sábado, 30 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 4 YA MWAKA-C

JUMAPILI WIKI YA 4 YA MWAKA-C

Somo I: Yer 1:4-5, 17-19
Zab: 71:1-6, 15-17
Somo II: 1Kor 12:31-13:13
Injili: Lk 4:21-30
Nukuu:
Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao,” 1Kor 13:1

Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi,” 1Kor 13:2

Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu,” 1Kor 13:3 

Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni,” 1Kor 13:4 

haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya,” 1Kor 13:5

haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli,” 1Kor 13:6 

huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote,” 1Kor 13:7

Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika,” 1Kor 13:8 

Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo,” 1Kor 13:13

Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21

Akawaambia, Hapana shaka mtaniambia mithali hii, Tabibu, jiponye nafsi yako; mambo yote tuliyosikia kwamba yametendeka Kapernaumu, yatende na hapa pia katika nchi yako mwenyewe,” Lk 4:23 

Akasema, Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24 

Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo,” Lk 4:28

Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini,” Lk 4:29 

lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake,” Lk 4:30 

Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa,” Yer 1:5

Maana, tazama, nimekufanya leo kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote; juu ya wafalme wa Yuda, na juu ya wakuu wake, na juu ya makuhani wake, na juu ya watu wa nchi hii,” Yer 1:18

Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema Bwana, ili nikuokoe,” Yer 1:19

TAFAKARI: Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo,”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 4 ya mwaka ‘C’ wa Kanisa. Leo kwa namna ya pekee Mama Kanisa anatutaka tuzame ndani zaidi katika fumbo hili la UPENDO. Uwepo wetu na yote yaliyopo katika ulimwengu huu ni tokeo la Upendo wa Mungu Baba. Mungu alivijua vitu vyote hata kabla ya kuumbwa kwayo, na ndivyo ilivyokuwa kwa mwanadamu. Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa,” Yer 1:5. Wito huu wa Nabii Yeremia unatukumbusha kwamba hakuna aliyeko duniani hapa kwa bahati mbaya. Kila mmoja wetu ni kusudi la Mungu, kwa sababu ya Mungu, na kwa ajili ya Mungu. Mungu aliviumba vitu vyote kwa sababu alipenda kuviumba na kuvifanya kama vilivyo kwa sifa na utukufu wake. Pamoja na uzuri huu, binadamu amependelewa zaidi kwa sababu ndiye aliyechukua chapa halisi ya Mungu. Mungu alichagua kumuumba mtu kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27.

Hivyo asili ya Upendo ni Mungu, uwepo wa upendo ni Mungu, na Upendo ni Mungu. Upendo wa Mungu Baba kwetu ni Upendo wa Mwana pia kwetu. Kwa sababu,Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:1-3. Huu wote ni upendo wa kweli wa Mungu Baba kwetu, na kupitia Mwana ambaye alifanyika mwili akakaa kwetu, Yoh 1:14. Hivyo upendo huu asili yake ni Mungu mwenyewe kama asemavyo Yesu, Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Yoh 15:16. Mungu ndiye aliyetupenda kwanza. Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. Sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza,” 1Yoh 4:9-10, 19. Ni kwa namna hiyo tunajifunza haya kama sababu ya kuumbwa kwetu.

Tumeumbwa ili tumjue Mungu, tumpende Mungu, tumtumikie Mungu, na mwisho turudi kwake mbinguni. Hivyo ishi ya binadamu hapa duniani na ustawi wake wampasa kuustawisha upendo huo wa Mungu kwake mwenyewe, jirani, mazingira yanayomzunguka, na Mungu. Upendo na ambatio lake, yaani, ‘jukumu’ hili la msingi lisipoonekana kwa mwanadamu basi mwanadamu huyo kesha potea njia, na ishi yake haina makusudi ya kuumbwa kwake.

Yesu anaanza safari yake ya kukamilisha kile alichokijia kwa maneno haya, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Huu ndiyo mpango kazi wa Yesu ambao unasukumwa na UPENDO. Mpango kazi huenda pia na kauli mbiu ya kazi. Kauli mbiu ya Yesu juu ya wokovu wetu ndiyo hii, “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili,” Mk 1:15. Upendo na huruma ya Mungu huenda pamoja.

Upendo huu wa Mungu kupitia mwanaye Mpenzi Yesu Kristo unafungua mlango mpya wa huruma ya Mungu, yaani, ‘mwaka wa Bwana uliokubaliwa.’ Hivyo tuutumie vyema mwaka huu wa Kanisa wa huruma ya Mungu kwa kuchota baraka na neema za Mungu. Leo Yesu anatuambia, “maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21. Maandiko haya yametimia kwetu kwa sababu nguvu na uwezo vina yeye (Kristo) hata milele yote, Yud 1:25. Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile,” Yoh 5:19.

Ni wazi katika kutenda lililo la Mungu, yaani lenye kuongozwa na upendo wa kweli, tujiandae kupata upinzani. Yule mwovu shetani hafurahii yaliyo mazuri na mema yenye kuufunua Utukufu wa Mungu. Yesu Kristo mwenyewe alipata upinzani nyumbani mwake mwenyewe. Katika hili Yesu anasema, Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24. Je, kama hatukubaliki nyumbani kwetu na watu wanaotufahamu iwe sababu ya kutokutenda mema? Jibu ni HAPANA! Tuendelee kutenda wema na upendo kwa wote, kwa sababu asili ya upendo ni Mungu, uwepo wa upendo ni Mungu, na Upendo ni Mungu.

Mtume Paulo anaeleza kwa undani upendo na mapaswa yake na yenye kutupeleka katika kusudi la uumbaji wetu. Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao,” 1Kor 13:1. Vipaji vyetu na karama zetu za pekee tulizopewa na Mungu, kama hazitakuwa kwa ajili ya wengine na furaha ya Mungu na jirani zetu, ni hasara kwetu. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi,” 1Kor 13:2. Wengine wamepewa unabii si kwa ajili yao binafsi au kujineemesha, bali umepewa unabii ili upeleke ujumbe huo wa Mungu kwa faida ya watu na wokovu wao na wewe mwenyewe.

Ndugu yangu, hata huo utajiri Mungu aliokupa si kwa ajili yako mwenyewe na kujiburudisha nafsi yako, bali kwa ajili ya kufaidiana na hasa kuwajali kwa njia ya pekee wale wahitaji wasio na chochote. Ni jambo la kusikitisha kuona jirani yako kila siku anaomba Mungu amkirimie angalau apate mlo mmoja kwa siku, wewe unayejua shida na dhiki ya jirani yako huyo ukiwa unasali na kuomba kila siku Mungu akupe maisha marefu ili uendelea kuvitumbua vinono katika utajiri wako. Ndugu yangu, swala hapa si tu kuona hitaji la jirani yako muhitaji, bali kutambua upendo wa Mungu na paswa lake kama Paulo Mtume anavyosema, Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu,” 1Kor 13:3. Ukweli ni kwamba unaweza kutoa bila kupenda, ila huwezi kupenda bila kutoa.

Maisha ya upendo wa kweli yana tabia zifuatazo kama anavyotufundisha Mtume Paulo. Sehemu ya kwanza ya tabia ya upendo ni hii, kwamba, Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni,” 1Kor 13:4. Kwa maneno mengine ‘upendo haujifaidishi wenyewe. Upendo wa kweli hutoka na kutafuta zaidi ya pale ulipo.’ Upendo huwa kwa ajili ya kingine zaidi ya kile kilicho katika ukamilifu wake. Sehemu ya pili ya tabia ya upendo ni kwamba, upendo haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya,” 1Kor 13:5. Kwa maneno mengine upendo ulenga katika ukamilifu bila kupoteza hata kile kilicho katika hali ya udhaifu. Sehemu ya tatu ya tabia ya upendo ni kwamba, upendo haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli,” 1Kor 13:6. Upendo huu ulenga faida ya wote katika wote. Sote tu wana wa Mungu, wenye mahitaji yaliyo sawa licha ya tofauti zetu.

Sehemu ya nne ya tabia ya upendo ni kwamba, upendo huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote,” 1Kor 13:7. Mwenye upendo wa kweli hana sababu ya kuishi na mashaka pasipo sababu. Upendo huu utusaidia kukua mwili na roho. Upendo huu upo kwa ajili ya kurekebishana katika kukua na kuongezeka pasipo kuangamizana. Upendo huu unatoa fursa ya kuvumiliana katika kujengana na  kujuana tabia. Upendo huu hutoa fursa bila kipimo katika kusamehana. Sehemu ya tano ya tabia ya upendo ni kwamba, Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika,” 1Kor 13:8. Upendo huu unatoa fursa ya mazungumzano hata pale ambapo hakuna uwezekano kinadharia wa mazungumzano hayo ambayo hayazungumziki. Kwenye tabia hii ya upendo hakuna lisilowezekana.

Tabia hizo tano za upendo hutuandaa kujibu maswali mawili la mwisho na ya pekee mbele ya Mungu katika kitu chake cha hukumu na haki. Pasipo shaka yoyote ile, ninashawishika kuona kwamba kila mmoja wetu kadiri ya wito na nafasi yake ataulizwa maswali haya na Mungu;
 Swali la kwanza: Je, ulifanya nini na Upendo wa Mwanangu Yesu Kristo aliyekupenda hadi akayatoa maisha yake kwa ajili yako?
Swali la pili: Je, umefanya nini na vipaji nilivyokupa?

Leo tuwapo hapa duniani tunaongozwa na mambo yote matatu, yaani, Imani kwa kile tusichokijua sawasawa ila kina uzima ndani yake, pili, Matumaini tukijua yote yatapita na uzuri wake na mwisho tutapata kile tunachokichuchumili yaani maisha ya umilele. Na tatu, twaishi ulimwenguni hapa kwa mapendo na hasa tukielekeza nguvu zetu katika tabia za upendo. Haya mawili, yaani Imani na Matumaini ukomo wake ni pale tutakapo ifikia Mbingu. Upendo na tabia zake zitadumu katika umilele wote kwa sababu UPENDO NI MUNGU. Hivyo, Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo,” 1Kor 13:13.

Mzee Mapinduzi alikuwa mlinzi nyumbani kwa tajiri Mwana Mboka. Mzee Mapinduzi kila siku ufikapo muda wa kwenda lindoni kwa tajiri yake huchukua kindoo kidogo kwa ajili ya kubebea mabaki ya chakula na hasa mifupa ya nyama ambayo kwa kiasi kikubwa hubaki.

Mzee Mapinduzi alifanya hivi kwa zaidi ya miaka mitano. Siku moja Tajiri yake alimuuliza Mzee Mapinduzi, “hivi kwa sasa una mbwa wangani?” “Bosi idadi ya mbwa wangu ni ileile,” Mzee Mapinduzi alimjibu tajiri yake kwa hali ya uzuni. Muonekano ule wa Mzee Mapinduzi ulimfanya tajiri yake afikiri zaidi.

Kesho yake asubuhi na mapema Bwana Mboka kama ilivyo kawaida yake alidamka kwa ajili ya kufanya mazoezi ya kukimbia. Ila siku ile alidhamiria kuondoka mguu kwa mguu na Mzee Mapinduzi kuwatazama mbwa wake. Walipo karibia nyumbani, mjukuu wa Mzee Mpinduzi alyejulikana kwa jina kama Tatu, alikuja mbio na kumpokea Babu yake kile kindoo cha mifupa na mabaki ya chakula.

Mtoto huyu alienda na kindoo kile moja kwa moja jikoni. Bwana Mboka alipotazama huku na kule hakuona dalili yoyote ya Mbwa. Hivyo alimuuliza Mzee Mapinduzi, “wale mbwa unaowaletea mifupa wapo  wapi?” Mzee Mapinduzi alimwita mke wake na wajukuu wake watano nje. “Hawa ndiyo mbwa wangu. Huyu ni mke wangu mpendwa Bibi Zaituna, na wajukuu wangu watano ambao tunawalea tangu wazazi wao wafariki kwa ugonjwa wa ukimwi.” Mzee Mapinduzi alimjibu tajiri yake huku machozi yakimtoka.

Bwana Mboka aliondoka taratibu kurudi nyumbani bila kusema neno. Siku ile ilikuwa nzito sana kwa Bwana Mboka. Jioni ilipofika, Mzee Mapinduzi alifika lindoni kama kawaida yake na kindoo chake. Bwana Mboka alimwita Mzee Mapinduzi na kumwambia, “hali niliyoiona leo asubuhi imenisikitisha sana. Mimi na familia yangu tumeamua haya yafuatayo: kukujengea nyumba nzuri ya kuishi, kuwasomesha wajuu zako, na kukutunza kama mzazi wetu wewe na familia yako.” Wote walikumbatiana kwa furaha na uchungu huku machozi yakiwatoka.

Tumsifu Yesu Kristo! 


Heri amkumbukaye mnyonge; Bwana atamwokoa siku ya taabu. Bwana atamlinda na kumhifadhi hai, Naye atafanikiwa katika nchi; Wala usimtie katika hali wamtakiayo adui zake,” Zab 41:1-2

No hay comentarios:

Publicar un comentario