SHEREHE YA BIKIRA MARIA KWENDA KUMWAMKIA ELIZABETI
Somo: Sef 3:14-18a.
Zab: Isa 12:2-3, 4abc, 5-6
Injili: Lk 1:39-56
Nukuu:
“Bwana
ameziondoa hukumu zako, Amemtupa nje adui yako; Mfalme wa Israeli, naam, yeye
Bwana, yu katikati yako; Hutaogopa uovu tena,” Sef 3:15
“Bwana,
Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; Atakushangilia kwa furaha
kuu, Atakutuliza katika upendo wake, Atakufurahia kwa kuimba,” Sef 3:17
“Elisabeti akajazwa
Roho Mtakatifu; akapaza sauti kwa nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake,
naye mzao wa tumbo lako amebarikiwa,” Lk 1:41b-42
“Mariamu
akasema, Moyo wangu wamwadhimisha Bwana, Na roho yangu imemfurahia Mungu,
Mwokozi wangu; Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama,
tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa; Kwa kuwa Mwenye nguvu amenitendea
makuu, Na jina lake ni takatifu,” Lk 1:46-49
TAFAKARI: “Moyo wangu wamwadhimisha Bwana, Na roho yangu
imemfurahia Mungu, Mwokozi wangu.”
Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anatambua ushiriki wa Mama
Bikira Maria katika safari nzima ya wokovu wetu, na hivyo anaadhimisha siku
hii, tendo lile ya Bikira Maria kwenda kumwamkia mpwa wake Elizabeti. Mama
Bikira Maria naheshimiwa sana na kutukuzwa katika Kanisa letu Katoliki siyo kwa
sababu ya uzuri wake, au upekee wake wa ajabu kama mwanamke, bali kwa
unyenyekevu wake, hasa kwa kuwa tayari kuyapokea yote licha ya kutokujua nini
hasa kitakachofuata au tokea katika maisha yake. Bikira Maria anaishinda hofu
ile ya sintofahamu. Ukweli huu unajidhihirisha kwa maneno haya mazito ya Bikira
Maria, “mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema,”
Lk 1:38a. Maneno haya ya Mama yetu Bikira Maria, ni
fundisho tosha ya kujiachia pasipo kujibakiza, hasa katika mazingira ya yale
tusiyoelewa sawa sawa.
Leo tunaposherehekea siku ile Bikira Maria alipokwenda kumpasha habari
Mpwa wake Elizabeti, itukumbushe kudumisha ujirani mwema. Ujirani mwema
hudumishwa kwa kuwa na moyo safi, Lk 1:46-47. Moyo usio jilimbikizia maovu.
Moyo uliyotayari kuona mazuri mara zote kwa watu wote. Moyo usipungukiwa kiti
kwa nyakati zote na shida zote. Moyo uliyo tayari kutaambika kwa ajili ya
wengine. Usafi wa moyo huu, ni tiketi ya kuuona uso wa Mungu. Moyo usio na
hatia una nafasi kubwa sana kumwaona Mungu. Moyo huu una heri kama asemavyo
Bwana wetu Yesu Kristo, “Heri wenye moyo safi; Maana hao watamwona Mungu,” Mt 5:8.
Mama yetu Bikira Maria pamoja na kuhesabiwa haki hiyo ya kuwa Mama wa Mungu,
nafasi hiyo haikuwa sababu ya kujivunia, bali kujinyenyekesha katika udogo wa
hali ya chini kabisa. Kujinyenyekesha kwake huku kuna kuwa chanzo cha
mawasiliano ya kimungu kati ya fumbo lile lilikokuwa limejificha kati ya kile
kilichokuwa tumboni mwake, yaani, Neno kufanyika Mwili na kukaa kwetu, na kile
kilichokuwa kimeandaliwa kwa ajili ya kuitaarisha njia ya Neno hili, yaani,
Yohani Mbatizaji. Na mambo yalikuwa hivi, “Ikawa
Elisabeti aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu, kitoto kichanga kikaruka ndani
ya tumbo lake,” Lk 1:41. Huu ni uthibitisha wa ubebaji wa Habari Njema
aliyokuwa nayo Mama Bikira Maria. Je, wewe ni habari njema hapo ulipo? Hatuwezi
kuwa habari njema kama tu wafuasi wa majungu. Wengi wetu tumebeba mimba za
majungu na kwa namna hiyo hatuwezi kuwa habari njema hata kama tutajifungua.
Ndugu yangu, palipo
habari njema, Roho Mtakatifu aliye umoja na tunda la upendo wa Mungu Baba na
Mwana, hutuunganisha katika umoja wa kweli, na usio na unafiki. Na hivi ndivyo
ilivyotokea kwa mpwa wake Bikira Maria, Elizabeti. “Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu; akapaza
sauti kwa nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo
lako amebarikiwa,” Lk 1:41b-42. Roho Mtakatifu ndiye anayezungumzu ndani ya
Elizabeti. Ndugu yangu, hata pale ambapo hatuna cha kusema ila tumejiachia bila
kujibakiza kwa Kristo Yesu, Roho Mtakatifu utusemea na kutushuhudia. Katika
hili Yesu anasema, “nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa
ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Lakini hapo watakapowapeleka,
msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho
wa Baba yenu asemaye ndani yenu,” Mt 10:18-20. Mawasiliano haya kati ya Mama
Bikira na Mpwa wake Elizabeti ni mawasiliano yenye Umungu ndani yake.
Naye
bila kujibakiza, Bikira Maria anayasema yaliyo moyoni mwake, “Moyo
wangu wamwadhimisha Bwana, Na roho yangu imemfurahia Mungu, Mwokozi wangu; Kwa
kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi
vyote wataniita mbarikiwa; Kwa kuwa Mwenye nguvu amenitendea makuu, Na jina
lake ni takatifu,” Lk 1:46-49. Mama Bikira Maria kwa tendo hili anaona mpango
mzima wa Mungu ndani yake. Pamoja na Mpango huo, Mama Bikira Maria hakuwa na
sababu ya kujivuna na kujiinua zaidi ya kujinyenyekesha mbele za Mungu. Tendo
hili linamtafakarisha Mama Bikira Maria kuyaona makuu ya Mungu kupitia kwake.
Naye anasema, “Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na
wanyonge amewakweza,” Lk 1:52. Akiwa mnyonge na mwenye kutostahili chochote
zaidi ya kuwa mtumishi wa Bwana, Mama Bikira Maria anapata fursa ya kumshukuru
Mungu na kulitukuza jina lake daima kwa kuutazama upya unyonge wa watu wake na
taifa lake. “Amemsaidia Israeli, mtumishi wake; Ili kukumbuka rehema
zake; Kama alivyowaambia baba zetu, Ibrahimu na uzao wake hata milele,” Lk
1:54-55. Hakika Mama Bikira Maria ni kielelezo cha fadhila ya unyenyekevu.
Hivyo kama kuna sababu ya kujisifu tujisifu kwa mambo ya udhaifu wetu kama
asemavyo Mtume Paulo, 2Kor 11:30. Na penye udhaifu ndipo penye nguvu, 2Kor
12:10. Ni kwa unyenyekevu tu tunaweza kuona udhaifu wetu.
Wapendwa wana wa Mungu, unyenyekevu huu kama ulivyo wa Mama
yetu Bikira Marian dio unaoweza kutuondolea hukumu ya Mungu pale tunapomkosea
Mungu na kuwa tayari kuanza upya Naye kwa njia ya toba ya kweli na majuto.
Unyenyekevu wetu huujenga upya ukaribu wetu na Mungu na kwa namna hivyo Mungu
yupo tayari kughairi hukumu yake kwetu. “Bwana
ameziondoa hukumu zako, Amemtupa nje adui yako; Mfalme wa Israeli, naam, yeye
Bwana, yu katikati yako; Hutaogopa uovu tena,” Sef 3:15. Mungu kamwe hafurahii kuangamia kwetu kama
asemavyo Nabii Isaya, “Mtu mbaya na
aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye
atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa,” Isa 55:7. Ndugu
yangu, “Bwana, Mungu wako, yu katikati yako
shujaa awezaye kuokoa; Atakushangilia kwa furaha kuu, Atakutuliza katika upendo
wake, Atakufurahia kwa kuimba,” Sef 3:17. Sifa na Utukufu kwa Mungu wetu ajuaye
mwisho wa maisha yetu. Amini.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Bwana
ameziondoa hukumu zako, Amemtupa nje adui yako; Mfalme wa Israeli, naam, yeye
Bwana, yu katikati yako; Hutaogopa uovu tena,” Sef 3:15
Tusali:- Ee Mama Bikira
Maria, tujalie unyenyekevu wako ili nasi tufumbuliwe siri na mpango wa Mungu
katika maisha yetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario