martes, 31 de mayo de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 9 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 9 YA MWAKA-C
Somo: 2Tim 2:8-15
Zab: 25:4-5ab, 8-9, 10, 14
Injili: Mk 12:28-34
Nukuu:
Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi,” 2Tim 2:9 

Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele. Ni neno la kuaminiwa. Kwa maana, Kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia; Kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; Kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi; Kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe,” 2Tim 2:10-13 

 “Katika amri zote ni ipi iliyo ya kwanza?” Mk 12:28b

 Yesu akamjibu, Ya kwanza ndiyo hii, Sikia, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja; nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote,” Mk 12:29-30 

Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi,” Mk 12:31

Naye Yesu, alipoona kwamba amejibu kwa busara, alimwambia, Wewe hu mbali na ufalme wa Mungu. Wala hakuthubutu mtu kumsaili neno tena tokea hapo,” Mk 12:34 

TAFAKARI: Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele.” 

Wapendwa wana wa Mungu, mwanadamu kwa kuumbwa kwake, Mwa 1:27, na uwepo wake hapa duniani, mara zote hutafuta maana ya maisha yake. Hufanya hivyo si kwa bahati mbaya, au udadisi fulani, bali kama alivyo, mwanadamu ni tokeo la historia  yake na kijamii na jamii anayoishi leo na sasa. Hivyo, mwanadamu huyu hapo alipo kadiri ya imani na maadili yake, hakosi kuifikiria kesho ambayo bado kuiishi akiwa na matumaini kuwa ipo. Na kama ni Mkristo achoki kuyafikiria maisha yale ya umilele na hukumu yake ya mwisho, kwa sababu anatambua wazi maisha ya hapa nduniani ni jukumu la muda mfupi tu. Kwa maana imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya,” 2Kor 5:10

Kwa hali na mtazamo huo, mwanadamu hakosi kutafuta maana ya maisha yake. Utafutaji wa maana juu ya maisha yake humpa pia maana ya mahangaiko na mateso yake. Katika hali hii Mtume Paulo anasema, Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi,” 2Tim 2:9. Neno la Mungu ni hai, na pia ni uhai. Tulisadiki neno kama alivyofanya Diwani yule wa Kana ya Galilaya, Yoh 4:46, mwanaye aliyekuwa hajiwezi, naye akapata uponyaji. Yesu akamwambia, Enenda; mwanao yu hai. Mtu yule akalisadiki lile neno aliloambiwa na Yesu, naye akashika njia,” Yoh 4:50 

Maisha yakikosa maana, binadamu hujikabidhi katika ‘ovu’ lolote lile bila kujali chochote kwa sababu maisha yake kesha yahesabu kuwa si chochote. Huku ni kutaka tamaa pale tunapokosa tumaini la kweli. Ila kwa upande wa Mtume Paulo ni tofauti. Yesu Kristo ndiye nahodha wa maisha yake, na kwake, yaani kwa Kristo, maisha yake (Paulo Mtume) yamepata maana halisi. Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele. Ni neno la kuaminiwa. Kwa maana, Kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia; Kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; Kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi; Kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe,” 2Tim 2:10-13. Huyu ndiye Kristo ambaye kwake kama wafuasi wake, kuna tumaini la kweli.

Hata pamoja na ukweli huo, Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli,” 2Tim 2:15. Ndani na katika Yesu Kristo hakuna sababu ya kuishi kwa hofu. Mmoja wa waandishi ili kupata uhakika na kuiondoa hofu yake, anamuuliza Yesu, Katika amri zote ni ipi iliyo ya kwanza?” Mk 12:28b. Swali hili ni la msingi kabisa, ingawa yawezekena muuliza swali alifanya hivyo ili kujiridhisha na pengine kujua ameegemea upande upi. Ni vizuri pia kujihakiki kama kweli unatembea njia iliyo salama. Yesu akamjibu, Ya kwanza ndiyo hii, Sikia, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja; nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote,” Mk 12:29-30. Jibu la Yesu linamkumbusha muuliza swali kuwa yeye ni tokeo la historia yake, na hivyo historia hiyo ina nguvu katika maisha yake.

Yesu hakuishia hapo tu, bali anaenda mbele zaidi ile muuliza swali afahamu vizuri ubinadamu wake. Maisha huwa na maana unapoishi tumaini la kweli, yaani, kuelekea ule umilele ambalo ndilo lengo kwa yeyote yule aishie duniani hapa. Naye Yesu anamwambia,  Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi,” Mk 12:31. Kumbe mimi na wewe siyo tu tokeo la historia yetu, bali pia masisha ya kijamii tunayoishi kila siku. Hapa duniani hatuishi kama visiwa. Mahusiano yetu (ya haki, kweli, usawa, upendo) na wenzetu utujenga kimaadili na imani, na hivyo kutufanya kukua kiroho. Huu pia ni mtihani muhimu sana wa kujipatia taji lile la gharama kupita mataji yote, yaani, utakatifu wako. Bila hili kuiona Mbingu na Mungu ni ndoto! Kuhusu historia yake, na mahusiano yake na wenzake, mwaandishi yule alijibu vyema, Mk 12:32-33. Naye Yesu, alipoona kwamba amejibu kwa busara, alimwambia, Wewe hu mbali na ufalme wa Mungu. Wala hakuthubutu mtu kumsaili neno tena tokea hapo,” Mk 12:34. Ndugu yangu, wewe na mimi tuutafakari umbali wetu na ufalme ule wa Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Naye Yesu, alipoona kwamba amejibu kwa busara, alimwambia, Wewe hu mbali na ufalme wa Mungu. Wala hakuthubutu mtu kumsaili neno tena tokea hapo,” Mk 12:34


Tusali:-Ee Yesu Mwema, nijalie ufahamu wa kuona maana ya maisha yangu kila siku licha ya changamoto nazokumbana nazo kila kukicha. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario