domingo, 31 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 4 YA MWAKA-C

JUMATATU WIKI YA 4 YA MWAKA-C

Somo: 2Sam 15:13-14, 30, 16:5-13
Zab: 3:2-7
Injili: Mk 5:1-20
Nukuu:
Daudi akamwambia Abishai, na watumishi wake wote, Angalieni, huyu mwanangu, aliyetoka viunoni mwangu, anautafuta uhai wangu; si zaidi Mbenyamini huyu sasa? Mwacheni alaani, kwa sababu Bwana ndiye aliyemwagiza,” 2Sam 16:11 

Labda Bwana atayaangalia mabaya yaliyonipata, naye Bwana atanilipa mema kwa sababu ya kunilaani kwake leo,” 2Sam 16:12

akapiga kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha kwa Mungu usinitese,” Mk 5:7 

Akawapa ruhusa. Wale pepo wachafu wakatoka, wakaingia katika wale nguruwe; nalo kundi lote likatelemka kwa kasi gengeni, wakaingia baharini, wapata elfu mbili; wakafa baharini,” Mk 5:13 
Wakaanza kumsihi aondoke mipakani mwao,” Mk 5:17

lakini hakumruhusu, bali alimwambia, Enenda zako nyumbani kwako, kwa watu wa kwenu, kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi alivyokurehemu,” Mk 5:19 

Akaenda zake, akaanza kuhubiri katika Dekapoli, ni mambo gani makuu Yesu aliyomtendea; watu wote wakastaajabu,” Mk 5:20

TAFAKARI:Kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi alivyokurehemu.”    

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna kati yetu asiye na jambo lolote la kumshukuru Mungu hata kama tumesongwa na dhiki ya kupindukia. Kushukuru kwa jambo lolote lile ni kuomba pia. Ni mara ngapi sala zetu zimekuwa na muono wa kushukuru? Mfalme Daudi anasongwa na upinzani mkubwa kutoka nje na ndani ya ufalme wake. Pamoja na hali hiyo, Mfalme Daudi hatoi nafasi ya kumlaumu Mungu. Kusamehewa  kifo kwa kosa la kuzina na mke wa Uria, hakukumwondolea upanga dhidi ya Ufalme wake. Bwana Mungu akasema, Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako,” 2Sam 12:10.

Mtoto wake wa kumzaa, Absalomu anakuwa mwiba mkali katika ufalme wake. Mfalme Daudi anakosa ujasiri na kuingiwa hofu na amani kutoweka. Huyu ndiye aliyemua Goliathi kwa jiwe. Daudi akamwambia Abishai, na watumishi wake wote, Angalieni, huyu mwanangu, aliyetoka viunoni mwangu, anautafuta uhai wangu; si zaidi Mbenyamini huyu sasa?” 2Sam 16:11a. Mfalme Daudi anatambua wazi matendo aliyomtendea Mungu na kujikwaa kwake. Hivyo kila kinachomtokea kina sababu na mkono wa Mungu ndani yake. Alipodhihakiwa njia na mtu asiyemjua alikotoka, Mfalme Daudi alijibu, Mwacheni alaani, kwa sababu Bwana ndiye aliyemwagiza. Labda Bwana atayaangalia mabaya yaliyonipata, naye Bwana atanilipa mema kwa sababu ya kunilaani kwake leo,” 2Sam 16:11b-12. Mfalme Daudi pamoja na kuujua ukweli huu, hakukata tamaa na wala hakumwasi Mungu.

Injili ya leo inaubeba ujumbe kama wa Mfalme Daudi ila kwa mtazamo mwingine. Hapa tunakutana na uponyaji wa mtu aliyeteswa na kundi kubwa la pepo. Hata walipoulizwa mpo wangapi haikuwa rahisi tutoa jibu la haraka. Badala yake walijibu, ‘Legioni, kwa kuwa walikuwa wengi.’ Uwepo wa Yesu ni vita dhidi ya uovu. Ni vita vya mwanga dhidi ya giza. Jina la Yesu linatisha. Jina hili ni tishio dhidi ya Shetani na mamlaka yake. Ni kwa sababu hiyo, mtu yule alipomwona Yesu, akapiga kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha kwa Mungu usinitese,” Mk 5:7. Pepo wachafu wanatambua nguvu na mamlaka aliyokuwa nayo Yesu, na wanajua vita dhiki yake hawatashinda. Je, unaliamini jina hili Tukufu na Kuu kuliko Majina Yote?

Na hali ilivyozidi kuwa mbaya, pepo wale waliomba na kujisalimisha chini ya Mamlaka ya jina hili kuu, kwa kuwaingia nguruwe. Akawapa ruhusa. Wale pepo wachafu wakatoka, wakaingia katika wale nguruwe; nalo kundi lote likatelemka kwa kasi gengeni, wakaingia baharini, wapata elfu mbili; wakafa baharini,” Mk 5:13. Ukiangalia tendo hili alilofanya Yesu kiuchumi la kuwaruhusu wale pepo kuwaingia wale nguruwe waweza kutafsiri kwamba Yesu hakutenda haki kwa mfugaji wa wale nguruwe. Ndugu yangu, viumbe vyote ni mali ya Mungu, na Yeye Mungu anamamlaka yote juu ya viumbe vyake vyote. Na maandiko Matakatifu yanatuambia, Neno huyu alifanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:2. Hivyo Yesu alikuwa na mamlaka yote na uamuzi wake ulikowa sahihi.

Kwa upande mwingine, tendo hili la Yesu linathibitisha upekee na thamani ya mwanadamu kati ya viumbe vyote. Na sababu kubwa ni kwamba Mungu alipenda na kuchakua kumuumba mtu kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kiumbe huyu, yaani mwanadamu imebeba chapa ya Mungu ndani yake. Binadamu anastahili heshima kubwa licha ya tofauti za kibinadamu tunazojiwekea, na zinazotokana na utofauti wa kimaisha, na kwa makusudi kabisa tunaruhusu zitugawe kimatabaka. Pamoja na upekee huu aliokuwa nao Mwanadamu, kamwe Mwanadamu huyu hawezi kumshurutisha Mungu atende kadiri atakavyo yeye. Kwani “Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake,” 1Sam 2:6-8. Kumbe kila alitendalo Bwana lina sababu yake katika umilele wake.

Kama tendo la shukrani, mtu yule aliyewekwa huru na Yesu kutoka mamlaka ya shetani, anaomba kuandamana ya Yesu. Lakini Yesu hakumruhusu, bali alimwambia, Enenda zako nyumbani kwako, kwa watu wa kwenu, kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi alivyokurehemu,” Mk 5:19. Ndugu yangu, unapotambua mkono wa Mungu katika maisha yako, anza hapo hapo kutoa ushuhuda huo na kulisifu jina la Bwana. Mtakatifu Fransisko wa Assis wakati fulani alisema, ‘hakuna sababu ya kwenda sehemu fulani na kuhubiri, ila tuhubiri kadiri tutembeavyo.’ Kwa upande mwingine, katazo hili ya Yesu kwa mtu huyu asiandamane naye linalenga kukoleza Imani ya kweli sehemu ile Mungu aliyokutendea makuu yake. Hivyo mtu yule akaenda zake, akaanza kuhubiri katika Dekapoli, ni mambo gani makuu Yesu aliyomtendea; watu wote wakastaajabu,” Mk 5:20. Ndugu yangu, wewe na mimi tunayo mengi ya kutoa shukrani kwa Mungu. Basi anza hapo ulipo.

Tumsifu Yesu Kristo!

Ee Bwana, Mungu wangu, uangalie, uniitikie; Uyatie nuru macho yangu, Nisije nikalala usingizi wa mauti,” Zab 13:3


No hay comentarios:

Publicar un comentario