ALHAMISI WIKI YA 3 YA MWAKA-C
Somo: 2Sam 7:18-19, 24-29
Zab: 132:1-5, 11-14
Injili: Mk 4:21-25
Nukuu:
“Kwa kuwa wewe, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli
umenifunulia mimi, mtumwa wako, ukisema, Nitakujengea nyumba; kwa hiyo mimi,
mtumwa wako, nimeona vema moyoni mwangu nikuombe dua hii,” 2Sam 7:27
“Na sasa, Ee Bwana MUNGU, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako
ndiyo kweli, nawe umemwahidia mtumwa wako jambo hili jema,” 2Sam 7:28
“basi, sasa, uwe radhi, ukaibarikie nyumba ya mtumwa wako,
ipate kudumu milele mbele zako; kwa maana wewe, Ee Bwana MUNGU, umelinena na
kwa baraka yako nyumba ya mtumwa wako na ibarikiwe milele,” 2Sam 7:29
“Kwa maana hakuna neno
lililositirika, ila makusudi lije likadhihirika; wala hakuna lililofichwa, ila
makusudi lije likatokea wazi,” Mk 4:22
“Akawaambia, Angalieni
msikialo; kipimo kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa,” Mk
4:24
“Kwa maana mwenye kitu
atapewa, naye asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang'anywa,” Mk 4:25
TAFAKARI: “Kipimo kile mpimacho
ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa.”
Wapendwa wana wa Mungu, hakuna binadamu asiyetaka kupendwa na
hakuna asiyeyajua maumivu ya kutokupendwa. Upendo ni sehemu muhimu sana kwa mtu
yeyote yule ikiwa ni pamoja na makuzi yake. Upendo wa kweli utuweka pia karibu
na viumbe vile visivyo na utashi, mathalani; paka na mmbwa. Tunapowaonyesha
upendo wa dhati viumbe hivi visivyo na utashi hutambua upendo huo na kwa namna
moja au nyingine hurudisha upendo huo kwetu. Je, kama viumbe hivi visivyo na utashi
urudisha upendo kwetu kwa yale tunayowafanyia itakuwaje vizuri na vyema
tukipendana sisi kwa sisi?
Tumeumbwa ili tuwe na ushirika wa kweli sisi kwa sisi. Hivyo
hakuna aishiye kama kisiwa bali tunategemeana katika kukamilishana. Ukamilisho
huu huja pale tunapotambua uwezo na mapungufu yetu. Hivyo kujitoa kwa ajili ya
mwingine ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Hii ndiyo changamoto ya upendo
kwamba ujitoavyo ndivyo navyo utakavyokirimiwa siku ile ya mwisho. ‘Kipimo cha
upendo ni kupenda bila kipimo,’ Mt. Augustino. Naye Yesu “Akawaambia, Angalieni msikialo; kipimo kile mpimacho ndicho
mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa,” Mk 4:24. Je, usipofanya chochote juu ya
jirani yako ili hali unajua wajibu huu itakuaje? Katika jambo hili Yesu
anasema, “Kwa maana mwenye kitu atapewa, naye asiye na kitu, hata kile
alicho nacho atanyang'anywa,” Mk 4:25. Mwenye kitu ni yule anayetambua anao
wajibu wa kufanya zaidi kwa ajili ya wengine. Na asiye na kitu ni yule
anayefikiri hana wajibu wa kufanya chochote kwa ajili ya wengine na hasa wenye
uhitaji. Kwa hawa kundi la pili Yesu anasema, “hata kile alicho nacho
atanyang’anywa.”
Ndugu
yangu, lazima tuelewa kwamba siyo sisi tuliyeanza kumpenda Mungu, bali ni Mungu
mwenyewe alianza kutupenda, na kwa pendo hilo alichagua kutuumba kwa sura na
mfano wake, Mwa 1:27. Hivyo kupenda ni amri ya Mungu mwenyewe aliyoiweka ndani
mwetu. Hivyo upendo huo lazima uzae matunda kwa kujitoa kwa wengine bila
kujibakiza. Na Yesu analisema jambo hili kwa ufasaha, “Si ninyi mlionichagua
mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda;
na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu
awapeni,” Yoh 15:16. Ndugu yangu lazima ufanya kitu kwa ajili ya baraka na
neema Mungu anazokujalia kila siku.
Mfalme
Daudi baaba ya kuupokea ujumbe ule wa Mungu kutoka kwa Nabii Nathani juu ya
ujenzi wa nyumba ya Mungu, Daudi anauchukua wajibu huo kama sehemu muhumu
katika Ufalme wake. Naye anasema, “Kwa kuwa wewe, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli umenifunulia
mimi, mtumwa wako, ukisema, Nitakujengea nyumba; kwa hiyo mimi, mtumwa wako,
nimeona vema moyoni mwangu nikuombe dua hii,” 2Sam 7:27. Maneno ya Mungu kwetu
ni kweli na tena ni uhai. Kulifanya akuagizalo Mungu ni kutimiza kweli hiyo ya
Mungu ndani yako na kuupata uhai huo ambao ni mali ya Mungu na zawadi kwako. “Na sasa, Ee Bwana MUNGU, wewe ndiwe Mungu, na
maneno yako ndiyo kweli, nawe umemwahidia mtumwa wako jambo hili jema,” 2Sam
7:28. Ni furaha iliyoje kuyafanya yale yampendezayo Mungu?
Hakuna shaka ya baraka na neema za Mungu pale tuyafanyapo
mapenzi ya Mungu bila kujibakiza.
Tulivyo navyo vyote ni mali yake mwenyewe na tunapovitumia kwa mapenzi yake
ndivyo tunavyozidishiwa na kubarikiwa zaidi. “Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote
wakaao ndani yake,” Zab 24:1. Je una kilicho chako zaidi ya dhambi zako? Hivyo
kwa kulitambua hili, Mfalme Daudi anasema, “basi, sasa, uwe radhi, ukaibarikie nyumba ya mtumwa wako,
ipate kudumu milele mbele zako; kwa maana wewe, Ee Bwana MUNGU, umelinena na
kwa baraka yako nyumba ya mtumwa wako na ibarikiwe milele,” 2Sam 7:29. Ndugu
yangu, hakuna aliyekuwa masikini kwa kutoa, na ndivyo ilivyo kwa baraka huvuta
baraka.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Azitegemeaye mali zake ataanguka; Mwenye haki atasitawi kama
jani,” Mit 11:28
No hay comentarios:
Publicar un comentario