martes, 24 de mayo de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 8 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 8 YA MWAKA-C
Somo: 1Pet 2:2-5, 9-12
Zab: 100:2, 3, 4, 5
Injili: Mk 10:46-52
Nukuu:
“Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima,” 1Pet 2:4 

 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu,” 1Pet 2:9 

 “Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili zipiganazo na roho,” 1Pet 2:11 

Naye aliposikia ya kwamba ni Yesu Mnazareti, alianza kupaza sauti yake, na kusema, Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu,” Mk 10:47

Yesu akamjibu, akamwambia, Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu wangu, nataka nipate kuona,” Mk 10:51 

TAFAKARI: “Wakata nikufanyie nini?”

Wapendwa wana wa Mungu, tupo wengi akina Bartimayo, mwana wa Timayo, Yule mwombaji kipofu wa Yeriko, Mk 10:46. Hakika kilio chake Bartimayo “Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu” Mk 10:47, alipousikia ule msafara wa Yesu ukipita, kinaonyesha ni kwa namna gani alivyokuwa amechoshwa na hali yake ile. Licha ya watu kumzuia, Yesu anasikia kilio kile na kutaka kumwona. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, ni wazi kuna nyakati nyingine unakumbwa na matatizo na unapoomba wajisikia kama vile sala yako haisikiki kabisa. Ukweli ni kwamba Yesu Mwana wa Mungu aliye hai anasikia kilio chako, hivyo usiache kumwita. Hata Bartimayo licha ya kusongwa na kundi na msafara ule hakukoma kumwita Yesu. Je, unajua utakacho akufanyie Yesu atakapokuuliza?

Yesu kabla ya kumpa uponyaji Bartimayo, anamuuliza, “Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu wangu, nataka nipate kuona,” Mk 10:51. Yesu bila kukawia kwa kuiona imani yake Bartimayo pasipo shaka yoyote anajibu ombi lake hapo hapo nakumwambia, Enenda zako, imani yako imekuponya. Mara akapata kuona; akamfuata njiani,” Mk 10:52. Kwa uponyaji huu wa moja kwa moja, Bartimayo siyo tu anapata kuona kutoka upofu wake, bali anaona njia sahihi ya kuifuata na yenye usalama, “mara akapata kuona, akamfuata njiani.” Bartimayo anatufundisha na kutukumbusha fundisho la Yesu, kwamba, ‘Yeye ndiye njia, na ukweli, na uzima,’ Yoh 14:6.

Unapopata kuona njia kwa macho ya kiroho ni sawa na kuzaliwa upya. Ni kushibishwa nuru ile iangazayo katika kweli halisi. Ni msukumo wa neema ndani yako unaoangaza na kuyaona yale yaliyo juu ya uwezo wako kiakili kama wanadamu. Neema ya Mungu ndani na kwa njia yake Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai, utuwezesha na kutuongoza kuyafikia yale Mungu anayotamani sote siku moja kuyafikia. Hivyo ndugu yangu, “Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima,” 1Pet 2:4. Jiwe hili ndilo Kristo Yesu Mwana wa Mungu aliye hai.

Kwa Sakramenti ya Ubatizo miili yetu inakuwa Hekalu la Roho Mtakatifu, na viungo wa Kristo kama Kanisa. Kwa Sakramenti ya Ubatizo tunashirikishwa ukuhani wa kawaida wa Yesu Kristo. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo,” 1Pet 2:5. Licha ya kuwa makuhani wa kawaida wa Kristo, kwa Sakramenti ya Ubatizo, tu wa milki ya Mungu katika nuru ya ajabu-wana wa Mungu aliye Mtakatifu. Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu,” 1Pet 2:9. Tu wana wa nuru na kwa sababu hiyo ndicho alichokijia Yesu. Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani,” Yoh 12:46.

Kuishi katika nuru hii aliyotuletea Yesu Kristo ni kutenda na kupenda tunda la Roho. “Tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria,” Gal 5:22-23. Kuishi tunda la Roho kunatuhesabia haki na Mungu mwenyewe kuwa taifa lake na kupata rehema zake.  “Ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema,” 1Pet 2:10. Hivyo tukielewa hapa duniani tu wapitaji na wasafiri, kuendelea kuneemeka na rehema hizi za Mungu kama sehemu ya maandalizi ya maisha yale ya umilele, yakupasa wewe na mimi kuziepuka tamaa za mwili zinazopingana na tunda la Roho. Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili zipiganazo na roho,” 1Pet 2:11. Matendo ya mwili na tamaa zake utuweka kando na nuru ya Mungu, na kwayo hakuna Mbingu. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Ndugu yangu, tafakari na chukua hatua!

Mwaliko wa Kristo kwangu na kwako leo ni kwamba tuwe na mwenendo mzuri, na tusomwe kwa matendo yetu mazuri ili watenda mabaya wabadilike na kumtukuza Mungu. Wapendwa katika Kristo, Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa,” 1Pet 2:12. Huku ndiko kuusulibisha mwili ndani na katika Kristo Yesu kama asemavyo Mtume Paulo, Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake,” Gal 5:24. Tu katika yote ndani na katika Kristo Yesu. Je, wauonea huruma Mwili wako na mwisho kuiangamiza Nafsi na Roho?

Tumsifu Yesu Kristo! 

Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili zipiganazo na roho,” 1Pet 2:11


Tusali:-Ee Yesu, Mwana wa Mungu aliye hai, niwezeshe niweze kuona nuru yako yenye kuangaza umilele wa maisha yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario