JUMAMOSI BAADA YA EPIFANIA, KIPINDI CHA NOELI
9/1/2016
Somo: 1Yoh 5:14-21
Zab: 149: 1-2, 3-4, 5-6a, 9b
Injili: Yoh 3:22-30
Nukuu:
“Na huu ndio ujasiri
tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia,”
1Yoh 5:14
“Mtu akimwona ndugu
yake anatenda dhambi isiyo ya mauti, ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili
ya hao watendao dhambi isiyo ya mauti. Iko dhambi iliyo ya mauti. Sisemi ya
kwamba ataomba kwa ajili ya hiyo,” 1Yoh 5:16
“Kila lisilo la haki
ni dhambi, na dhambi iko isiyo ya mauti,” 1Yoh 5:17
“Twajua ya kuwa kila
mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi; bali yeye aliyezaliwa na Mungu
hujilinda, wala yule mwovu hamgusi,” 1Yoh 5:18
“Nasi twajua kwamba
Mwana wa Mungu amekwisha kuja, naye ametupa akili kwamba tumjue yeye aliye wa
kweli, nasi tumo ndani yake yeye aliye wa kweli, yaani, ndani ya Mwana wake
Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli, na uzima wa milele,” 1Yoh 5:20
“Watoto wadogo,
jilindeni nafsi zenu na sanamu,” 1Yoh 5:21
“Basi palitokea
mashindano ya wanafunzi wa Yohana na Myahudi mmoja juu ya utakaso,” Yoh 3:25
“Yohana akajibu,
akasema, Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni,”
Yoh 3:27
“Ninyi wenyewe
mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake,”
Yoh 3:28
“Aliye naye bibi arusi
ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na
kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana arusi,” Yoh 3:29
“Basi hii furaha yangu
imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua,” Yoh 3:30
TAFAKARI: “Watoto wadogo, jilindeni
nafsi zenu na sanamu. Yeye hana budi kuzidi (Kristo), bali mimi kupungua.”
Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu yote mawili wanatutaka
tutafakari fadhila ya ‘unyenyekevu.’ Hivyo, “Watoto
wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu. Yeye hana budi kuzidi (Kristo), bali
mimi kupungua.” Neno ‘watoto wadogo’ limebeba umbo la ‘unyenyekevu,’ na wito wa
kuishi fadhila hiyo. Sifa chache za utoto katika udogo ni ule utayari kwa
kupokea pasipo shaka yale aambiwayo na wazazi wake. Utoto katika udogo ni ile
hali ya kuamini pasipo shaka. Na utoto katika udogo ni ile hali ya kuwa wazi
katika kweli na haki.
Neno
‘kujilinda nafsi na sanamu,’ linakutaka uelewa mwegemeo wa nafsi yako upo wapi.
Hivyo basi kabla ya kujua nafsi yako imeegemea wapi ni vyema tukaitazama NAFSI
katika uhusiano wake kati ya MWILI na ROHO kadiri ya Maandiko Matakatifu. Mtu kamili anakuwa katika sehemu kuu
tatu:- Nafsi, Roho, na Mwili. “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi Nafsi
zenu na Roho zenu na Miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila
lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.” I The 5:23
Katika hili Roho na Nafsi huwa pamoja na ndizo wewe
mwenyewe. Mwili ni nyumba ya roho na nafsi. Katika uumbaji Mungu aliumba mwili
kwa udongo halafu akapulizia pumzi puani ambayo ni roho yake ndipo mtu huyo
akawa nafsi iliyo hai. “Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi,
akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Mwa. 2:7. Miili
tuliyonayo ni nyumba ya Nafsi na Roho. Kwa hali hii sisi binadamu ni wawili.
Kuna mtu wa ndani na mtu wa nje. Mtu wa ndani ni Nafsi na Roho, na mtu wa nje
ni Mwili lakini watu hawa wapo pamoja hatuwezi kuwatenganisha wala kumwona kwa
macho ya nyama huyu mtu wa ndani, ila yupo.
Katika hili twaona haya yafuatayo:- Huyu mtu wa nje hukua,
kuzeeka na kufa. Mtu wa ndani hakui, hazeeki, wala hafi. Mtu wa ndani
hubadilika kwa kuchakaa kunakotokana na kujeruhiwa na kuumizwa kunakosababishwa
na dhambi na matukio mbalimbali yanayomsibu binadamu. Mtu wa ndani alianza
tangu pale kutungwa mimba siku ya kwanza wakati yai na mbegu na pumzi ya Mungu
alipoweka roho yake. Mtu huyu wa ndani hakui wala haongezeki ila hufanywa upya.
“Kwa hiyo hatulegei, bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu
wa ndani unafanywa upya siku kwa siku,” 2Kor 4:16. Kwa hiyo huyu mtu wa nje
akifa mtu wa ndani huenda mahali atakapokuwa amejiandalia ama Mbinguni au
motoni.
Wapendwa wana wa Mungu, kwenye Nafsi ndipo penye tatizo
lenyewe kwani ni katikati ya Roho na Mwili. Nafsi hutawaliwa na Hisia, mfano:-
Hofu, Chuki, Hasira, Kujihukumu, Kujikataa, Kukosa furaha, Kukosa upendo,
Kukosa amani, n.k. Ni muhimu sana mtu atawale hisia zake. Nafsi ikiegemea
rohoni huleta matunda mazuri. “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani,
uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo
hakuna sheria.” Gal. 5:22-23. Ila nafsi inapoegemea Mwili mambo huwa mabaya
kwani ufanya matendo ya mwili kama tusomavyo katika maandiko matakatifu, “basi
matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya
sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi husuda,
ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama
nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo
hawataurithi ufalme wa Mungu.” Gal.5:19-21. Ni vizuri kujua nafsi yako
imeegemea wapi. Ikiegemea rohoni utaenda Mbinguni, ikiegemea mwilini utaenda
motoni.
Hivyo wapendwa katika Kristo, kujilinda nafsi na sanamu ni
kuiruhusu nafsi yako kuegemea katika matendo ya mwili. Sanamu hizo ambazo
tunapewa angalizo leo ni hizi: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu,
uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi husuda, ulevi,
ulafi, na mambo yanayofanana na hayo mfano: fedha, sifa, mamlaka na kujiinua
zaidi ya Muumba wako, na kujulikana kunakofifisha utukufu wa Mungu. Hizi zote
ni sanamu. Mambo haya yakiwa ndiyo dira ya maisha yako kamwe Kristo hawezi
kupata nafasi katika maisha yako hata kama utafanya mambo mazuri kupitia miwani
ya Kanisa au Vyama vya kitume. Yote hayo utakayoyafanya yatakuwa na lengo la
kujitukuza mwenyewe ukimwinua sanamu SIFA.
Ili niepukane sanamu hizi yanipasa niielekeze nafsi yangu
katika tunda la Roho. Tunda hili la Roho litabadili mfumo mzima wa maisha yangu
kutoka hali ya kujitukuza na kuelekea hali ya kujinyenyekeza. Tunda la Roho ni
hili: upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole,
kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Katika hali hii Kristo atapata
nafasi katika maisha yangu kwa sababu, “Yeye hana
budi kuzidi, bali mimi kupungua,” Yoh 3:30b. Yohane Mbatizaji ni mfano hai wa
yule aliyeishi tunda la Roho. Yohane Mbatizaji anajua mipaka yake na kile
kimpasacho kufanya kadiri ya mipaka hiyo. “Ninyi wenyewe
mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake,”
Yoh 3:28. Huku ndiko kuishinda nafsi na kukumbatia tunda la Roho.
Anayeishi
katika tunda la Roho ni “Mtu yule amwonaye ndugu yake anatenda dhambi isiyo ya mauti,
ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao watendao dhambi isiyo ya
mauti,” 1Yoh 5:16a. Moja ya dhambi isiyo ya
mauti ni dhambi ile tunayoikiri katika sala ya ‘Nakuungamia Mungu Mwenyezi…,’
yaani dhambi ya “kutotimiza wajibu.” Tunapoishi katika tunda la Roho, nafsi
yetu ukiri uwepo wa Kristo kwa kila tunayekutana naye. Hivyo, “Nasi twajua kwamba Mwana wa Mungu amekwisha kuja, naye ametupa
akili kwamba tumjue yeye aliye wa kweli, nasi tumo ndani yake yeye aliye wa
kweli, yaani, ndani ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli, na
uzima wa milele,” 1Yoh 5:20. Ufunuo huu wa nafsi katika uwepo wa Kristo ndani
na katika maisha yetu unatupeleka karibu
zaidi na Mungu na kututenga na dhambi. “Twajua ya kuwa kila
mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi; bali yeye aliyezaliwa na Mungu
hujilinda, wala yule mwovu hamgusi,” 1Yoh 5:18.
Ndugu yangu tuliyesafiri
wote katika tafakari hii nikuombe ufanye tafiti NAFSI yako ili uweze kubaini
egemeo la nafsi lako lipo wapi. Na utakapo gundua nafsi yako ilipoegemea na
hasa katika tunda la Roho utajawa na furaha na kusema kama alivyosema Yohane
Mbatizaji, “Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake
bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana
arusi. Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi
kupungua,” Yoh 3:29-30. Bwana harusi wetu ni
Kristo mwenyewe. Kiti chake cha Kifalme ni Msalaba wake Mtakatifu, na Kofia
yake ya Kifalme ni taji lile la miiba. Haya ndiyo ya kujisifia katika maisha
yangu kila siku ninapompa Kristo nafasi ndani ya maisha yangu kama
Mkristo-mfuasi wa Kristo. AMINA.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini mimi, hasha,
nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo,
ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14
No hay comentarios:
Publicar un comentario