ALHAMISI BAADA YA EPIFANIA, KIPINDI CHA NOELI
7/1/2016
Somo: 1Yoh 4:19-5:4
Zab: 72:1-2, 14, 15abc, 17
Injili: Lk 4:14-22
Nukuu:
“Sisi twapenda kwa
maana yeye alitupenda sisi kwanza,” 1Yoh 4:19
“Mtu akisema, Nampenda
Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake
ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona,” 1Yoh 4:20
“Katika hili twajua
kwamba twawapenda watoto wa Mungu, tumpendapo Mungu, na kuzishika amri zake.”
1Yoh 5:1
“Kwa maana kila kitu
kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako
ulimwengu, hiyo imani yetu,” 1 Yoh 5:4
“Roho wa Bwana yu juu
yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma
kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha
huru waliosetwa, Na
kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19
“Akaanza kuwaambia,
Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21
“Wakamshuhudia wote,
wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake, wakasema, Huyu siye
mwana wa Yusufu?” Lk 4:22
TAFAKARI: “Mtu akisema, Nampenda
Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo.”
Wapendwa wana wa Mungu, si jambo la ajabu kati yetu kuona
mtu kila siku hakosi katika ibada mbalimbali ikiwa ni pamoja na kushiriki Misa Takatifu
za kila siku. Kwa Mkristo mwenye hofu ya Mungu ni jambo jema kwani amechagua
fungu lililo jema kama Yesu alivyomwambia Martha ndugu yake Mariamu ambaye
alionekana anajishughulisha sana na kazi kama kazi. “Bwana akajibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na
kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini
kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo
hataondolewa,” Lk 10:41-42. Lakini pamoja na uchaji huu ambao unaonekana kwa
watu kama tendo jema, hauendani na namna baadhi yetu tunavyoishi na ndugu zetu
na majirani zetu. Leo kuwa kwako mwanachama wa shirika fulani la kitume, au
chama cha kitume na kushiriki kila siku sala katika chama hicho cha kitume
ilhali hauna uelewano na ndugu yako, wazazi wako au jirani kuna maana gani??? “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake,
ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda
Mungu ambaye hakumwona,” 1Yoh 4:20. Ni Mungu gani huyo unayempenda na
kumwabudu? Ukweli ni kwamba, “Sisi
twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza,” 1Yoh 4:19. Hivyo kama shukrani na kutambua upendo huu wa
Mungu, yanipasa kuwapenda wote wanaonizunguka bila kujali historia zao,
uhusiano uliopo kati yangu na wao,
familia zao, koo zao, kabila zao, jiografia zao, na utaifa wao. Yanipasa
nimpende huyo kwa sababu ana sura na mfano wa Mungu na anaufunua Utukufu wa
Mungu kama mimi nilivyosehemu ya Utukufu huo wa Mungu.
Si jambo la ajabu pia kati
yetu kila siku tunasali sala ya Baba Yetu, Sala ya kutubu, kuzitaja amri za Mungu
kama kasuku, na kushiriki Ekaristi Takatifu ili hali naishi kama kisiwa. Je,
naonja moyoni ninayotamka mdomoni? Kipimo cha upendo kama asemavyo Mt.
Augustino ni kupenda bila kipimo. Hivyo hivyo mizania ya kusamehe ni kusamehe
bila kipimo. Na ndivyo ilivyo katika sala ya Baba yetu, “utusamehe makaso yetu
kama vile tunavyowasamehe wale waliotukosea, Lk 11:4.” Kumbe msamaha wa makosa
yetu ni mizania ya kuwasamehe wale tuliowakosea. Je, ninalitambua jambo hili?
Ni “Katika hili twajua kwamba twawapenda watoto wa Mungu, tumpendapo
Mungu, na kuzishika amri zake.” 1Yoh 5:1. Bila shaka mimi na wewe tumekuwa kama
yule ndege KASUKU aliye maarufu kurudia maneno asiyoyajua.
Wapendwa
wana wa Mungu, katika vita hii ya kuushinda ubinadamu wetu kwa kutenda yale
yampendezayo Mungu yatupasa kuzama zaidi ndani na kuzaliwa upya katika Roho
Mtakatifu kama asemavyo Mtume Paulo. Kuzaliwa
huku si kwa matendo ya mwili, bali kwa rehema ya Mungu. Hii ni nguvu ya ziada
kutoka kwa Mungu mwenyewe. Hivyo, “si kwa sababu ya
matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa
kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu; ambaye alitumwagia kwa wingi, kwa njia ya Yesu Kristo Mwokozi
wetu; ili tukihesabiwa haki kwa neema yake, tupate kufanywa warithi wa
uzima wa milele, kama lilivyo tumaini letu,” Tit 3:5-7. Huu ndio uthibitisho wa
sisi kuzaliwa na Mungu, kwa ajili ya Mungu, na kwa sababu ya Mungu ili
kuushinda ulimwengu kwa imani hiyo. “Kwa maana kila kitu
kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako
ulimwengu, hiyo imani yetu,” 1 Yoh 5:4. Je,
bila kusamehe wathubutu kusema kweli unampenda Mungu?
Yesu Kristo ndiye mfano
hai na hali kwetu wa kuiga na kufuata hata kama kwa hali yetu na ubinadamu wetu
si rahisi. Leo Yesu katika Sinagogi huko Nazareti, wanapomjua vizuri anawaacha
midomo wazi. Ni kweli walimfahamu Yesu katika maana ya historia yake. Mara zote
tunajisikia vizuri na nyumbani pale tunapofikiri sawa, na hata kuishi maisha
yaliyowiyana. Kwa hali hii tunahitaji nguvu ya pekee kuwa tofauti. Yesu
anatufundisha kuwa tofauti na kutokufanya mambo kimazoea. Ukweli na hali ibaki
kama ilivyo. Yesu kama ilivyokuwa kawaida ya siku ya sabato, anaingia kwenye
sinagogi na kulisoma neno la Mungu, “Roho wa Bwana yu juu
yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma
kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha
huru waliosetwa, Na kutangaza
mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Hii ndiyo tofauti ya Yesu na kauli
mbiu yake. Hiki ndicho kinachomtofauti Yesu na wengine ingawa neno hili
lilishasomwa na wengi waliomtangulia. Kwa kukazia Yesu anasema, “Leo maandiko
haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21. Maneno haya ndiyo msukumo wa
mabadiliko yote na mtazamo mpya juu ya Yesu.
Mwana
sayansi Isaac Newton wa Uingereza (1643-1727) alipolichukua jiwa na kulirusha
juu na likarudi ardhini na kugundua nadharia “theory” ya mvutano “gravitation,” hakuwa mwanadamu wa kwanza kurusha
jiwe juu na likarudi ardhini. Ila kwa kwenda zaidi ya mazoea ya urushwaji wa
jiwe na kurudi ardhini ndiko kunakomfanya leo tofauti na wengine
waliomtangulia. Yesu anatualika kutokuishi kwa mazoea, bali tuende zaidi ya
kile kilichozoeleka. Ukweli huu ni kwa hali zote za maisha na kwa namna ya
pekee mahusiano yetu na wenzetu ambayo msingi wake ni Upendo, kweli na haki.
Kwenda tofauti na yaliyozoeleka ni mshangao kwa wale wasiopenda kuwa tofauti
katika kile kilichojificha. Hivyo, “wakamshuhudia (Yesu)
wote, wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake, wakasema, Huyu
siye mwana wa Yusufu?” Lk 4:22. Historia ya
Mtu siyo kikwanzo cha yeye kuwa vizuri, mzuri, au kufanya vizuri zaidi hata
kama historia ya kule alikotoka kuonekana kuwa mbaya.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana; Bali humpenda mtu
afuatiaye wema,” Mit 15:9
No hay comentarios:
Publicar un comentario