu, familia yako, ndugu zako, marafiki zako, na mwisho kupoteza
dhima nzima ya kutumika na umma. Hapa tunahitaji nidhamu ya hali ya juu na
yenye kusukumwa na utii wa kweli. Hivyo, “Mkiisha kujitakasa roho
zenu kwa kuitii kweli, hata kuufikilia upendano wa ndugu usio na unafiki, basi
jitahidini kupendana kwa moyo,” 1Pet 1:22. Kupendana kwa moyo ni kumwona Kristo
Yesu kwa wote unaotumika kwao. Hapa ndipo kule kutoa nafsi yako iwe fidia ya
wengi, Mk 10:45b.
Pili, kuwa tayari
kutumika kunatutaka kusahu uzamani wetu na mazoea yetu. Ni kuzaliwa mara ya
pili kwa kuliishi neno la Mungu lenye uzima. Kuliishi neno la Mungu lenye uzima
kwanza kabisa ni kuwa tayari kuhusu neno
hilo. Pili, ni kuwa na uwezo wa kusikia neno, kulipokea neno, kulitafakari
neno, kulishirikisha neno, na kuwa shahidi wa neno hilo likiakisi maisha yako. “Kwa
kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile
isiyoharibika; kwa neno la Mungu lenye uzima, lidumulo hata milele,” 1Pet 1:23.
Ndugu yangu, neno hili tunahubiriwa kila siku. Lifanye kuwa sehemu ya maisha
yako kwa sababu, “Neno la Bwana hudumu hata milele. Na neno hilo ni
neno lile jema lililohubiriwa kwenu,” 1Pet 1:25.
Tatu, kuwa tayari
kutumika ni kuukubali utumishi kwanza ambao mwisho wa siku ndio utakao sadifu
ukubwa ule kama kweli ndio unaoutamani. Hivyo, “bali
mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu,” Mk 10:43b. Pili,
kuikubali hali ya utumwa kwa ajili ya wote. Hali hii ya utumwa ndiyo
itakayotuweka kuwa wa kwanza au wa mwisho. Hivyo, “na
mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote,” Mk 10:44. Ndugu
yangu, huu ndio utumishi na kutumika kwa yeyote yule mwenye hofu ya Mungu. Na
kama upo tayari kutumika na unamatamanio haya, omba hivyo ukifahamu wajibu
wa kile ukiombacho. La sivyo hutotumika vyema na mwisho wa siku ni kupoteza
vyote: Utakatifu wako, na uzima ule wa milele.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kikombe
ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa
kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa
tayari,” Mk 10:39b-40
Tusali:-Ee
Yesu, tufundishe namna ya kuomba kile tukitamanicho tukiusahau ubinafsi wetu.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario