JUMATANO WIKI YA 2 YA MWAKA-C
20/1/2016
Somo: 1Sam 17:32-33, 37, 40-51
Zab: 144:1b, 2, 9-10
Injili: Mk 3:1-6
Nukuu:
“Daudi akamwambia
Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako
nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu,” 1Sam 17:32
“Sauli akamwambia
Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana
tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake,” 1Sam 17:33
“Daudi akasema, Bwana
aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti
huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe,” 1Sam 17:40
“Akaichukua fimbo yake
mkononi, akajichagulia mawe laini matano katika kijito cha maji, akayatia
katika mfuko wa kichungaji aliokuwa nao, maana ni mkoba wake, na kombeo lake
alikuwa nalo mkononi mwake, akamkaribia yule Mfilisti,” 1Sam 17:40
“Mfilisti akamwambia
Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa
miungu yake,” 1Sam 17:43
“Mfilisti akamwambia
Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa
mwituni,” 1Sam 17:44
“Ndipo Daudi
akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali
mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli
uliowatukana,” 1Sam 17:45
“Siku hii ya leo Bwana
atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo
nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili
kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli,” 1Sam 17:46
“Nao jamii ya watu
wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni
vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu,” 1Sam 17:47
“Daudi akatia mkono
wake mfukoni, akatwaa humo jiwe moja, akalitupa kwa kombeo lake, akampiga Mfilisti
katika kipaji cha uso; jiwe hilo likamwingilia kipajini, akaanguka chini
kifudifudi,” 1Sam 17.49
“Hivyo Daudi
akamshinda yule Mfilisti kwa kombeo na jiwe, akampiga Mfilisti, akamwua;
walakini Daudi hakuwa na upanga mkononi mwake,” 1Sam 17:50
“Ndipo Daudi akapiga
mbio, akasimama juu ya Mfilisti, akautwaa upanga wake, akaufuta alani mwake,
akamwua, akamkata kichwa kwa upanga huo. Nao Wafilisti walipoona ya kuwa shujaa
wao amekufa, wakakimbia,” 1Sam 17:51
“Akaingia tena katika
sinagogi; na palikuwako huko mtu mwenye mkono uliopooza; wakamvizia ili kuona
kama atamponya siku ya sabato; wapate kumshitaki,” Mk 3:1-2
“Akamwambia yule mtu
mwenye mkono uliopooza, Simama katikati,” Mk 3:3
“Akawauliza, Ni halali
siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya? Kuponya roho au kuiua?
Wakanyamaza,” Mk 3:4
“Akawakazia macho
pande zote kwa hasira, akiona huzuni kwa ajili ya ugumu wa mioyo yao,
akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Naye akaunyosha; mkono wake ukawa mzima
tena,” Mk 3:5
“Mara wakatoka wale Mafarisayo,
wakawa wakifanya shauri juu yake pamoja na Maherodi, jinsi ya kumwangamiza,” Mk
3:6
TAFAKARI: “Mimi ninakujia wewe kwa
jina la Bwana wa majeshi. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana
haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana.”
Wapendwa wana wa Mungu, Mungu wetu hakufanya makosa
kutuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Ni kwa namna hiyo ilimpendeza
kutuumba na kuweka chapa yake ndani yetu nasi leo ni wanadamu. Ni kwa ubinadamu
wetu huu hadi siku ya mwisho wa uhai wetu hapa duniani ndivyo Mungu anapenda
tuwe. Ni tatizo kubwa sana pale tunapokataa ubinadamu wetu na kutaka kuwa kitu
kingine. Binadamu anapoukataa ubinadamu wake anakuwa mbaya kuliko shetani. Hata
wale Malaika waliomwasi Mungu walitaka kuwa zaidi ya kile walichoumbwa kuwa na
hivyo wakageuka kuwa Mashetani.
Binadamu anapokataa kuwa kile alicho kadiri ya uwezo na
mipaka ya Mungu aliyependezwa awe, na kibinadamu huyo kuchukua nafasi ya Mungu
hugeuka kuwa Shetani. Huku ndiko kuasi kulikofanywa na Msalaika. Ushetani wa
mtu ni mtu mwenyewe! Shetani ni roho, kwayo yenyewe haiwezi kufanya chochote
nje ya mtu bila kuikubali roho hiyo. Shetani kama roho hufanya kazi ndani ya
mtu kama mwezeshaji wa ile roho. Hivyo, “shetani wa mtu ni mtu mwenyewe.”
Mara nyingi kinachotuponza kutokuukubali ubinadamu wetu na
mapungufu yake ni yale tunayoyapokea kutoka kwa watu na namna wansemavyo juu
yetu. Hapa ndipo sifa ujijengea mizizi, umaarufu unapokuzwa, uwezo unapoabudiwa
kwa wale wanaokupaka mafuta kwa mgongo wa chupa, na nafasi ya pesa na utajiri
unaposhika hatama. Yeyote yule anayeyakubali haya na kuyafanya kuwa sehemu ya
maisha yake, hatochelea kuwa Shetani. Kama wabisha jaribu!
Waisraeli wanapatwa hofu juu ya Goliathi ambaye alikuwa
tishio kubwa kwao. Historia ya Goliathi ilikuzwa sana na watu waliamini juu ya
uwezo wake bila kuona nguvu na uwezo wa Mungu. Hivyo Sauli Mfalme anamwambia
Daudi kuhusu Mfilisti huyu aliyekuwa tishio kwao, “huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u
kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake,” 1Sam 17:33. Daudi kijana
shupavu aliyeyaweka yote mikononi mwa Mungu, na mwenye hofu ya Mungu, anaona
lililo kuu na zaidi ya mwanadamu na fahari yake. Naye anamwambia Mfalme Sauli,
“Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono
wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja
nawe,” 1Sam 17:40. Huku ndiko kumtumaini
Mungu kuliko kweli na haki. Maji uliyoyavulia nguo lazima kuyakoga!
Tunapojikabidhi kwa Mungu
bila kujibakiza hasa katika nyakati hizi zilizojuu ya uwezo wetu, Mungu hutumia
yale yaliyokawaida ndani ya uwezo wetu na kutimiza hazma yake iliyo kweli ndani
yetu. Anayepigana vita hii kwa asilimia zote 100 ni Mungu mwenyewe. Wewe na
mimi kwa upande wetu ni vyombo vya amani yake Mungu kama aombavyo Mtakatifu
Fransisko, “Bwana unifanya chombo cha amani yako.” Hivyo Daudi “Akaichukua fimbo yake mkononi, akajichagulia mawe laini matano
katika kijito cha maji, akayatia katika mfuko wa kichungaji aliokuwa nao, maana
ni mkoba wake, na kombeo lake alikuwa nalo mkononi mwake, akamkaribia yule
Mfilisti,” 1Sam 17:40. Mpinzani wake Goliathi
kutokana na uzoefu wake wa vita na sifa alizojichotea na kumvimbisha kichwa
aliona ziaka kubwa kufanywa na Daudi. Anayepigana vita hivi vya kweli na haki
si Daudi bali Mungu mwenyewe. Kwa dharau kubwa Goliathi anaukataa ubinadamu
wake na kusema maneno mazito juu ya Mungu anayemtumia Daudi mtumishi wake, “Je!
Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake.
Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa
angani na wanyama wa mwituni,” 1Sam 17:43-44.
Daudi anayejua ni Mungu
gani anayemtumikia hakuwa na hofu juu ya Mungu wake. Daudi hana shaka kabisa na
kile akifanyacho kwa sababu anajua uwezo wa Mungu anayemwamini na kumtumikia. “Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na
upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa
majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana,” 1Sam 17:45. Silaha kubwa ya
mtu ni unyenyekevu wake juu ya kile kilicho nje ya uwezo wake. Binadamu licha
ya uwezo na akili zake bado kuna sintofahamu ndani ya ufahamu wake. Ni Mungu tu
mwenye kukamilisha hiki ambacho bado hakijafunuliwa kwa binadamu. Ndiyo maana
kwa ufahamu wetu na mahesabu zetu twaweza kupanga yote na mwisho wa siku
yakaenda kinyume na ufahamu wetu na mahesabu zetu. Ndugu yangu bado huamini
kuna kitu zaidi ya ufahamu wako?
Pamoja na
vitisho vyote vya Goliathi, Daudi habadilishwi na kile anachokiamini juu ya
Mungu anayemtumikia. Daudi kijana mdogo
sana na asiyeshikika katika mikono ya Goliathi anamwambia Goliathi, “Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga,
na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa
nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko
Mungu katika Israeli,” 1Sam 17:46. Ndugu
yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, kamwe usitangulize mbele chochote
kile wasemacho watu juu yako zaidi ya Mungu anayewezesha hayo wasemayo watu juu
yako. Daudi anayafanya hayo yote si kwa kulitukuza jina lake, bali Mungu
ainuliwe juu zaidi na ulimwengu wote ufahamu nafasi ya Mungu. Tumwache Mungu
aitwe Mungu ndugu zangu. Watu wanapokusifia ni vyema kulichukulia jambo hilo
kama jaribu kubwa kati ya uhusiano wako na Mungu. Ni vyema kujibu hivi,
“Tumshukuru Mungu, na sote tubarikiwe!”
Wapendwa wana wa Mungu,
yule aliyejulikana kama kikaka wa vita na kupata medali nyingi za ushindi wa
kivita anasitishwa kwa jiwe moja tu la Daudi. “Daudi akatia mkono
wake mfukoni, akatwaa humo jiwe moja, akalitupa kwa kombeo lake, akampiga
Mfilisti katika kipaji cha uso; jiwe hilo likamwingilia kipajini, akaanguka
chini kifudifudi,” 1Sam 17.49. Ndugu zangu wapendwa, mara nyingi binadamu
anapochagua kuwa shetani na kuukataa ubinadamu wake hutegemea vitu ambavyo vipo
chini ya uwezo wake. Na kwa ajabu Mungu uthibitisha kwetu kwamba hivyo
tunavyovitegemea haviwezi kamwe kutuokoa. Mungu huyu aliliangamiza jeshi kubwa
la wamisri kwa maji tu. “Yale maji yakarudi yakafunikiza magari na wapanda farasi, hata
jeshi lote la Farao lililoingia katika bahari nyuma yao; hakusalia hata mtu
mmoja. Kwa
maana farasi za Farao na magari yake na wapanda farasi wake waliingia ndani ya
bahari, Bwana akayarudisha maji ya bahari juu yao; bali wana wa Israeli
walikwenda katika nchi kavu katikati ya baharí,” Kut 14:28, 15:19
Ndugu
yangu unaweza kuchezea haki za watu kwa kujificha nyuma ya kivuli cha mitutu,
vifaru vya kijeshi, na magari ya maji washa washa ili kuzima sauti zao, ila ipo
siku Mungu atasimama na kusema inatosha juu ya watu wangu unaowanyanyasa. Hapo
ndipo kwenye kulia na kusaga meno. Jambo la kufahamu ni hili, “mara zote elewa
kwamba wewe siyo kipimo cha ukweli kwa hayo unayoyalazimisha yawe kwa manufaa
yako na kile ukiwakilishacho kisicho kweli na haki, iwe jamii au chama chako
cha siasa.” Mungu mara zote huzungumza na watu. “Kwa
kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo
katikati yao,” Mt 18:20.
Kifo cha Goliathi ni jibu la Mungu kwamba sasa inatosha juu
wa watu wangu wanaoteseka bila sababu. Goliathi awe mfano wetu wa kujifunza
mipaka yetu na namna yetu ya kuenenda juu wa wale Mungu aliowaumba kwa sura na
mfano wake. Kwa “maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga,” Mt
26:52b. Kwa kadiri tutumiavyo njia mbovu kukandamiza haki za watu ni kwa njia
hiyo hiyo tutakavyofikwa na umauti. “Ndipo Daudi akapiga
mbio, akasimama juu ya Mfilisti, akautwaa upanga wake, akaufuta alani mwake,
akamwua, akamkata kichwa kwa upanga huo. Nao Wafilisti walipoona ya kuwa shujaa
wao amekufa, wakakimbia,” 1Sam 17:51. Kile alichokuwa anakitegemea Goliathi
kuwaangamiza watu wa Mungu ndicho Daudi alichokitumia kuhitimisha udhalimu
wake. Hakika wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga!
Wapendwa
wana wa Mungu, Mungu wetu hututakia mema muda wote. Tatizo letu ni pale
tunapotaka Mungu kufanya kadiri tuonavyo sisi. Tatizo kubwa ndani ya utashi
wetu ni kwamba mara nyingi hatuoni vitu kama vilivyo bali huviona kama tulivyo.
Injili ya leo Yesu anaturudisha katika makusu ya Mungu mwenyewe naye akiwa
Mungu, yaani, Neno aliyefanyika mwili na kukaa kwetu. Ni kweli isiyo shaka
kwamba mara nyingine ufahamu wetu unagota kwenye mila na desturi zetu na
kutufanya kuendana na mitazamo hiyo ambayo haina uhai ndani yake zaidi ya ufu.
Yesu hafanyi lolote kwa kujificha. “Akamwambia yule mtu mwenye mkono uliopooza, Simama katikati,” Mk
3:3. Kila mtu lazima aone yale ayafanyao
Yesu. Yote ayafanyayo Yesu katika maisha yetu siyo mazingaumwe. Ni kweli kabisa
wapo baadhi yetu kwa kuyakuza majina yao uishia katika nguvu za giza na kuvaa
miwani ya Kristo. Mwisho ya hayo yote wanayoyaigiza huwa aibu yao.
Yesu hachoki kutuelekeza
kwa kile kilicho haki na kweli mbele ya Mungu na uzima wetu wa milele. Yesu
anauliza swali la msingi sana juu ya mila na desturi zetu juu ya uhai ambao ni
mali ya Mungu na zawadi ya Mungu kwetu. “Akawauliza, Ni halali
siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya? Kuponya roho au kuiua?
Wakanyamaza,” Mk 3:4. Kwa namna nyingine Yesu anakuuliza wewe na mimi hivi: “je
kile unachokiamini kinakuzuia kutenda lililo jema ambalo kwa uhalali ni zaidi
ya kile unachokiamini?” Mila na desturi zetu zinaitaji kutakatifuzwa kwa sababu
zimejawa hofu nyingi bila maelezo ya kina kwani lengo lake huwa utiii bila
kuhoji. Utii upofu. Na ukitaka kuchunguza kwa undani mila hizi zilikuwa kwa
manufaa ya wale walioziweka au kuzifanya. Pamoja
na ukweli kwamba Yesu hakupata jibu ya swali lake, Yesu hakuacha kufanya lililo
jema mbele ya Mungu Baba na watu wake kwa hofu ya macho ya watu na misimamo
yao. “Akawakazia macho pande zote kwa hasira, akiona huzuni kwa ajili
ya ugumu wa mioyo yao, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Naye akaunyosha;
mkono wake ukawa mzima tena,” Mk 3:5. Ndugu yangu uliyesafari nami katika
tafakari hii, ukweli utatuweka huru na si vinginevyo. “Ninyi mkikaa katika neno
langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena
mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru,” Yoh 8:31-32
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni
ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani?” Zab 27:1
No hay comentarios:
Publicar un comentario