viernes, 15 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI YA 1 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 1 YA MWAKA-C
16/1/2016
Somo: 1Sam 9:1-4, 17-19; 10:1
Zab: 21:2-3, 4-5, 6-7
Injili: Mk 2:13-17
Nukuu:
Basi, kulikuwa na mtu mmoja wa Benyamini, jina lake akiitwa Kishi, mwana wa Abieli, mwana wa Serori, mwana wa Bekorathi, mwana wa Afia, mwana wa Mbenyamini, mtu shujaa, mwenye nguvu,” 1 Sam 9:1 

Naye alikuwa na mwana, aliyeitwa jina lake Sauli, kijana, tena mzuri; wala katika wana wa Israeli hakuwako mtu mzuri kuliko yeye; tangu mabega yake kwenda juu alikuwa mrefu kuliko watu wote,” 1 Sam 9:2 

Hata Samweli alipomwona Sauli, Bwana akamwambia, Huyu ndiye niliyekuambia habari zake; huyu ndiye atakayewamiliki watu wangu,” 1Sam 9:17 

Ndipo Samweli akatwaa kichupa cha mafuta, akayamimina kichwani pake, akambusu, akasema, Je! Bwana hakukutia mafuta [uwe mkuu juu ya watu wake Israeli? Nawe utamiliki watu wa Bwana, na kuwaokoa na mikono ya adui zao; kisha hii itakuwa ishara kwako ya kuwa Bwana amekutia mafuta] uwe mkuu juu ya urithi wake,” 1Sam 10:1

Hata alipokuwa akipita, akamwona Lawi wa Alfayo, ameketi forodhani, akamwambia, Nifuate. Akaondoka akamfuata,” Mk 2:14

Hata alipokuwa ameketi chakulani nyumbani mwake, watoza ushuru wengi na wenye dhambi waliketi pamoja na Yesu na wanafunzi wake; kwa maana walikuwa wengi wakimfuata,” Mk 2:15

Na waandishi na Mafarisayo walipomwona anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi, waliwaambia wanafunzi wake, Mbona anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi?” Mk 2:16 

Yesu aliposikia aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi; sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mk 2:17

TAFAKARI:Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.”

Wapendwa wana wa Mungu, utabiri wa malaika juu ya kuzaliwa kwa Yesu, uliweka wazi juu ya kile anachokijia Yesu katika ulimwengu huu. Malaika Gabriel anamtoa hofu Yusufu mume wa Bikira Maria juu ya mimba ile kwani Yusufu alikuwa mtu wa haki na hakupenda makuu. Hivyo njia ya pekee ni kumwacha kimya kimya mkewe. Malaika akamwambia Yusufu, “Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao,” Mt 1:20-21. Hivyo Yesu anathihirisha ukweli huu katika Injili ya leo wakati Mafarisayo wanapowashambulia wanafunzi wa wake kuona Yesu anakula na watoza ushuru na wenye dhambi. Yesu aliposikia aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi; sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mk 2:17. Kristo amekuja na yupo muda wate kutupatanisha na Mungu Baba. Kristo kwetu leo ni daraja imara kuelekea uzima wa milele.

Hakuna hata mmoja kati yetu asiyehitaji huruma, msamaha, na upendo wa Mungu. Hata kama twajiona wenye haki na wasio na hatia, bado tunaitaji upendo wa Mungu. Pendo lake Yesu utuvutia tuwe wake milele. Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe ndani yao,” Yoh 17:26. Hivyo uwe una afya ya mwili na roho, au hauna afya hiyo bado wahitaji pendo la Mungu.

Basi wapendwa wana wa Mungu, tusipoteze muda mwingi kuzichunguza dhambi za watu kama walivyopoteza muda huo Mafarisayo na kusahau wongofu wao wenyewe. Yesu anasema hili juu ya yeyote yule mwenye kupoteza muda wake kwa kuzitazama dhambi za mwenzake bila kuhangaikia wongofu wake mwenyewe. Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako,” Mt 7:5. Ninapogundua mwenzangu kaanguka katika dhambi tendo lile liwe kioo cha kujitazama kwanza ndani ya nafsi yangu kabla ya kuhukumu. Tendo hilo liwe kielelezo cha mimi kuiona huruma ya Mungu ndani yangu na kwa yule aliyedondoka katika dhambi. Na mara zote nionapo tendo hilo nijiulize hivi; “ya mwenzangu yamejulikana, yangu yamesitiriwa kwa muda tu, yanipasa kutubu.”

Tusipoona na kuonja huruma ya Mungu ndani ya nafsi zetu na kwa wenzetu, hatuwezi kukua kiroho. Nisipoonja hali hii ndani yangu, ukristo wangu na huduma niitoayo haina maana yoyote  zaidi ya uigizaji tu. Huruma na upendo wa Mungu wajidhihirisha pia katika somo letu la kwanza juu ya Sauli Mfalme mteule. Pamoja na yote mabaya yaliyofunuliwa juu yake, bado Mungu anaruhusu awe Mfalme na kuitenda kazi yake. Ndipo Samweli akatwaa kichupa cha mafuta, akayamimina kichwani pake, akambusu, akasema, Je! Bwana hakukutia mafuta [uwe mkuu juu ya watu wake Israeli? Nawe utamiliki watu wa Bwana, na kuwaokoa na mikono ya adui zao; kisha hii itakuwa ishara kwako ya kuwa Bwana amekutia mafuta] uwe mkuu juu ya urithi wake,” 1Sam 10:1. Je, waweza mkabidi mtoto wako simba mwenye njaa? Mungu hufanya bila shaka yoyote.

Tumsifu Yesu Kristo.


Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema,” Zab 145:8

No hay comentarios:

Publicar un comentario