viernes, 29 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 4 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 3 YA MWAKA-C
30/1/2016
Somo: 2Sam 12:1-7a, 10-17
Zab: 59:12-17
Injili: Mk 4:35-41
Nukuu:
Ndipo hasira ya Daudi ikawaka sana juu ya mtu yule; akamwambia Nathani, Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa; naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma,” 2Sam 12:5-6

Basi Nathani akamwambia Daudi, Wewe ndiwe mtu huyo,” 2Sam 12:7 

Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako,” 2Sam 12:10

Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa,” 2Sam 12:12 

Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia?” Mk 4:38 

Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu,” Mk 4:29 

Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado?” Mk 4:40

Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?” Mk 4:41

TAFAKARI: “Wewe ndiye Mtu huyo.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, kunatofauti kubwa kuusema ukweli na kuuishi ukweli. Kuna tofauti kubwa pia ya kuhubiri haki na kutenda haki. Vile vile kunatofauti kubwa sana ya kusema kuhusu upendo na kuishi upendo. Kuyasema mambo kwa ufasaha ni taaluma ambayo mtu anaweza kuipa kwa kupitia njia na miongozo inayohusu jambo hilo. Kuishi jambo fulani ni kugeuzwa na jambo hili na kuwa sehemu ya jambo hilo. Kumbe kwa namna nyingine kama wasemavyo waswahili, ‘kuna kusoma na kuelimika.’ Hivi ni vitu viwili tofauti.

Nabii Nathani anatumwa na Mungu kwenda kwa Mfalme Daudi na kumwambia chukizo alilomfanyia. Nathani anamweleza Daudi uzito wa tatizo na dhambi aliyoifanya kwa jamii, kwa yeye mwenyewe na kwa Mungu. Kwa nafasi aliyokuwa nayo Daudi kama Mfalme ilimpasa awe mtetezi wa kweli, haki, Amani na Upendo. Ufalme wake kama ulivyo uliwakilishwa na taswira na fadhila hizo. Badala yake, Daudi anakuwa muhujumu wa hiyo kweli, haki, Amani, na Upendo. Huu ndio ule mfano wa mtu yule aliyekuwa na kondoo wake mmoja na aliyempenda kupita vitu vyote. Nathani hapa anamaanisha, mtu yule ni Uria, na kondoo wake ni mkewe Bath-sheba Daudi aliyezini naye, na matokeo yake kupelekea umauti wa Uria. Kama Kondoo, yaani wanawake, Daudi alikuwa nao wengi na ofisi yake kama Mfalme iliruhusu kuwa na wake hao wengi.

Mazungumzo ya Nabii Nathani na Mfalme Daudi kwa kupitia mfano wa Mtu na Kondoo wake aliyekuwa anampenda na hivyo kudhulumiwa, yanaamasisha sifa kuu na uwepo wa falme yoyote ile iliyo kwa ajili ya watu, yaani: ufalme wa haki, amani, kweli, na upendo. Hivyo Mfalme Daudi anaguswa na mfano ule na kumwambia Nabii Nathani, “Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa; naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma,” 2Sam 12:5-6. Mfalme Daudi anajiweka kitanzi mwenyewe kwa makosa yake. Ndugu yangu, kumbuka maneno ya Yesu, Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa,” Lk 6:38. Ni kwa mizania hii, Nabii Nathani anamwambia Daudi bila kupepesa macho, Wewe ndiwe mtu huyo,” 2Sam 12:7. Hivyo kosa na adhabu inamstahili yeye mwenyewe.

Mungu anatoa adhabu kwa Mfalme Daudi kwa kosa lile ambayo ni chukizo kwake mwenyewe kama Mfalme na mtetezi wa haki za watu, chukizo na makwazo kwa jamii, na chukizo kwa Mungu aliye haki, kweli, amani, na pendo. Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako,” 2Sam 12:10. Kwa kutambua kosa lake na kulikiri, Mungu anathibitisha kuwa Yeye ni Upendo na Huruma na kumwondolea adhabu ya kifo Mfalme Daudi. Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa,” 2Sam 12:12. Pamoja na hayo, kiumbe kile kama tokeo la uzinifu wa Daudi hakikuishi.

Wapendwa katika Kristo, wewe na mimi kwa njia moja au nyingine tumefanya kama Daudi na wakati mwingine zaidi hata ya Daudi. Hakuna njia nyingine ya kujikwamua katika hali hii zaidi ya kufanya toba ya kweli na majuto. Mungu aliye mwingi wa rehema na upendo yu tayari kutusamehe. Kwa maana Wewe, Bwana, U Mungu wa rehema na neema, Mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli,” Zab 86:15. Amina 

Injili ya leo inatufundisha kwamba tukiamini nguvu na uwepo wa Mungu yote huwa salama. Maisha ni kama chombo cha kusafiri baharini, kuna nyakati husongwa na  dhoruba kali. Chombo chetu cha kusafiri “Mtumbwi”-pale tulipo, iwe maisha ya ndoa, au kitawa huanza kuzama kutokana na dhoruba kali-changamoto nyingi katika maisha. Hata hivyo, katika hali hii Bwana wetu Yesu Kristo si kwamba yupo mbali na dhoruba hizi. Katika sintofahau habarini, wanafunzi wake Yesu walianza kupiga mayowe kwa hofu ya kuzama maji. Yesu alikuwa nao, ila kalala. Wanafunzi wanamlalamikia Yesu wakiwa na tafsiri ya Yesu kutokujali kuagamia kwao. Yesu hana muda wa kujibizana nao zaidi ya kuokoa maisha kwanza. Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu,” Mk 4:29. Ndipo Yesu akawaambia, “Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado?” Mk 4:40.

Mara nyingi tunapopatwa na matatizo na mahangaiko katika maisha tunakosa utulivu na kuhangaika hapa na pale, kuagua kwa mganga moja na mwingine, na kufanya matambiko kwa kila mzimu katika ukoo. Kitu cha kwanza ndugu yangu yakupasa kuutafuta utulivu wa ndani. Utulivu wa ndani tunaupata kwa Kristo mwenyewe kwa kuwa na Imani naye. Yesu anatuambia, “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;  kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:28-30. Je, yupo zaidi ya Yesu? Kwa akili yako tu bila Yesu hutoweza, kwa umashuhuri wako tu bila Yesu hutoweza, kwa utajiri wako tu bila Yesu hutoweza, na kwa nguvu ya madaraka yako tu bila Yesu hutoweza pia. Basi na tuwe na hofu ya Mungu ndani yetu hata kama hatujamjua Yesu. Tuongozwe na dhamiri njema katika utu wema.

Tumsifu Yesu Kristo!


Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema, Umekuwa tayari kusamehe, Na mwingi wa fadhili, Kwa watu wote wakuitao,” Zab 86:5

No hay comentarios:

Publicar un comentario