miércoles, 20 de enero de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 2 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 2 YA MWAKA-C
21/1/2016
Somo: 1Sam 18:6-9; 19:1-7
Zab: 56:2-3, 9-10a, 10a-11, 12-13
Injili: Mk 3:7-12
Nukuu:
Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme?” 1Sam 18:8

Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile,” 1Sam 18:9 

Kisha Sauli akasema na mwanawe Yonathani, tena na watumishi wake wote, kwamba wamwue Daudi,” 1Sam 19:1

Lakini huyo Yonathani, mwana wake Sauli, alikuwa akipendezwa sana na Daudi. Basi Yonathani akamwambia Daudi, akasema, Sauli, baba yangu, anatafuta kukuua; basi, nakusihi, ujiangalie sana asubuhi, ukae mahali pa siri na kujificha,” 1Sam 19:2

Na pepo wachafu, kila walipomwona, walianguka mbele yake, wakalia wakisema, Wewe ndiwe Mwana wa Mungu,” Mk 3:11 

Akawakataza sana, wasimdhihirishe,” Mk 3:12

TAFAKARI: “Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile.”

Wapendwa wana wa Mungu, wivu ni mbaya sana unapomtia mtu upofu wa kutokuyaona mazuri ya mwenzake na kuyatafsiri kama kikwazo katika maisha yako. Wapo wengi kati yetu wametendwa vibaya sana kwa sababu tu wametenda yaliyo mema na yakawa na mwitikio chanya kwa watu. Chanzo kikubwa cha wivu kadiri ya mang’amuzi yangu ni kutokutambua karama zako. Kila mmoja wetu angetambua karama zake kusingekuwa na nafasi ya kuoneana wivu. Tatizo kubwa ni kwamba tunapoteza muda mwingi kutaka kufanana na wengine na wakati mwingine kuiga kusiko kujifunza.

Uungwana ni pale unapoona mazuri ya mwenzako na kusadifu kama yalivyo. Sauli Mfalme anaingiwa na hofu kwa wasifu aliopewa Daudi baada ya kumuua Goliathi. Goliathi Mfilisti alikuwa tishio kubwa kwa taifa zima la wana wa Israeli. Ushindi wa Daudi ulipaswa kuwa furaha kwa wote na hasa Mfalme ambaye kwa sasa ufalme wake amani imerejeshwa. Sauli anatafsi wasifu aliopewa Daudi kama tishio kwa nafasi yake kama mfalme. Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme?” 1Sam 18:8. Hivi kwa nini unakosa usingizi kwa vile tu mwenzako kafanya vizuri tena kwa manufaa ya wote?

Wivu unaegemeao upande hasi matokea yake ni umauti. Wivu kama ulivyo ni amsho la ndani la moyo wa mtu juu ya kitu fulani. Wivu kama wivu si tatizo. Tatizo linakuja kwenye egemeo la wivu huo, yaani egemeo hasi au chanya. Egemeo chanya la wivu linamsukuma mtu kufanya vizuri zaidi ya kile kilichofanywa na mtangulizi wake. Aliyoyafanya mtangulizi wake yanakuwa msingi na dira ya yeye kuboresha na kufanya vizuri zaidi. Hapa ndipo tunapoongelea wivu wa maendeleo. Mfano: kama mwenzako kajenge nyumba nzuri na kuweka bati za rangi nzuri na imara, wewe ukijenga nyumba yako weka vigae vizuri na imara. Huu ni wivu wa maendeleo. Egemeo hasi la wivu ni pale ambapo mtu anatumia akili zake, moyo wake, nguvu zake na mbinu zake zote  kuyadhoofisha mazuri ya mwenzake. Hiki ndicho anachojaribu kukifanya Mfalme Sauli. Kisha Sauli akasema na mwanawe Yonathani, tena na watumishi wake wote, kwamba wamwue Daudi,” 1Sam 19:1. Maamuzi haya ni sawa na wale wasemao “wote tukose!”

Mtoto wa Sauli, Yonathani, hakubaliani na wazo la Baba yake, hivyo anakuwa mtetezi wa siri ya Daudi. Ndugu zangu tuelewe ukweli huu; chochote kile ufanyacho kiwe kizuri au kibaya, watu huona palipo kweli na pasipo kweli. Hivyo kweli hubaki kuwa kweli na uongo hujitenga. Ni kwa mantiki hii tunaona Yonathani, mwana wake Sauli, alikuwa akipendezwa sana na Daudi. Basi Yonathani akamwambia Daudi, akasema, Sauli, baba yangu, anatafuta kukuua; basi, nakusihi, ujiangalie sana asubuhi, ukae mahali pa siri na kujificha,” 1Sam 19:2. Tofauti katika utendaji zipo na hatuwezi kuzizuia kwa sababu kila mmoja wetu ni tofauti na wapekee. Tunachotakiwa kufanya ni kuruhusu ndani ya mioyo yetu na katika utendaji wetu, umoja katika utofauti. Mfumo huu unatija sana katika maendeleo ya mwanadamu na watu wanaomzunguka. Vipaji hukuzwa, na jamii hufaidika navyo.

Wasifu aliopewa Daudi na wanawake wale walioyaona makuu ya Mungu kupitia kifo kile cha Goliathi, “Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake,” mapepo pia wanaona utofauti uliopo kwa Yesu kwa kile alicho na huduma ile aitoayo. Na pepo wachafu, kila walipomwona, walianguka mbele yake, wakalia wakisema, Wewe ndiwe Mwana wa Mungu,” Mk 3:1. Jambo la ajabu Yesu hayasadifu wala kuyashabikia haya yasemayo na mapepo. Kumbe tunakumbushwa kuwa makini hasa na vyanzo vya wasifu tupewao. Yesu Akawakataza sana (mapepo), wasimdhihirishe,” Mk 3:12. Ndugu yangu, kila kishindo kina maana yake. Mara uyapatapo hayo katika utume wako chukua nafasi ya pekee kuyatafakari kwa kina.

Tumsifu Yesu Kristo


Kwani hasira humwua mtu mpumbavu, Nao wivu humwua mjinga,” Ayu 5:2

No hay comentarios:

Publicar un comentario