JUMATATU, KIPINDI CHA NOELI
4/1/2016
Somo: 1Yoh 3:7-10
Zab: 97:1, 7-8, 9
Injili: Yoh 1:35-42
Nukuu:
“Watoto wadogo, mtu na
asiwadanganye; atendaye haki yuna haki, kama yeye alivyo na haki,” 1Yoh 3:7
“atendaye dhambi ni wa
Ibilisi; kwa kuwa Ibilisi hutenda dhambi tangu,” 1Yoh 3:8
“Katika hili watoto wa
Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki
hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake,” 1Yoh 3:10
“Akamtazama Yesu akitembea, akasema, Tazama, Mwana-kondoo wa
Mungu!” Yoh 1:36
“Yesu aligeuka, akawaona wakimfuata, akawaambia, Mnatafuta nini?
Wakamwambia, Rabi, (maana yake, Mwalimu), unakaa wapi?” Yoh 1:38
“Akawaambia, Njoni, nanyi mtaona. Wakaenda, wakaona akaapo,
wakakaa kwake siku ile. Nayo ilikuwa yapata saa kumi,” Yoh 1:39
“Andrea, nduguye Simoni Petro, alikuwa mmoja wa wale wawili
waliomsikia Yohana na kumfuata Yesu,” Yoh 1:40
“Huyo akamwona kwanza Simoni, ndugu yake mwenyewe, akamwambia,
Tumemwona Masihi (maana yake, Kristo),” Yoh 1:41
“Akampeleka kwa Yesu. Naye Yesu akamtazama, akasema, Wewe u
Simoni, mwana wa Yohana; nawe utaitwa Kefa (tafsiri yake Petro, au Jiwe),” Yoh
1:42
TAFAKARI: Yesu akawaambia, Mnatafuta
nini? Wakamwambia, Rabi, (maana yake, Mwalimu), unakaa wapi?” Yoh 1:38
Wapendwa wana wa Mungu, kila mmoja wetu kwa kuishi kwake
hapa duniani utafuta maana ya maisha yake. Kwa maana nyingine yote uyafanyayo
mwisho wake nini? Yohane Mbatizaji akiwa na wanafunzi wake wawili anamwona Yesu
kwa mbali na kusema, “Tazama, Mwana-kondoo wa
Mungu!” Yoh 1:36. Kwa maneno haya, Yohane Mbatizaji anaona hitimisho lote kwa
Yesu. Huyu ndiye tumtazamiaye na tumtafutaye kwani kwake upo ukamilisho wote.
Pamoja na ukweli huu, Yesu anauliza swali la msingi kabisa, ‘Mnatafuta nini?’
Kwa maana nyingine Yesu anataka kujua haya kutoka kwako na kwangu; pamoja na
mahangaiko uliyonayo nini msingi wa maisha yako? Nini kisukumacho maisha yako
na kufanya ufanyavyo? Na mwisho, nini hatma ya hayo yote? Maisha ya mtu yaweza
kuongozwa na hali zifuatazo ambazo kwa uhakika hali hizo hazitatupeleka kule
Yesu aliko na anapotaka tuwe.
1. Watu wengi huongozwa na hatia.
Watu hawa hutumia muda wa maisha yao yote wakiepuka
lawama na kuficha aibu. Watu wanaoongozwa na hatia wanaonewa sana na
kumbukumbu. Wanaruhusu mambo yaliyopita kutawala mambo yao ya usoni. Wanajiadhibu
bila kujua kwa kuharibu mafanikio yao. Kaini alipotenda dhambi, hatia yake
ilimtenga na Mungu, na Mungu akasema, "utakapoilima ardhi haitakupa mazao
yake; utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani," Mwa 4:12. Hii
inawaeleza jinsi watu wengi walivyo siku hizi-wanatangatanga katika maisha bila
lengo. Mfano mzuri angalia katika vyama vyetu vya kitume. Wapo walio wengi
huama chama kimoja cha kitume kwenda kingine na mwisho huishia katika nyumba za
sala. Nyumba za sala hapa ninamaanishisha vijikanisa vinavyojiibua na kujiinua
kwa wachungaji wao kuwa manabii.
Ndugu yangu, sisi ni matokeo ya muda wetu uliopita
lakini hatupaswi kuwa wafungwa wa muda huo. Kusudi la Mungu halifungwi na muda
wako uliopita. Ona! Alimbadilisha muuaji Musa na kuwa kiongozi mzuri;
akambadilisha Gidioni aliyekuwa mwoga akawa shujaa na hodari; anaweza kufanya
mambo ya ajabu na maisha yako yaliyobaki. Tazama pia maisha ya
Mt. Augustino wa Hippo kabla na baada ya kuongoka kwake.
Mungu ni mtaalam wa
kutupa mawazo mapya. "Heri aliyesamehewa dhambi, na kusitiriwa makosa
yake," Zab 32:1. Kwa maana nyingine twaweza kusema, "wana furaha
kubwa wale waliosamehewa hatia zao. Na wana amani wale waliotubu dhambi zao na
Mungu amefuta mashtaka yao." Ni kwa Kristo tu tupo huru tunapoziungama dhambi
zetu. “Watoto wadogo, mtu na asiwadanganye; atendaye haki yuna
haki, kama yeye alivyo na haki; atendaye
dhambi ni wa Ibilisi; kwa kuwa Ibilisi hutenda dhambi tangu,” 1Yoh 3:7-8.
2. Watu wengi wanaongozwa na chuki na hasira.
Wapendwa wana wa Mungu, kati yetu wapo wanaoshikilia
maumivu (machungu) bila kuyaacha. Badala ya kutoka katika maumivu kwa kusamehe,
wanaendelea kuyakumbuka katika mawazo yao tena na tena. Baadhi ya watu
wanaongozwa na chuki kutunza ndani uchungu wao, na wengine huwalipukia watu
wengine. Hali zote hizi si nzuri na hazisaidii maishani. Chuki mara nyingi
huleta maumivu kwako kuliko yule unayemchukia. Mtu aliyekukosea anaweza kuwa
amesahau lile kosa na anaendelea na maisha yake vizuri, wewe unaendelea kuumia
na kuhangaika na yaliyopita.
Sikiliza ndugu yangu: Wale waliokuumiza wakati
uliopita hawawezi kuendelea kufanya hivyo sasa "isipokuwa" kama
utaendelea kutunza uchungu. Yakiyopita yamepita! Hakuna kitakachoyabadilisha.
Unajiumiza tu na uchungu wako. Kwa ajili yako, jifunze kutokana na hilo na
kisha achana nalo. Maandiko matakatifu yanatuakumbusha kuwa, "kwani hasira
humwua mtu mpumbavu, nao wivu humwua mjinga." Ayu 5:2. Kuwa na hofu kiasi cha kufa kwa sababu ya
uchungu ni upumbavu, ni kitu kipumbavu kukifanya. Ndugu, kwa nini wajifungia
katika tanuru hili? “Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa
Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda
haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake,” 1Yoh 3:10.
3. Watu wengi wanaongozwa na woga.
Ndugu, woga hapa unaweza kutokana na jambo baya sana
lililokupata au lililowapata, matarajio yasiyotekelezeka, kukulia katika jamaa
isiyo na uhuru, au hata maumbile ya asili. Bila kujua sababu, watu wanaongozwa
na woga mara nyingi hupitwa na nafasi kubwa kwa sababu wanaogopa kuchukua
hatua. Badala yake wanajitahidi kuwa salama, wakiepuka hasara na hivyo hujaribu
kulinda hadhi yao. Woga ni kifungo ambacho mtu hujifunga mwenyewe na chaweza
kukuzuia kuwa mtu yule ambaye Mungu anapenda uwe.
Unatakiwa kutoka humo
kwa silaha ya IMANI na UPENDO. "Katika pendo hamna hofu; lakini pendo
lililo kamili huitupa nje hofu, kwa maana hofu ina adhabu, na mwenye hofu
hakukamilishwa katika pendo." 1Yoh 4:18. Kwa maneno mengine, upendo halisi
huiondoa hofu kwa kuwa hofu hulemaza, maisha ya hofu-hofu ya kifo, hofu ya
hukumu- ni maisha ambayo hayajakamilika katika upendo.
4.
Watu wengi wanaongozwa na mali
Ndugu tupo pamoja?
Tamaa yao ya kupata vitu linakuwa ndilo lengo la maisha yao yote. Jambo hili
haijalishi upo utawani au kwenye maisha ya ndoa. Msukumo huu wa kutaka zaidi
kila siku una misingi yake katika udanganyifu wa kuwa nikiwa na vingi nitakuwa
na furaha zaidi, nitakuwa wa muhimu, na nitakuwa salama; lakini mawazo hayo
yote matatu si ya kweli. Mali huleta furaha ya "muda mfupi tu." Na
sababu kubwa ndugu yangu, vitu havibadiliki, hivyo vinatuchosha na tunataka
vipya, vikubwa, na bora zaidi.
Kuna imani pia kwamba
nitapata mali nyingi nitakuwa wa muhimu. Umuhimu wako na mali ni vitu viwili
tofauti. Thamani yako haitegemei mali zako, Mungu anasema kitu cha muhimu
maishani mwako si vitu! Imani ya watu wengi kuhusu fedha ni kwamba kuwa nazo
nyingi kutanipa usalama. Huwezi! Tulio utawani hatuchoki kuwa na tumiradi
binafsi twa siri twingiiii. Usicheke ndiyo ukweli kwa baadhi yetu. Mambo
yanapokwenda vibaya kwenye huto tumiradi tupresha twa kupanda na kushuka
hatukomi. Yesu anawaambia wale wafuasi wa Yohane Mbatizaji, “Mnatafuta nini?”
Wanafunzi wale wakamjibu, Rabi, (maana yake, Mwalimu), unakaa wapi?” Yoh 1:38.
Anapokaa Yesu ndipo kwenye usalama kupita vitu vyote na hali zote tunazoweza
kufikiria. Mt. Augustino anasema, “mioyo yetu haitulii mpaka itakapotulia kwako
Ee Bwana.”
Ndugu yangu, utajiri
unaweza kupotezwa mara moja kwa sababu zisizozuilika. Usalama halisi unaweza
kupatikana katika kile ambacho huwezi kunyang'anywa yaani uhusiano wako na
Mungu. Mt. Augustino anatuwasa kutoka kwenye kanuni yake, "kuna furaha
kubwa kuwa na vichache kuliko kuwa na vingi." Hata hivyo tatizo hapa ni
kipimo cha huo uchache na huo wingi.
5. Watu wengi wanaongozwa na kutaka sifa
Ndugu yangu, wakati mwingine watu hawa wanaruhusu
matarajio ya wazazi, waume, au wake, watoto, waalimu au rafiki zao kutawala
maisha yao. Watu wazima bado wanajaribu kupata sifa kwa wazazi wao ambao
hawajafurahi kamwe. Wengine wanasukumwa na vikundi vya marafiki, wanahofu
wenzao watawafikiriaje. Kwa bahati mbaya, wale wafuatao kundi au maoni ya mtu
binafsi hupotea ndani yake. Ndugu yangu, kwa nini kujifungia katika gereza hili
la fikra na maoni?
Ndugu yangu mpendwa katika Kristo, sijui funguo zote
za mafanikio, lakini ufunguo mmoja wa kushindwa ni kujaribu kumpendeza kila
mtu. Kutawaliwa na maoni ya watu wengine ni njia wazi ya kukosa makusudi ya
Mungu katika maisha yako. Bwana wetu Yesu Kristo anatupa angalizo kwa jambo hili,
"hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu,
na kumpenda huyu, ama atashindana na huyu na kumdharau huyu: hamwezi kumtumikia
Mungu na mali." Mt 6:24.
Kuna nguvu nyingi zinazoweza kuongoza maisha yako
lakini zote mwisho wake ni mfu: kutotumia vipawa ulivyo navyo, mahangaiko ya
moyo, na maisha yasiyo ya utoshelevu.
Ndugu yangu, kuishi maisha yanayoongozwa na malengo,
ni kutawaliwa, na kuelekezwa na makusudi ya Mungu. Hakuna kitu cha muhimu zaidi
kama kujua malengo ya Mungu kwa maisha yako, na hakuna mbadala kwa hilo-siyo
mafanikio, utajiri, kujulikana, au anasa. Bila malengo, maisha ni
mwendo usio na maana, shughuli bila mwelekeo, na matukio bila sababu. Bila
malengo, maisha ni kitu duni, kidogo sana, kisicho na umuhimu wowote.
Wapendwa wana wa Mungu,
usalama wetu upo ndani na katika Kristo. Yesu leo anatuambia, “Njoni, nanyi
mtaona,” Wanafunzi wale wa Yohane Mbatizaji waliunjo amani ya kweli kwa muda
ule waliofuatana na Yesu na kukaa naye jioni ile. “Wakaenda, wakaona akaapo,
wakakaa kwake siku ile. Nayo ilikuwa yapata saa kumi,” Yoh 1:39. Unapogundua
siri hii usiacha mshirikisha na mwenzako furaha hii iliyopo ndani na katika
Kristo kama alivyofanya Andrea kwa ndugu yake Simoni. “Huyo akamwona
kwanza Simoni, ndugu yake mwenyewe, akamwambia, Tumemwona Masihi (maana yake,
Kristo),” Yoh 1:4. Huu ni wajibu wa kila mbatizwa kuwapeleka wale wote wenye
hofu ya Mungu kwa Kristo. Wewe uliyesafiri nami katika tafakari hii una deni
hili kubwa kwa Kristo.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Ikinibidi kujisifu,
nitajisifia mambo ya udhaifu wangu,” 2Kor 11:30
No hay comentarios:
Publicar un comentario