lunes, 18 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 2 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 2 YA MWAKA-C
19/1/2016
Somo: 1Sam 16:1-13
Zab: 98:20, 21-22, 27-28
Injili: Mk 2:23-28
Nukuu:
Lakini Bwana akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo,” 1Sam 16:7 

Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku,” 1Sam 16:11 

Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye,” 1Sam 16:12 

Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama,” 1Sam 16:13 

Akawaambia, Sabato ilifanyika kwa ajili ya mwanadamu, si mwanadamu kwa ajili ya sabato,” Mk 2:27 

Basi Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato pia,” Mk 2:28

TAFAKARI: “Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni mang’amuzi yangu na bila shaka yako pia kwamba Mungu hutenda mambo makuu kwa watu ambao kadiri ya mtazamo wetu uliojijenga katika mila na desturi utushangaza kabisa.  Huyu ndiye Mungu kama asemavyo Mama Bikira Maria, Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52. Mungu wetu aliye haki, upendo, huruma na wema kamwe hatendi na kutazama kama sisi wanadamu. Tatizo kubwa la mwanadamu huwa haoni vitu kama vilivyo, bali huviona vitu kama alivyo yeye. Ni kwa mantiki hii mtu husongwa na mila na desturi zilizomkuza katika maamuzi yake.

Baada ya Sauli kukosa sifa mbele za macho ya Mungu, Mungu anafanya zaidi kwa manufaa ya watu wake. Hivyo Mungu anawachagulia tena Mfalme wana wa Israeli. Samweli mtumishi wa Mungu anapewa maelekezo na Mungu na anafanya kadiri ya maelekezo hayo. Yese alikuwa na wana wazuri na wenye uwezo. Pamoja na hayo yote, Mungu anamchagua yule amtakaye kwa makusudi yake. Baada ya kukosekana yule amtakaye Mungu, Samweli mtumishi mwaminifu anamuuliza Yese, “Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku,” 1Sam 16:11

Mtazamo wa leo na msukumo wa kijamii na kisiasa ni vigumu sana kusikia sauti ya Mungu ndani ya mioyo yetu. Tunaishi sana katika ushabiki na wakati mwingine tunaingiwa upofu na kutokuona vitu sawasawa. Leo si jambo la ajabu kuona mtu asiyependwa na watu ndiye anayetangazwa kuwa mshindi na aliyechakuliwa na watu. Demokrasia yetu leo kwa nchi zenye mfumo wa kimla ni kwamba wengi usema ila baadhi ndio wanaoamua. Udhalimu huu hauna nafasi mbele ya Mungu. Kilicho cheupe na kiwe cheupe na kilicho giza na kitambulike kuwa giza. Kwa nini tunatanguliza nafsi zetu mbele zaidi ya kile atakacho Mungu kupitia watu wake?

Mungu wetu hatazami kama sisi tutazamavyo katika hulka na ushabiki wetu. Mungu hufanya kadiri na ukamilifu wake. Nasi kama wanadamu tunaalikwa kila siku kuwa wakamilifu kama alivyo Mungu wetu. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mk 5:48. Ni vyema ufahamu uwepo wako hapa duniani. Ndugu yangu unanyesafiri nami katika tafakari hii elewa kwamba upo hapa nduniani kupigana kufa na kupona juu ya cheo chako ambacho ni utakatifu wako. Mengine yote na fahari zake ni mbwembe tu. Huwezi kumwona Mungu kama si mtakatifu. Je, unajua hilo?

Hivyo, Daudi anapata sifa mbele za Mungu ingawa hakuwa matarajio ya familia ya Yese. Lakini Bwana akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo,” 1Sam 16:7. Mungu utazama moyo ule unaomwelekea na kufanya mapenzi yake. Na katika jambo hili, kutenda lililo jema hakuwezi kugubikwa na mila na desturi zetu.

Leo katika Injili Yesu anatukumbusha lililo la muhimu. Ni kweli mila na desturi zetu zina umuhimu wake, ila sauti ya Mungu ni muhimu zaidi kwa sababu ndiyo hatma yetu. Wanafunzi wa Yesu wanakoselewa na kulaumiwa kwa kufanya lisilo sahihi siku ya sabato kadiri ya mapokeo ya kiyahudi. Yesu anawajibu, “Sabato ilifanyika kwa ajili ya mwanadamu, si mwanadamu kwa ajili ya sabato,” Mk 2:27. Utu wa mtu ni kitu cha kwanza kabisa kutazama zaidi ya mitazamo. Ndani ya mtu kuna chapa ya Mungu ndani yake. Mtu lazima aheshimiwe kama alivyo bila kuangalia nafasi na cheo chake katika jamii. Hivyo Kristo ndiye sababu ya yake yote kuyafanyayo.Basi Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato pia,” Mk 2:28. Kristo amekuja kuitakatifuza sheria na kuikamilisha. Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza,” Mt 5:17. Binadamu na utu wake kwanza, mengine yafuate.

Tumsifu Yesu Kristo


Toka mbinguni Bwana huchungulia, Huwatazama wanadamu wote pia. Toka mahali pake aketipo Huwaangalia wote wakaao duniani,” Zab 33:13-14

No hay comentarios:

Publicar un comentario