domingo, 24 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 2 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 2 YA MWAKA-C
23/1/2016
Somo: 2Sam 1:1-4, 11-12, 19, 23-27
Zab: 80:2-3, 5-7
Injili: Mk 3:20-21
Nukuu:
Daudi akamwambia, Yalikwendaje? Tafadhali uniambie. Akajibu, Watu wamekimbia vitani, tena watu wengi wameanguka wamekufa; hata Sauli naye na Yonathani, mwanawe, wamekufa,” 2Sam 1:4

wakaomboleza, wakalia, wakafunga hata jioni, kwa ajili ya Sauli, na kwa ajili ya Yonathani mwanawe, na kwa ajili ya watu wa Bwana na kwa ajili ya nyumba ya Israeli; kwa sababu wameanguka kwa upanga,” 2Sam 1:12

Nimesikitika kwa ajili yako, Yonathani, ndugu yangu, Ulikuwa ukinipendeza sana; Upendo wako kwangu ulikuwa wa ajabu, Kupita upendo wa wanawake,” 2Sam 1:26

Mkutano wakakusanyika tena, hata wao wenyewe wasiweze hata kula mkate,” Mk 3:20
Jamaa zake walipopata habari wakatoka kwenda kumkamata; maana walisema, Amerukwa na akili,” Mk 3:21 

TAFAKARI: “Usifurahie anguko la mtesi wako, bali mwombee huruma, msamaha, na upendo wa Mungu aliye hai

Wapendwa wana wa Mungu, ulimwengu wa ushindani tunaoishi leo, ni ulimwengu uliopunguza kwa kiasi kukubwa thamani ya mtu na utu wake. Leo tunafurahia sana kukua kwa sayansi na teknologia na hivyo kurahisiha mambo mengi na wakati huo huo kuhathiri utu wa mtu. Katika hali hii ya ushindani ni wazi ‘mwenye nguvu upishwa apite.’ Ni ukweli pia katika hali hii ambapo tunaona utu wa mtu kutokuheshimiwa na wakati mwingine kulinganishwa na kitu, ni wazi kuna anguko kubwa sana la kukua kiroho.

Kukua kiroho ni kufanana na Kristo katika kuona, kufikiri, kuamua na kutenda. Ipo mifano mingi ya namna aonavyo Yesu. Yesu akawaita wanafunzi wake, akasema, Nawahurumia mkutano, kwa kuwa yapata siku tatu wamekaa pamoja nami, wala hawana kitu cha kula, tena kuwaaga wakifunga sipendi, wasije wakazimia njiani,” Mt 15:32. Yesu anaona zaidi ya kile kionekanacho kwa macho ya kawaida. Ni kuona katika kuzama ndani ya fumbo zima ya kile ukionacho kwa macho. Namna hii ya kuona ni hatua ya kufanana na Kristo.

Yesu hufikiri tofauti akilenga lililo zuri na la umilele. Naye anatutaka tufikiri kwa mwelekeo huu, anasema, “Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao? Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii,” Mt 7:9-12. Kumbe kukua kiroho ni kuwafikiria pia wengine na kuwapenda kama unavyojipenda. Ni kutambua unaishi katika jamii, na unawajibu wa kufikiri na jamii husika.

Maamuzi ya Yesu yaliwashangaza wengi na hasa wale ambao walisukumwa na hisia, hasiri, visasi, na hata utekelezaji wa sheria mbovu katika jamii. Yesu mara zote anakutaka utoapo hukumu uende mbali ya kile kinachokuruhusu kufanya au kutekeleza hukumu hiyo. Tazama jinsi Yesu anavyotoa hukumu juu ya mwanamke yule aliyeletwa kwake kwa kosa la uzizi. Nao walipozidi kumhoji, alijiinua, akawaambia, Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe. Akainama tena, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao waliposikia, wakashitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia tangu wazee hata wa mwisho wao; akabaki Yesu peke yake, na yule mwanamke amesimama katikati,” Yoh 8:7-9. Kumbe kukua kiroho ni kujiweka katika hali ya mtuhumiwa kabla ya kutoa hukumu husika. Lengo ni kumpata mwovu kuliko kumpoteza.

Kutenda kwa Yesu kulishangaza wengi na hasa wanafunzi wake. Kutenda kwa Yesu ni kwa kutumika kuliko kutumikiwa. “aliondoka chakulani; akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga. Basi alipokwisha kuwatawadha miguu, na kuyatwaa mavazi yake, na kuketi tena, akawaambia, Je! Mmeelewa na hayo niliyowatendea? Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo. Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi,” Yoh 13:4-5, 12-14. Kumbe kufanana na Kristo ni kutenda kama alivyotenda.

Wapendwa katika Kristo, namna hii ya kukua kiroho, yaani, kufanana na Kristo Yesu katika kuona, kufikiri, kuamua, na kutenda ndicho tunachotakiwa tuwe kama kweli sisi ni wafuasi wake Kristo. Maisha yako yakiongozwa na mfanano huu wa Kristo wa kuishi ndani na katika Kristo, kamwe hutofurahia anguko la mtesi wako, bali utamwombea huruma, msamaha, na upendo wa Mungu aliye hai. Ni Mungu tu aliye muumba mtesi wako kwa sura na mfano wake ndiye mwenye uwezi wa kumbadili na kuwa mwema.

Daudi mwenye hofu ya Mungu, hakufurahia kuanguka kwa Sauli licha ya kwamba Sauli aliiwinda sana roho yake mchana na usiku. Badala yake, Daudi alipopata habari za kifo cha Sauli, wakaomboleza, wakalia, wakafunga hata jioni, kwa ajili ya Sauli, na kwa ajili ya Yonathani mwanawe, na kwa ajili ya watu wa Bwana na kwa ajili ya nyumba ya Israeli; kwa sababu wameanguka kwa upanga,” 2Sam 1:12. Ndugu yangu tuliyesafiri pamoja katika tafakari hii, tujifunze kutoka kwa Daudi, na hasa kufanana na Kristo Yesu katika ili tukue kiroho. Amina

Tumsifu Yesu Kristu


Maana hukumu haina huruma kwake yeye asiyeona huruma. Huruma hujitukuza juu ya hukumu,” Yak 2:13

No hay comentarios:

Publicar un comentario