jueves, 14 de enero de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 1 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI YA 1 YA MWAKA-C
15/1/2016
Somo: 1Sam 8:4-7, 10-22a
Zab: 89:16-17, 18-19
Injili: Mk 2:1-12
Nukuu:
Ndipo wazee wote wa Israeli wakakutana pamoja, wakamwendea Samweli huko Rama; wakamwambia, Angalia, wewe umekuwa mzee, na wanao hawaendi katika njia zako; basi, tufanyie mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote,” 1Sam 8:4-5 

Lakini neno hilo likawa baya machoni pa Samweli, waliposema, Tupe mfalme atuamue. Naye Samweli akamwomba Bwana,” ISam 8:6 

Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti ya watu hawa katika kila neno watakalokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao,” 1Sam 8:7 

Walakini hao watu wakakataa kuisikiliza sauti ya Samweli; wakasema, Sivyo hivyo; lakini tunataka kuwa na mfalme juu yetu;  ili sisi nasi tufanane na mataifa yote; tena ili mfalme wetu atuamue, tena atoke mbele yetu na kutupigia vita vyetu,” 1Sam 8:19-20

Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti yao, ukawafanyie mfalme,” 1Sam 8:22 

Wakaja watu wakimletea mtu mwenye kupooza, anachukuliwa na watu wanne,” Mk 2:3

Na walipokuwa hawawezi kumkaribia kwa sababu ya makutano, waliitoboa dari pale alipokuwapo; na wakiisha kuivunja wakalitelemsha godoro alilolilalia yule mwenye kupooza,” Mk 2:4

Naye Yesu, alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako,”Mk 2:5

Na baadhi ya waandishi walikuwako huko, wameketi, wakifikiri mioyoni mwao, Mbona huyu anasema hivi? Anakufuru. Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa mmoja, ndiye Mungu?” Mk 2:6-7

Mara Yesu akafahamu rohoni mwake kwamba wanafikiri hivyo nafsini mwao, akawaambia, Mbona mnafikiri hivi mioyoni mwenu?” Mk 2:8 

Vyepesi ni vipi, kumwambia mwenye kupooza, Umesamehewa dhambi zako, au kusema, Ondoka, ujitwike godoro lako, uende?” Mk 2:9 

Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (hapo amwambia yule mwenye kupooza)” Mk 2:10 

TAFAKARI:Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi.”

Wapendwa wana wa Mungu, maisha ni pamoja na kuzikabili changamoto za kila siku. Ila jambo la kukumbuka ni kwamba changamoto hizi ziwe sehemu za makuzi yako kimwili na kiroho. Mtu ukua kimwili na kiroho anapoikamili changamoto husika kwa mwelekeo ulio sahihi na bila kupoteza malengo yake kuelekea kule kuliko sahihi-uzima wa milele. Wengi wetu hupenda kuzikabili changamoto kwa njia rahisi na za mikato. Ukweli ni kwamba chochote kile ‘rahisi’ kwisho wa siku huwa ‘ghali.’

Wapo pia baadhi yetu uzikabili changamoto kwa mtazamo ‘mfanano’ kwa lengo la kujiridhisha nafsi baada ya kutamani kitu hicho kwa muda mrefu bila kukipata. Mfano kama ulitamani gari kama alilokuwa nalo jirani yako na hukuwa na uwezo wa kulinunua, inapotokea nafasi ya kupata hata lililo bovu ila linamfanano na lile jirani yako na lipo chini ya uwezo wako kifedha, mtu huyu ulinunua tu ili kukidhi tamaa ya moyo wake. Ila vilivyo ‘rahisi’ mwisho huwa ‘ghali.’ Matokeo yake ni kwamba badala ya kusonga mbele kimaisha hurudi nyumba kwa sababu matunzo ya gari hili bovu ulilolinunua ujeuka kuwa kitafuno cha fedha na mali zako zote ulizokwisha kukusanya muda mrefu kwa shida na taabu.

Hali hii ndiyo iliyowakuta wana wa Israeli wakiongozwa wa WAZEE walipomwendea Samweli na kumwambia, “Angalia, wewe umekuwa mzee, na wanao hawaendi katika njia zako; basi, tufanyie mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote,” 1Sam 8:5. Maisha ya wana wa Israeli muda wote yalikuwa mikoni mwa Mungu. Mungu ndiye aliyekuwa kiongozi wao na aliwaongoza vyema ingawa hapa na pale waliweza kumwasi. Mungu alibaki na amebaki kuwa Upendo na Huruma. Mungu wetu si kama mtu katili mwenye kuwashurutisha watu kama alivyo kamanda wa vita. Kama mzazi aliyekomaa kimaadili, Lk 15:11-32 (soma habari ya mwana mpotevu), Mungu uruhusu yale tuyapendayo ili tujionee wenyewe kama waswahili wasemavyo, ‘mtoto akilia wembe mpe.’ Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti ya watu hawa katika kila neno watakalokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao,” 1Sam 8:7. Hata pamoja na kupewa angalizo la mfalme huyo wanayemtaka kutokuwa mzuri, 1Sam 8:11-18, bado wanang’ang’ania kile wasichokijua. Walakini hao watu wakakataa kuisikiliza sauti ya Samweli; wakasema, Sivyo hivyo; lakini tunataka kuwa na mfalme juu yetu;  ili sisi nasi tufanane na mataifa yote; tena ili mfalme wetu atuamue, tena atoke mbele yetu na kutupigia vita vyetu,” 1Sam 8:19-20. Hakika sikio la kufa halisikii dawa. Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti yao, ukawafanyie mfalme,” 1Sam 8:22. Hivi ndivyo Waisraeli walipotamani kuwa na mfalme na Mungu aliruhusu. Mfalme atakayechaguliwa ndiye yule aliyejulikana kama Mfalme Sauli. Chini ya mfalme huyu taifa hili liliyumba sana na kukosa amani na mwelekeo.

Wapendwa katika Kristo, nasi kwa namna fulani hupenda kuwa huru ndani ya nafsi zetu na kwa namna hiyo humtafuta mfalme na kumkabidhi nafsi yako aiongoze. Mfalme huyu aweza kuwa ulevi, fedha, chuki, majungu, wivu, zinaa, nk. Unapoikubali roho hizi ndani yako na kuruhusu kuwa roho hiyo kuyaongoza maisha yako, basi ujue ni kwa namna hiyo hiyo tunamkataa Mungu kuwa kiongozi wa maisha yetu. Hapa hapatakuwa na usalama hata kidogo.

Somo la Injili leo tunaona mamlaka aliyokuwa nayo Yesu yanahojiwa. Wengi wanamwona Yesu katika mtazamo ‘mfanano.’ Licha ya ishara nyingi alizozifanya Yesu baadhi ya watu hawakuona zaidi na ishara zile. Wapo walimchukulia Yesu kama mwana mazingaumbwe fulani hivi. Lakini Yesu anasema, Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba,” Yoh 10:37-38. Kwa kutambua ukweli huu, Yesu anayasema maneno haya bila kupepesa macho kutokana na kutokulipokea tendo lile kama tendo la Mungu baada ya kumponya mtu yule aliyekuwa amepooza. Kwa kutambua yaliyokuwa mioyoni mwao, Yesu akawaambia, lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (hapo amwambia yule mwenye kupooza)” Mk 2:10. Wapo kati yetu hadi leo hawaambia uwezo wa Yesu na nafasi yake katika fumbo zima la Utatu Mtakatifu. Utatu Mtakatifu huu, yaani Mungu Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, ni umoja usiogawanyika. Ilipo nafsi moja katika utendaji na nafsi nyingine uwepo hapa hapa.

Tumsifu Yesu Kristo!

Mimi na Baba tu umoja,” Yoh 10:30

No hay comentarios:

Publicar un comentario