SIKUKUU YA KUTOLEWA BWANA HEKALUNI
Siku ya Maisha ya Wakfu-Maisha ya Kitawa
2/2/
Somo I: Mal 3:1-4
Zab: 24:7-9
Somo II: Ebr 2:14-18
Injili: Lk 2:22-40
Nukuu:
“Angalieni,
namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana
mnayemtafuta atalijilia hekalu lake ghafula; naam, yule mjumbe wa agano
mnayemfurahia, angalieni, anakuja, asema Bwana wa majeshi,” Mal 3:1
“Wakati
ule ndipo dhabihu za Yuda na Yerusalemu zitakapopendeza mbele za Bwana, kama
katika siku za kale, na kama katika miaka ya zamani,” Mal 3:4
“awaache
huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali
ya utumwa,” Ebr 2:15
“Hivyo
ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu
mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za
watu wake,” Ebr 2:17
“Kisha,
zilipotimia siku za kutakasika kwao, kama ilivyo torati ya Musa walikwenda naye
hata Yerusalemu, wamweke kwa Bwana, (kama
ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba
ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa Bwana),” Lk
2:22-23
“wakatoe
na sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya Bwana, Hua wawili au makinda ya
njiwa wawili,” Lk 2:24
“Sasa,
Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu
wako,” Lk 2:29-30
“Simeoni
akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka
na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa,” Lk 2:34
“Yule
mtoto akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu
yake,” Lk 2:40
TAFAKARI:
“Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa
Bwana.”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Kutolewa Bwana Hekaluni.
Yesu
anapotolewa hekaluni kama ilivyo desturi ya Wayahudi kwa kila mzaliwa wa kwanza
wa kiume. “Kisha, zilipotimia siku za kutakasika kwao, kama
ilivyo torati ya Musa walikwenda naye hata Yerusalemu, wamweke kwa Bwana, (kama ilivyoandikwa katika sheria ya
Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu
kwa Bwana),” Lk 2:22-23. Hata
hivyo, kumkomboa huyu mzaliwa wa kwanza kutoka hekaluni iliwapasa wazazi wake
kumtolea Bwana sadaka kama shukrani. “Wakatoe
na sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya Bwana, Hua wawili au makinda ya
njiwa wawili,” Lk 2:24. Sadaka hii inaonyesha umasikini wa Familia hii Takatifu
ya Yesu, Maria na Yosefu.
Ni
katika tendo hili pale Hekaluni, Simeoni mtu wa kweli na haki ahadi yake
inatimizwa na Mungu. “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake
Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na
Roho Mtakatifu alikuwa juu yake,” Lk 2:25.
Yesu Kristo hapa ndiye nuru halisi na uhuru wa kweli wa wana wa Taifa la Mungu.
Kristo ndiye ile nuru aliyokuwa
ikisubiriwa, “Nuru ya kuwa mwangaza
wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli,” Lk 2:32. Mungu anaifunua nuru ya Yesu ndani ya moyo wa
Simeoni naye anayaona makuu ndani ya Yesu: “Simeoni
akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka
na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa,” Lk 2:34.
Kristo ndiye sababu ya kuanguka na kuinuka wengi, kwa sababu ulimwenguni hapa
ni vita dhidi ya mwanga ambaye ndiye Kristo, na giza ambayo ndiye yule mwovu
shetani. Watainuliwa wale watakaoambatana na mwanga na wataangushwa wale
waambatanao na giza, yaani yule mwovu.
Katika
vita hii Mama Bikira Maria hatakuwa salama katika maana ya kufurahia tu uwepo
wa mwanaye. Ni katika uchungu na kushiriki mateso ya mwanaye nuru ya kweli na
haki itafunuliwa ndani yake. Hivyo ni katika msalaba ambao mwanaye anauendea
ndipo utakapokuwepo utukufu wake. “Nawe
mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi,”
Lk 2:35. Kwenye Msalaba Mtakatifu na wenye ushindi wa Bwana Yetu Yesu Kristo
ndipo penye utukufu, kufunguliwa kwa mioyo yetu kutoka utumwa wa dhambi, na
kuuelekea uzima wa milele. Hivyo kwa Mkristo na Mfuasi wa Kristo, hakuna
UTUKUFU pasipo MSALABA.
Kuyafanya
mapenzi ya Mungu wakati mwingine hakuhakisi kabisa miono na mitazamo ya
kibinadamu. Mitazamo yetu ni kwamba tuwapo karibu sana na Mungu na kufanya
mapenzi yake, ndiyo miminiko ya baraka na neema. Ndugu yangu uliyesafiri nami
katika tafakari hii, hatutendi mema wala kuwa waaminifu mbele ya Mungu ili
tununue baraka na neema zake, bali tunayafanya hayo yote kwa sababu ndiyo hali
na uwepo wa Mungu, na ndivyo impendezavyo sisi kufanya. Uwepo wetu hapa duniani
ni moja ya uzuri na utukufu wa Mungu. Mfano wa wale waliyafanya yote vyema ila
hayakuendana na miono na mitazamo ya kibinadamu ni Ana binti Fanueli.
Tunaambiwa “Palikuwa na nabii mke, jina lake Ana, binti Fanueli, wa
kabila ya Asheri, na umri wake ulikuwa miaka mingi, alikuwa amekaa na mume
miaka saba baada ya uanawali wake,” Lk 2:36. Bila shaka Ana kama Mwanamke na
Mama, kuwa na familia kamili katika maana ya Yeye, Mumewe na mtoto au watoto
ilikuwa moja ya furaha yake kubwa hapa
duniani. Pamoja na kukosa hilo, hakuwa na nafasi ya kumlaumu Mungu wala kuasi
Imani yake. Aliishi kwa matumaini makubwa ingawa umri wake ulisogea. “Naye ni mjane wa miaka themanini na minne;
haondoki katika hekalu, ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba,” Lk
2:37. Wangapi kati yetu tunaujasiri huu tunapoona mbele yetu ni giza tupu?
Furaha
ya Ana binti Fanueli inakamilika anapokutana na Yesu. Ni kama asemavyo Mt.
Agustino kwamba ‘mioyo yetu haitulii mpaka itakapotulia kwako Ee Bwana.’ Ndivyo
ilivyokuwa kwa Ana binti Fanueli alipokutana na Yesu. “Huyu (Ana binti Fanueli)
alitokea saa ile ile akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi
katika Yerusalemu akawatolea habari zake,” Lk 2:38. Alichokua akikitazamia amekiona kwa macho yake.
Na “Yule mtoto (Yesu) akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima,
na neema ya Mungu ilikuwa juu yake,” Lk 2:40. Maana yake aliyaishi maisha yetu,
furaha zetu, mahangaiko yetu, na kuyashiriki yote bila kutenda dhambi hadi
kikomo chake pale Msalabani kwa kutuweka huru. Hivyo “Nanyi
mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu;
mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa
damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya
Kristo,” 1Pet 1:18-19. Je, una chochote chenye thamani katika ulimwengu huu ambacho waweza kulinganisha
na wokovu aliyokupatia Kristo Yesu? Je, tendo hili la Bwana kutolewa hekaluni
na yale yote yaliyojiri kule hekaluni yanasema nini katika siku yetu hii ya
Watawa duniani?
Wapendwa katika Kristo,
Maisha ya Kitawa hayana tofauti na tendo hili la Bwana kutolewa hekalu na kile
wafanyacho watawa wanapojiweka wakfu kwa Mungu. Kujiweka Wakfu ni kujitenga kwa
kazi MAALUMU kwa ajili ya Kristo, kwa sababu ya Kristo, na Kwa Kristo. Huku
ndiko KUJISALIMISHA kwa MTAWA na KUABUDU kuliko na AMANI, FURAHA, na NGUVU. Ndugu
yangu, kujitoa kwa Mungu ndiyo kuabudu hasa. Tendo hili la kujisalimisha
binafsi huitwa kwa majina mengine; Kujiweka wakfu, Kumfanye Yesu Bwana wako,
Kuchukuwa msalaba wako, Kuifisha nafsi, na Kujitoa kwa Roho Mtakatifu. Cha
muhimu hapa ni kwamba ulitende, siyo linaitwaje. Mungu anapenda maisha yako
yote. Asilimia tisini na tano haitoshi. Ndugu, kuna vizuizi vitatu ambavyo
huzuia kujisalimisha kwetu kikamilifu kwa Mungu; Hatuelewi kiasi gani Mungu
anatupenda, Tunataka kutawala maisha yetu wenyewe, na Tunashindwa kuelewa maana
ya kujisalimisha.
Je,
naweza kumwamini Mungu?
Ndugu yangu, Imani ni
jambo muhimu sana katika kujisalimisha. Huwezi kujisalimisha kwa Mungu kama
Mtawa au yeyote yule mwenye hofu ya Mungu, mpaka uwe unamwamini, lakini huwezi
kumwamini Mungu mpaka umfahamu vyema. Hofu hutuzuia kujisalimisha, lakini
upendo huondoa hofu yote. Kadiri unavyotambua jinsi Mungu anavyokupenda, ndivyo
kujisalimisha kunavyokuwa rahisi. Jambo hili halitegemei umri wetu wa ukristo
wetu, wala kwa maisha ya utawani.
Je,
unajuaje Mungu anakupenda?
Ndugu yangu, Mtawa
mwenzangu, nawe mwenye hofu ya Mungu, Mungu anakupa ushindi mwingi: Mungu
anasema anakupenda, "Bwana ni mwema kwa watu wote, Na rehema zake zi juu
ya kazi zake zote." Zab 145:9. Hautoki kwenye uangalizi wake kamwe,
"Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu, umeelewa na njia zangu
zote," Zab 139:3. Yeye anaangalia mambo yote ya maisha yako, "Lakini
ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote," Mt 10:30. Alikupa
uwezo wa kufurahia aina zote za viburudisho, "bali wamtumaini Mungu
atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha," 1Tim 6:17b. Ana
mpango mzuri kwa ajili ya imani yako, "Maana nayajua mawazo ninayowawazia
ninyi; asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini
siku zote za mwisho," Yer 29:11. Yeye hukusamehe, "Kwa maana Wewe,
Bwana, Umekuwa tayari kusamehe, Na mwingi wa fadhili, kwa watu wote
wakuitao," Zab 86:5. Na kwa upendo anakuvumilia, "Bwana ana fadhili,
ni mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema," Zab
145:8. Ndugu na Mtawa mwenzangu nawe mwenye hofu ya Mungu, Mungu anakupenda
kiasi kisichopimika kuliko unavyoweza kufikiri.
Uthibitisho wa ukweli
huu ni dhabihu ya Mwana wa Mungu kwa ajili yako. "Bali Mungu aonyesha
pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu,
tulipokuwa tungali wenye dhambi, " Rum 5:8. Kama unataka kufahamu uthamani
wako mbele za Mungu, mwangalie Yesu Kristo na mikono yake ilivyowambwa, akisema,
"nakupenda sana! Bora nife kuliko kukukosa."
Ndugu yangu mwenye hofu
ya Mungu, na Mtawa mwenzangu, Mungu siyo kiongozi katili wa msafara wa watumwa
au mchokozi anayetumia mabavu kutulazimisha kumtii. Hajaribu kuvunja utashi
wetu, lakini hutusihi ili tujitoe wenyewe kwake kwa kupenda. Mungu ni mpendwa
na mkombozi, na kujisalimisha kwake huleta uhuru, siyo utumwa.
Tunapojisalimisha kwa Yesu kikamilifu, tunagundua kwamba yeye si mtawala wa
IMLA, lakini RAFIKI ANAYE KUKUBALI MIPAKA YETU. Kikwazo kingine cha kujisalimisha
kikamilifu ni majivuno yetu. Hatukubali kwamba sisi ni viumbe tu na kwamba
hatuna utawala juu ya kila kitu. Hili ni jaribu kila zamani "mtakuwa kama
Mungu, " Mwa 3:8, tamaa hiyo ya kuwa na utawala juu ya kila kitu ni chanzo
cha matatizo mengi katika maisha yetu. Maisha ni mapambano, lakini jambo ambalo
watu wengi hawaelewi ni kwamba mapambano yetu kama yale ya Yakobo hakika ni
mapambano na Mungu! Tunataka kuwa sawa na Mungu, na haitawezekana sisi kushinda
pambano hilo.
A. W. Tower alisema,
"sababu kwa nini watu wengi bado wanasumbuka, bado wanatafuta, bado
wanafanya maendeleo kidogo ni kwa vile bado hawajafikia mwisho wao wenyewe.
Bado tunajaribu kuamuru na kuingilia kazi ya Mungu ndani yetu."
Ndugu yangu, sisi siyo
Mungu na hatuta kuwa kamwe. Sisi ni wanadamu. Ni pale tunapojaribu kuwa Mungu
ndipo tunaishia kuwa kama Shetani kabisa, ambaye alitamani jambo hilo hilo.
Tunakubali ubinadamu
wetu kiakili lakini siyo kihisia. Tunapokabiliwa na mapungufu yetu, ndipo
tunaonyesha uchungu, hasira na chuki. Tunataka kuwa warefu (au wafupi), wenye
akili, wenye nguvu, wenye vipawa, warembo, na matajiri. Tunataka kuwa na kila
kitu na kufanya kila kitu na tunakata tamaa inaposhindikana. Kisha tunatambua
kwamba Mungu aliwapa watu wengine vipawa ambavyo sisi hatuna, na hivyo
tunapatwa husuda, wivu, na kujisikitikia.
Nini
maana ya kujisalimisha?
Kujisalimisha kwa Mungu
si kujiuzulu na kukaa tu kusubiri, au kuamini kuwa yote yameandikwa binadamu hana
hiari, au kuwa na udhuru na wivu. Siyo kukubali hali hiyo hiyo uliyo nayo.
Inaweza kumaanisha kinyume cha haya; kujitoa sadaka maisha yako au kuteseka ili
kubadilisha yanayohitaji kubadilishwa. Mara nyingi Mungu huwaita watu
waliojisalimisha kwake kupiga vita kwa jina lake.
Ndugu, kujisalimisha
sio kwa uoga au mazulia. Mungu asingependa kupoteza akili alizokupa! Mungu
hapendi watu wawe kama mitambo (robots) ili kumtumikia. Kujisalimisha siyo
kukomesha utu wako. Badala ya kukomesha utu wako, kujisalimisha huutia nguvu.
C. S. Lewis alisema, "kadiri tunavyomruhusu Mungu atutawale ndivyo
tunavyozidi kuwa sisi wenyewe-kwa sababu yeye ndiye aliyetuumba. Alibuni namna
mbalimbali za watu wote tofauti ambao mimi na wewe tulikusudiwa kuwa...Ni pale
ninapomgeukia Kristo, ninapojikabidhi nafsi yangu kwake, ndipo ninapokuwa na
ule utu wangu halisi."
Kujisalimisha
kunadhihirika vyema katika kutii. Ukisema 'ndiyo, Bwana' kwa chochote
anachokueleza. Kusema "Hapana, Bwana" ni kutamka vinyume. Hatuweza
kumwita Yesu Bwana na wakati huo huo hatutaki kumtii. Baada ya usiku kucha bila
kupata samaki, Simoni Petro alionyesha kujisalimisha pale Yesu alipomwambia
kujaribu tena. "Simoni akajibu akamwambia, Bwana Mkubwa, tumefanya kazi ya
kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha
nyavu," Lk 5:5. Watu waliojisalimisha hutii neno la Mungu hata kama
linaonekana kutokuwa na maana.
Ndugu yangu na Mtawa
mwenzangu, nawe mwenye hofu ya Mungu, jambo lingine katika kujisalimisha ni
IMANI. Ibrahimu (Mwa 12: 1-4) alifuata maelezo ya Mungu bila kujua alikokuwa
akienda. Hana (1Sam 1:1-20) alisubiri wakati wa Mungu bila kujua ni lini. Mama
Bikira Maria (Lk 1:26-35) alitarajia muujiza bila kufahamu utatendekaje. Yusufu
mume wa Bikira Maria (Mt 2: 19-25) aliamini lengo la mungu bila kujua kwa nini
mazingira yalikuwa hivyo. Kila mmoja wa watu hawa alikuwa amejisalimisha kwa
Mungu alipomtegemea bila kujibakiza.
Utafahamu
umejisalimisha kwa Mungu unapomtegemea Mungu akutengenezee mambo yako badala ya
kujaribu kuwafanyia hila wengine, ukapitisha jambo lako, na mwisho ukatawala
mazingira hayo. "Ukae kimya mbele za Bwana, Nawe umngojee kwa
saburi," Zab 37:7a. Baada ya kujaribu sana, umwamini zaidi. Pia ufahamu
kwamba unajisalimisha unapokuwa huchukizwi na lawama na kukimbilia kujitetea.
Mioyo iliyojisalimisha huonyesha mahusiano mazuri na wengine. Huwatupilia mbali
wengine, hudai haki zako, na hutumikii nafsi yako kama umejisalimisha.
Eneo gumu kwa watu
wengi kujisalimisha ni mali na pesa zao. Wengi wamefikiri, "Nataka kuishi
kwa ajili ya Mungu lakini pia nataka kupata pesa nyingi ili niishi kwa raha
baadaye nipumzike." Kupumzika siyo lengo la maisha ya kujisalimisha, kwa
sababu huku ni kushindana na Mungu kwa sababu ya kuweka mkazo kwanza kwa maisha
yetu. Yesu anasema, "hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa
maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau
huyu," Mt 6:24 na kwamba "kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo
utakapokuwapo na moyo wako," Mt 6:21.
Ndugu yangu, kielelezo
kikubwa cha kujisalimisha ni Yesu. Usiku ule kabla ya mateso Yesu
alijisalimisha kwa mpango wa Mungu. Alisali, "Aba, Baba, yote yawezekana
kwako; uniondolee kikombe hiki; walakini, si kama nitakavyo mimi, bali utakavyo
wewe," Mk 14:36. Yesu hakuomba, "Baba, kama unaweza kuniondolea
maumivu haya, tafadhali fanya hivyo." Alikuwa tayari amethibitisha kuwa
Mungu ana uwezo wa kufanya lolote! Badala yake anaomba, "Mungu kama
inapendeza kwako kuniondolea mateso haya, tafadhali fanya hivyo. Lakini kama
yanatimiza kusudi lako, ndivyo ninavyotaka pia.
Kujisalimisha halisi
husema, "Baba, kama tatizo hili, maumivu haya, ugonjwa huu, au hali yoyote
inahitajika kutimiza lengo lako na utukufu kwako katika maisha yangu au ya
mwingine, tafadhali usiliondoe." Kiwango hiki cha ukomavu hakiji kwa
urahisi. Kwa upande wa Yesu, aliugua sana kuhusu mpango wa Mungu kiasi cha
kutoa jasho la damu. Kwa upande wetu, ni vita kali dhidi ya asili yetu ya
ubinafsi.
Je,
baraka za kujisalimisha ni zipi?
Maandiko Matakatifu
yapo wazi kabisa kuhusu unavyoweza kufaidika unapojisalimisha kikamilifu kwa
Mungu. Kwanza unapata amani: "mjue sasa Mungu, ili uwe na amani; Ndivyo
mema yatakavyokujia," Ayu 22:21. Pili, unapata uhuru: "lakini Mungu
na ashukuriwe, kwa maana mlikuwa watumwa wa dhambi, lakini mliitii kwa mioyo
yenu ile namna ya elimu ambayo mliwekwa chini yake," Rum 6:17.
Tatu, unapata nguvu za
Mungu katika maisha yako. Majaribu makali na matatizo mazito yanaweza kushindwa
na Kristo kama atakabidhiwa. Joshua alipoviendea vita vile vikubwa maishani
mwake, (Yosh 5:13-15) alikutana na Mungu, akamsujudia, na akasalimisha mipango
yake. Kujisalimisha huko kulileta ushindi mkubwa pale Yeriko.
Hiki ni kitendawili:
Ushindi huja kwa kujisalimisha, kujisalimisha hakukudhoofishi wewe; kunakutia
nguvu. Jisalimishe kwa Mungu, hauhitaji kuogopa au kujisalimisha kwa chochote
kile. William Booth, mwanzilishi wa Jeshi la wokovu, alisema, "ukuu wa
nguvu za ubinadamu unapimwa kwa kiwango chake cha kujisalimisha."Watu
waliojisalimisha ndio Mungu anawatumia. Mungu alimchagua Bikira Maria Mama wa
Yesu, siyo kwa sababu alikuwa na kipawa, au utajiri wa uzuri wa umbile, lakini
kwa sababu alikuwa amejitoa kikamilifu kwake. Malaika wa Bwana alipomwelezea
mpango mgumu wa Mungu, alijibu kwa upole, "Tazama, mimi ni mjakazi wa
Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema," Lk 1:38a. Hakuna kitu kikubwa kama
maisha ya kujisalimisha katika mikono ya Mungu. "Basi mtiini Mungu.
Mpingeni Shetani, naye
atawakimbia," Yak 4:7a.
Je,
njia bora ya kujisalimisha ni ipi?
Kila mtu hatimaye
hujisalimisha kwa mtu au kitu fulani. Kama sio kwa Mungu, utajisalimisha kwa
matarajio au maoni ya watu wengine, au pesa, chuki, hofu, au kwa kiburi chako
au tamaa mbaya, au ubinafsi. Uliumbwa kumwabudu Mungu na kama utashindwa
kumwabudu, utatengeneza vitu vingine (sanamu) ili uvipe maisha yako.
Ndugu yangu na Mtawa
mwenzangu, nawe mwenye hofu ya Mungu, unao uhuru wa kuchagua usalimishe maisha
yako, lakini huko huru na matokeo ya uchaguzi huo. E. Stanly Jones alisema,
"kama hujajisalimisha kwa Kristo, utajisalimisha kwa machafuko." Kijisalimisha
si njia bora ya kuishi; ni njia pekee ya kuishi. Hakuna kitu kingine cha
kukufanikisha. Njia nyingine zote hukuongoza kwenye kukutatisha tamaa, na
kuziangamiza nafsi. Tafsiri ya King James huita kujisalimisha "huduma yenu
yenye maana," Rum 12:1. Tafsiri nyingine inasema, "njia yenye maana
zaidi ya kumtumikia." Rum 12:1.
Kusalimisha maisha yako
si hisia za kipumbavu kama wengu watuonavyo leo sisi Watawa, bali ni tendo la akili na busara ambalo
unaweza kulifanya kwa ajili ya maisha yako. Ndiyo maana Mtume Paulo anasema,
"kwa hiyo tena, ikiwa tupo hapa, au ikiwa hatupo hapa, twajitahidi
kumpendeza yeye," 2Kor 5:9. Nyakati zako za busara zitakuwa zile ambazo
unasema ndiyo kwa Mungu.
Wakati mwingine
huchukua miaka, lakini hatimaye unagundua kwamba kizuizi kikubwa kwa Baraka za
Mungu maishani mwako sio watu wengine, ni wewe mwenyewe-matakwa yako binafsi,
kiburi cha hali ya juu, na matarajio yako. Huwezi kutimiza lengo la Mungu kwa
maisha yako huku ukikazania malengo yako binafsi.
Kama ataenda kufanya
kazi ndani yako, itaanza hivyo. Kwa hiyo mpe yote Mungu: kushindwa kwako hapo
nyuma, matatizo yako ya sasa, matarajio yako ya mbele hofu zako, ndoto,
udhaifu, tabia, maumivu, na madhara yoyote uliyo nayo. Mtawa mwenzangu, nawe
mwenye hofu ya Mungu, mweke Yesu katika kiti cha dereva wa maisha yako na
uondoe mikono yako toka kwenye usukani. Usiogope; hakuna chochote katika
uongozi wake kinaweza kupoteza dira. Chini ya uongozi wa Kristo unaweza kudumu
chochote. Utakuwa na Mtume Paulo, "Nayaweza mambo yote katika yeye
anitiaye nguvu," Flp 4:13
Wapendwa wana wa Mungu,
kujisalimisha kwa Paulo kulitokea katika njia ya Dameski alipoangushwa chini na
mwanga mkali uliompofusha. Kwa watu wengine, Mungu anapata mwitikio wetu bila
kutumia njia ya ajabu sana. Pamoja na hayo kujisalimisha siyo tukio la wakati
mmoja tu. Kuna wakati wa kujisalimisha, na kuna tendo la kujisalimisha, ambalo
ni la muda-hadi-muda na maisha yote. Tatizo la sadaka iliyo hai ni kwamba
inaweza kutambaa na kutoka madhabahuni, hivyo unaweza kutakiwa kujisalimisha
hata mara hamsini kwa siku. Ni lazima ufanye jambo hili kuwa tabia yako ya kila
siku. Yesu anasema, "mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe,
ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate," Lk 9:23
Ngoja nikuonye:
unapoamua kuishi maisha ya kujisalimisha kikamilifu, uamuzi huo utapimwa.
Wakati mwingine itamaanisha kufanya mambo yasiyostahili, ya gharama, au
yanayoonekana hayawezekani. Mara nyingi itamaanisha kufanya kinyume cha
unavyojisikia kufanya. Mmoja ya viongozi wakuu wa Kikristo wa karne ya ishirini
alikuwa Bill Bright, mwanzilishi wa Campus Crusade for Christ. Kwa kutumia
watumishi wa shirika hili duniani pote, kipeperushi cha sheria nne za kiroho,
na filamu ya Yesu (iliyoonwa na watu zaidi ya bilioni nne), zaidi ya watu
milioni 150 wamekuja kwa Yesu.
Siku moja mtu mmoja
alimuuliza Bill, "Kwa nini Mungu anakutumia na kukubariki maisha yako
kiasi kikubwa hivyo? Alisema, "Nilipokuwa kijana mdogo, nilifanya mkataba
na Mungu. Niliandika na kutia sahihi ya jina langu chini yake. Mkataba huo
ulisema. 'Tangu siku hii ya leo na kuendelea, mimi ni mtumwa wa Kristo.'"
Je, umewahi kusaini
mkataba kama huo na Mungu? Au bado
unabishana na kupambana na Mungu juu ya haki yake kufanya lolote apendalo kwa
maisha yako? Ndugu na Mtawa mwenzangu, sasa ni wakati wako kujisalimisha-kwa
neema ya Mungu, upendo na hekima yake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Basi
wewe, mwanangu, uwe hodari katika neema iliyo katika Kristo Yesu,” 2Tim 2:1
No hay comentarios:
Publicar un comentario