sherehe ya moyo mtakatifu wa yesu-C
somo
I: Eze 34:11-16
Zab:
23, (K) 1
Somo
II: Rum 5:5 -11
Injili:
Lk 15:3-7
Nukuu:
“Maana,
Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi mwenyewe, naam, mimi, nitawatafuta kondoo
zangu, na kuwaulizia,” Eze 34:11
“Mimi
mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami nitawalaza, asema Bwana MUNGU,” Eze
34:15
“Nami
nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika,
nitawatia nguvu wagonjwa; nao wanono na wenye nguvu nitawaharibu; nitawalisha
hukumu,” Eze 34:16
“Kwa
maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili
ya waovu,” Rum 5:6
“Bali
Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa
ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi,” Rum 5:8
“Basi
zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu
kwa yeye,” Rum 5:9
“Wala
si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo,
ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho,” Rum 5:11
“Ni
nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini
na kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hata amwone?” Lk 15:4
“Nawaambia,
Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja
atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya
kutubu,” Lk 15:7
TAFAKARI:
“Moyo Mtakatifu wa Yesu ni thibitisho wazi la huruma ya Mungu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhmisha sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Kimantiki
sherehe hii ilipaswa kuadhimishwa siku ile ya Ijumaa Kuu, kwa sababu siku ile
ulimwengu mzima ulijionea jambo hili, yaani, “Mwana wa Mungu kuinuliwa
msalabani, na kujitoa mwenyewe kwa ajili ya kutupenda sisi. Kwa tendo hilo la
kutukuka lenye kubeba neema na huruma ya Mungu, alichomwa ubavu akamwaga damu
na maji, zipate kutoka humo Sakramenti za Kanisa. Na kwa namna hivyo, sote
tuvutwe na huo Moyo wazi wa Mwokozi, na kuchota kwa furaha neema katika
chemchemi ya wokovu.” Hiki ndicho kwa hakika tukisherehekeacho leo. Hata hivo
kwa mazingira yale ya Ijumaa Kuu yalighubikwa na majonzi makubwa na kutokupata
nafasi ya kuutafakari kwa undani Moyo huu Mtakatifu wa Yesu. Leo ndiyo siku
yake.
Maisha ya Bwana wetu
Yesu Kristo hapa duniani, na hasa ile miaka yake mitatu aliyoitumia kupandikiza
neno la uzima kwetu, mambo makuu matatu yalijidhihirisha pasipo shaka katika
Moyo wake huu Mtakatifu. Moja, kutafuta kile kilichopotea. Katika kutafuta kile
kilichopotea, Yesu anasema wazi mbele za watu sababu ya mahangaiko yake, na
kusema, “Wenye
afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi; sikuja kuwaita wenye haki, bali
wenye dhambi,” Mk 2:17. Ni upendo wa hali ya juu sana, Mungu aliyemwilishwa
pamoja na ukamilifu wake, yupo tayari kuwa karibu na mkosefu (mwenye dhambi) na
kufanya naye urafiki ili ampate katika kweli na haki. Mungu yupo tayari muda na
wakati wowote kuwa karibu na mkosefu ili ampate. Hapa ndipo tunapoweza kuona
kwa undani huruma ya Mungu tunapoyatafakari maneno haya: “Mtu mbaya na aache
njia yake Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye
atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa.” Isa 55:7.
Mungu aliye hai na
mwenye kusafiri nasi katika historia nzima ya wokovu wetu, huyaona mateso na
mahangaiko yetu. Yupo nasi katika kila jambo, na yote tuyapatayo au kutokea,
yanakusudi la Mungu hata pale tunaposhindwa kujua sababu yake kwa kadiri ya
ufahamu wetu, kama asemavyo Mungu, “mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zanu
si njia zangu.” Isa 55:8. Njia za Mungu ni tofauti na njia za mwanadamu. Njia
zetu zimethibitiwa na nafasi na wakati, ilhali njia za Mungu zipo katika
umilele wake. Na ndiyo “maana, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi mwenyewe,
naam, mimi, nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia,” Eze 34:11. Mungu hachoki
kukutafuta licha ya uovu wako. Ukiona umeufia uovu wako ujue ni chaguo la uhuru
wako bila shinikizo lolote. Ni uhuru na utashi wako, na umefikia hapa ulipo kwa
kuheshimu na kuutendea haki uhuru na utashi wako licha ya kwamba tokeo lake ni
chukizo kwa Muumba wako.
Mungu
wetu tunayemwamini utulisha yaliyo mema, ila baada ya kushiba umtendea yaliyo
maovu. Naye asema hivi, “Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami
nitawalaza,” Eze 34:15. Kutokuukubali utawala wa Mungu na kulazwa naye katika
nuru ya kweli na haki ni kukengeuka ukijua kuwa Yeye ndiye aliyetuumba kwa sura
na mfano wake, Mwan 1:27. Hata hivyo Mungu huyu aliye Upendo na Huruma hachoki
kututafuta hata pale unapomkana. Naye anasema, “Nami
nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika,
nitawatia nguvu wagonjwa; nao wanono na wenye nguvu nitawaharibu; nitawalisha
hukumu,” Eze 34:16. Ndugu yangu, hata
hukumu hii ya Mungu aitoayo ni
tokeo la Upendo mtupu. Ona jinsi Mungu anavyoangaika nawe. Huu ndiyo Moyo
Mtakatifu Yesu. Moyo usiochoka kukutafuta hata kuwambwa juu ya Msalaba kwa
sababu yako na yangu. Ujumbe Mkuu wa Moyo huu ni huu: “hakuna aliye na upendo
mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh
15:13. Hakika Moyo Mtakatifu wa Yesu ni bubujiko lisilo kifani la huruma ya
Mungu.
Pili,
miaka ile mitatu ya mwisho ya Yesu hapa duniani inathibitisha jambo hili;
“utayari wake wa kujitoa kwa ajili ya kile kilichopotea. Hapa ndipo tunapouona
utii wa Mungu kwa mwenye dhambi. Hii ni neema na huruma ya hali ya juu kwetu
wenye dhambi. Katika hili Mtume Paulo anatuambia hivi juu ya Yesu; “tena,
alipoonekana ana umbo kama la mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti,
naam, mauti ya msalaba,” Flp 2:8. Je, wathamini hilo alilokutendea Yesu kwa
sababu tu anakupenda kama ulivyo? Ndugu yangu, lazima uelewe jambo hili,
kwamba, “Kwa
maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili
ya waovu,” Rum 5:6. Je, mimi nimekamilika? Kama nimekamilika, je, mazingira
yangu na tenda kwa watu wangu ina akisi upendo huu alionifia Kristo? Ukweli ni
kwamba, “Mungu
aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili
yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi,” Rum 5:8. Sadaka yangu kila siku ni kuwa
mwaminifu pale nilipo, na kuvuja damu kila siku kwa kujitoa vilivyo kwa kile
nikifanyacho kama moja ya huduma na kuwajibika kwangu. Kutafuta huruma mbele za
watu ili kuonekana mwema ni kupoteza muda na neema ya Mungu ndani yako. Huu
ndio mchezo haramu na usiopendeza mbele ya Mungu unaofanywa na viongozi wetu,
hasa wa kisiasa kucheza na hisia zetu.
Wapendwa wana wa Mungu,
mwanadamu hata kwa hali yake ya utakatifu hawezi kukuhesabia haki mbele za
Mungu, kwani naye katika hali hiyo bado anahitaji huruma na neema ya Mungu. Kwa
nini basi watafuta huruma mbele za watu na kumwacha Bwana Mungu wako
anayekuhesabia haki? Kama Wakristo na wafuasi wake waaminifu wa Kristo, kwa
matendo yetu mema yenye kuubeba wokovu, yaweza kutunahesabiwa haki kwa damu
yake iliyomwagika pale Msalabani na si vinginevyo. Katika hili Mtume Paulo anasema, “Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika
damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye,” Rum 5:9. Kuokolewa katika ghadhabu hii ni pamoja na
kupatanishwa naye. Ndugu yangu, Moyo Mtakatifu wa Yesu ni uthibitisho wa
upatanishi wetu na Mungu. Moyo huu ndiyo uliowezesha patanisho hilo kwa sadaka
yake pale Msalabani. Ni kwa namna hiyo mimi na wewe leo, “twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu
Kristo, ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho,” Rum 5:11. Hakika
Kristo Yesu ni daraji imara la upatanisho wetu na Mungu.
Tatu, miaka ile mitatu
ya mwisho ya Yesu hapa duniani inathibitisha furaha ya Mungu, na hasa kwa
mwenye kutubu na kuacha njia yao mbaya. Furaha ya Mungu ni kuanza naye upya, na
Yeye utuchukulia katika upya wetu bila kuyahesabu yaliyopita. Mungu usamehe
yote bila kuhoji historia yake tufanyapo toba ya kweli na majuto. Mfano mzuri
ni wa yule Mwana Mpotevu, Lk 15:11-32. Katika hili Yesu anazihoji dhamiri zetu
katika kweli na haki, na kusema, “Ni nani
kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na
kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hata amwone?” Lk 15:4. Ujumbe hapa ni kwamba, wewe na mimi
kama Viiongozi tuwe tayari kukitetea kile kilicho dhaifu kwa sababu furaha ya
kweli ni sote tuwe salama. Kama kiongozi ni wajibu wako wote wafike salama
asipotee hata mmoja. Kiongozi anayekimbilia ukamilifu wa wachache, na
kuwapoteza wengu na wakati mwingine bila kujua “kulikoni,” kiongozi huyo ni
dhaifu sana. Kamwe Mungu hawezi kufurahia tendo hilo kwa sababu hata huyo
unayemuona si mkamilifu kwa vigezo vya kibinadamu, ilhali mtu huyu yupo tayari
kuiacha njia yake mbaya na kumrudia Mungu, ila wewe kwa kuishikilia sheria,
tena mbovu haupo tayari kufikiri nje ya sheria ile. Ndugu yangu, tambua kwamba
mtu huyo ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Na kwa sababu hiyo Mungu hachoki
kutafuta kile kionekacho dhaifu na kilichopotea. Katika hili Yesu anasema, “Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa
ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na
kenda ambao hawana haja ya kutubu,” Lk 15:7
Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka
waweza kuona ni kwa namna gani Moyo huu wa Yesu Mtakatifu tunao usherehekea leo
ulivyobeba uzito wa ubinadamu wetu, ile wewe na mimi tuhesabiwe haki.
Tunahesabiwa haki si kwa matendo yetu mema tu na ukaribu wetu mbele ya Mungu,
bali kwa utayari wetu wa kuona udhaifu ndani yetu na kufanya toba ya kweli na
majuto ambayo kwa kutenda dhambi ndiyo sababu kubwa ya teso la Moyo huu
Mtakatifu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Bali
Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa
ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi,” Rum 5:8
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, uniumbie Moyo safi, uifanye upya Roho iliyotulia ndani yangu,
usinitenge na uso wako, Wala roho wako mtakatifu
usiniondolee. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario