domingo, 29 de mayo de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 9 YA MWAKA-C

JUMATATU WIKI YA 9 YA MWAKA-C
Somo: 2Pet 1:2-7
Zab: 91:1-2, 14-15b, 15c-16
Injili: Mk 12:1-12
Nukuu:
kwa wale waliopata imani moja na sisi, yenye thamani, katika hali ya Mungu wetu, na Mwokozi Yesu Kristo,” 2Pet 1:1b

 “Na katika kutamani watajipatia faida kwenu kwa maneno yaliyotungwa; ambao hukumu yao tangu zamani haikawii, wala uvunjifu wao hausinzii,” 2Pet 1:3 

 “Hata kwa wakati wake akatuma mtumwa kwa wale wakulima, ili apokee kwa wakulima katika matunda ya mizabibu,” Mk 12:2 

Basi alikuwa na mmoja bado, mwana mpendwa wake; huyu naye akamtuma kwao mwisho, akisema, Watamstahi mwanangu,” Mk 12:6 

Lakini wale wakulima wakasemezana, Huyu ni mrithi; haya, na tumwue, na urithi utakuwa wetu,” Mk 12:7 

Wakamkamata, wakamwua, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu,” Mk 12:8 

TAFAKARI:Jiwe walilolikataa waashi, Hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni.”

Wapendwa wana wa Mungu, ufunuo wa wazi wa Mungu katika historia ya wokovu wetu imekamilishwa kwa tendo lile la kumwilishwa, yaani, neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Tendo hili linakuwa mtikisiko mkubwa kwa watu wengi, na hasa wale ambao hawakuwa katika njia ya kweli na haki. Ni wazi kabisa tendo hili la kumwilishwa kwa neno linaubadilisha mtazamo mzima wa maisha, na tumaini jipya la wale wote Mungu aliowaridhia. Kwa kupitia Musa, watu walipata tumaini kwa kuishika torati. Ila kwa kupitia Kristo, neema na kweli likazaliwa tumaini jipya na mwanzo mpya. Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:17. Hivyo mtikisiko wa wazi unaonekana kwa wale wote waliojihesabia haki na kuhodhi mamlaka kama wao ndio miungu watu.

Injili ya leo inaeleza historia nzima ya wokovu wetu hadi, kilele chake kikiwa ni ufunuo wa wazi wa Mungu kwa watu wake, yaani Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu. Mfano wa wakulima katika shamba la mizabibu unatupa taswira halisi ya wale waliokuwa wapinzani wa mpango huo wa wokovu wa Mungu. Wapinzani hawa amboa walijihesabia haki na kujitwalia nafasi ya Mungu na  kuwa miungu watu, ndio waliowaangamiza wale wote waliolitangulia Neno, yaani, Bwana wetu Yesu Kristo. Kundi hili kabla ya Neno ndilo lililowachukua Mababa wa Imani, Manabii mbalimbali, na waamuzi. Hata kwa wakati wake akatuma mtumwa kwa wale wakulima, ili apokee kwa wakulima katika matunda ya mizabibu,” Mk 12:2. Hata hivyo hawa wote waliuwawa.
Mungu hakuchoka, kukata tamaa, na wala kusitisha nia yake ya kumkomboa mwanadamu. Basi alikuwa na mmoja bado, mwana mpendwa wake; huyu naye akamtuma kwao mwisho, akisema, Watamstahi mwanangu,” Mk 12:6. Jambo la kushangaza mambo hayakuwa hivyo kutokana na ugumu wa mioyo ya watu, na hasa Wayahudi. Kwa kusukumwa na ubinafsi wao (ikia ni pamoja na mila na desturi zao) na kutetea maslahi yao kama miungu watu, Mwana huyu ya Mungu asiye na kosa wakamfanya kama walivyowafanya watangulizi wake. Lakini wale wakulima wakasemezana, Huyu ni mrithi; haya, na tumwue, na urithi utakuwa wetu,” Mk 12:7. Lengo hapa ni kulinda maslahi yao, na kuendelea kudumu katika dhambi. Yesu Kristo anawaambia yote haya na sisi leo, kwa lengo la kubadili mwelekeo wa maisha na kuanza naye upya kwani kwake lipo tumaini la kweli na lililojaa neema.

Hata hivyo, kwa kuing’ang’ania dhambi na furaha zake, Wakamkamata, wakamwua, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu,” Mk 12:8. Na haya ndiyo mauti yaliyomfika mtu yule mwenye haki, ambaye ndiyo Kristo mwenyewe kwa kifo kile cha Msalaba. Na hili ndilo jiwe la Msingi ambalo kwalo kila ajengaye nyumba juu yake (Imani juu ya Mwana wa Mungu), nyumba hiyo itakuwa imara daima. Na hili ndilo itimisho ya andiko lile kwamba, Jiwe walilolikataa waashi, Hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni,” Mk 12:10. Maneno haya ya Yesu kwa wakuu wa makuhani, na waandishi, na wazee, Mk 11:27,  yanazua tafrani kubwa kwani yaliwachoma vizuri ndani ya mioyo yao. Kama ni ujumbe, ulifika na kupokelewa! Hivyo wakatafuta kumkamata, wakaogopa mkutano; maana walitambua ya kwamba ule mfano amewanenea wao. Wakamwacha wakaenda zao,” Mk 12:12. Ndugu yangu, hii ni moja ya changamoto ya Imani yetu, hasa pale tunapopambana na giza kwa kuileta nuru ya kweli.

Kwa kuishi kweli ahadi zako za Ubatizo ni mwitikio wa wazi wa kupambana na lile lililo giza na gizani. Ni kuwa tayari kuyapokea na kuyapata yote aliyompata Kristo kwa sababu, Kulikuwako Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu, akija katika ulimwengu. Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea,” Yoh 1:9:11. Je, katika hali hii mimi na wewe tufanye nini?

Mpendwa katika Kristo, simulizi alilolitoa Yesu latukumbusha ni kwa namna gani mpango wa Mungu ulivyokuwa kuhusu wokovu wetu, na lina lengo la kuviendeleza vita hivi vya imani bila kuogoba. Nuru yapasa kuwa nuru ili giza lisiwepo. Hivyo mimi na wewe kwa kuwa nuru kuna mapaswa na sadaka yake. Basi pale tunapokuwa nuru kwa mapaswa na sadaka yake, isiwe sababu ya kuhuzunika wala kujiona tumesahauliwa na Mungu, bali tufurahi katika hali hiyo. Kwetu na iwe heri. Naye Yesu anasema hivi pale tutakapopatwa na hali hiyo, kwamba, “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu,” Mt 5:11-12. Hapa tunahesabiwa haki na kuwa na dhawabu kubwa mbinguni.

Mitume, na hata wafuasi katika jumuiya ile ya kwanza ya Wakristo, hawakuacha kuwa nuru pale walipokuwa licha ya ugumu wa mazingira ya wakati ule. Mtume Petro haachi kujitambulisha katika Imani ya kweli ndani na katika Kristo kwa watu kama asemavyo,   kwa wale waliopata imani moja na sisi, yenye thamani, katika hali ya Mungu wetu, na Mwokozi Yesu Kristo,” 2Pet 1:1b. Leo mimi kuwa Mkristo bila kielezo hai cha Kristo ndani yangu, ni sawa na kutokuishi nuru ile halisi ya Kristo ndani yangu. Kwa kutokufanya hivyo, Mtume Petro anasema, wengi watafuata ufisadi wao; na kwa hao njia ya kweli itatukanwa,” 2Pet 1:2. Kristo hatoheshimika kabisa mbele za watu, na hasa kwa matendo ya kifisadi yanapofanywa na wale ambaye hujishuhudia mbele za watu kama Wakristo. Moja ya uwepo wa nuru halisi ndani ya maisha yetu ni kule kuwa watu wa haki, na watetezi wa haki kama Kristo Yesu alivyofanya na hata kuifia haki hiyo ili mimi na wewe leo tuwe huru. Huku ni kuishi tumaini la kweli ndani na katika Kristo pale ulipo na kadiri ya wito wako. Kwa kutokufanya hivyo ukijua kwa faidi binafsi ni kujiandalia hukumu. Na katika kutamani watajipatia faida kwenu kwa maneno yaliyotungwa; ambao hukumu yao tangu zamani haikawii, wala uvunjifu wao hausinzii,” 2Pet 1:3. Je, Mungu hupendezwa haya yatokee kwako bila kusema lolote?

Wapendwa wana wa Mungu, dhamiri yako ndiyo mwalimu wako wa ndani. Dhamiri safi ni mwalimu wa kweli na haki ndani yako. Bila shaka mwalimu huyu ndani yako ni uwepo wa nguvu za Mungu ndani yako zenye lengo la kukufikisha pale Mungu alipo. Ni kwa maana hiyo kwamba, Mungu hakuwaachilia malaika waliokosa, bali aliwatupa shimoni, akawatia katika vifungo vya giza, walindwe hata ije hukumu; wala hakuuachilia ulimwengu wa kale, bali alimhifadhi Nuhu, mjumbe wa haki, na watu wengine saba, hapo alipoleta Gharika juu ya ulimwengu wa wasiomcha Mungu,” 2Pet 1:4-5. Ndugu yangu, hukumu utakayoipata kwa kutokuitii sauti ya Mungu ndani yetu, yaani, ile dhamiri hai na njema ndani yetu, itakuwa nimeiandaa wenyewe kwa kujua. Hapa ndipo kwenye kulia na kusaga meno (Mt 8:12, 13:42, 50, 22:13, 24:51, 25:30, Mk 9:18, na Lk 13:28), maana yake, hutakuwa na jambo lolote la kujitetea. Na hivi ndivyo ilivyokuwa juu ya miji ile ya Sodoma na Gomora, kwamba,  akaihukumu.., akiipindua na kuifanya majivu, akaifanya iwe ishara kwa watu watakaokuwa hawamchi Mungu baada ya haya,” 2Pet 1:6.

Wapendwa wana wa Mungu, heshimu na kuitii dhamiri yako njema. Walizitii dhamiri zao na kusimama katika kweli na haki, Mungu aliwaepusha na aina zote za ufisadi na mwisho akawahesabia haki. Ni kwa namna hiyo, Mungu  akamwokoa Lutu, yule mwenye haki aliyehuzunishwa sana na mwenendo wa ufisadi wa hao wahalifu,” 2Pet 1:7. Basi tuenenda kama wana wa Nuru kwa kuwa na hofu ya Mungu ndani yetu. Amina.

Tumsifu Yesu Kristo! 

“Huyu ni mrithi; haya, na tumwue, na urithi utakuwa wetu. Wakamkamata, wakamwua, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu,” Mk 12:7b-8


Tusali:-Ee Yesu, uliye neema na kweli, tuwezesha mara zote kuishi katika neema hiyo na kweli hiyo kila siku ya maisha yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario