lunes, 25 de enero de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA WATAKATIFU TIMOTEO NA TITO, MAASKOFU

SIKUKUU YA WATAKATIFU TIMOTEO NA TITO MAASKOFU
26/1/2016
Somo: 2Tim 1:1-8
Zab: 96:1-2ab, 3, 7-8a, 10
Injili: Mk 3:31-35        
Nukuu:
 kwa Timotheo, mwanangu mpendwa. Neema na iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Bwana wetu,” 2Tim 1:2

nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo,” 2Tim 1:5

Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,” 2Tim 1:7

Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu,” 2Tim 1:8

Akawatazama wale walioketi wakimzunguka pande zote, akasema, Tazama, mama yangu na ndugu zangu!” Mk 3:34

Kwa maana mtu ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu,” Mk 3:35

TAFAKARI: “Usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Watakatifu Timeteo na Tito Maaskofu. Timoteo na Tito, wanafunzi na washirika wa Mtume Paulo walikuwa mstari wa mbele kwa kulijenga na kuliimarisha Kanisa la Efeso, na baadaye huko Crate. Wote wawili walielekezwa na Mtume Paulo kwa barua zilizojulikana kama barua za kichungaji. Ndani ya maelekezo ya barua hizi kulikuwa na matamko hasa pale kulipotokea upotoshwaji wa jambo fulani, na maonyo kwa mafundisho ya waamini na wachungaji.

 Somo letu la kwanza tunaona Mtume Paulo akiandika barua hii angali gerezani. Na hapa inaonyesha yale aliyowaandikia Wafilipi sasa yameshatokea. Hivyo Paulo Mtume anamtuma Timoteo kwao ili naye apata habari zao. Walakini natumaini katika Bwana Yesu kumtuma Timotheo afike kwenu karibu, nifarijiwe na mimi, nikiijua hali yenu. Maana sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli. Maana wote wanatafuta vyao wenyewe, sivyo vya Kristo Yesu. Ila mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya Injili, kama mwana na baba yake. Basi, natumaini kumtuma huyo mara, hapo nitakapojua yatakayonipata,” Flp 2:19-23

Ni kweli kwamba Mtume Paulo alipendezwa sana na utendaji, ushiriki, na ushupavu  wa imani aliokuwa nao Timeoteo. Mtume Paulo anamchukulia Timoteo kama mwanaye. Kwa Timotheo, mwanangu mpendwa. Neema na iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Bwana wetu,” 2Tim 1:2. Imani aliyokuwa nayo Timoteo ilikuwa thabiti, na kamwe hakutetereshwa na jambo lolote. Akiwa gerezani Paulo anayasema haya juu ya Timoteo, nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo,” 2Tim 1:5

Kama ilivyokuwa uhusiano wa karibu wa Mtume Paulo na Timoteo, ndivyo ilivyokuwa kwa Tito. Barua ndogo kwa Tito tunaona Mtume Paulo anakutana kwa mara ya kwanza na Tito huko Antiokia bila shaka mwaka (48 bk), na Tito alimsindikiza Mtume Paulo kwenye ule mtaguso wa Yerusalemu, Mdo 15. Kisha, baada ya miaka kumi na minne, nalipanda tena kwenda Yerusalemu pamoja na Barnaba, nikamchukua na Tito pamoja nami,” Gal 2:1. Kwa nyakati mbalimbali Tito anawatembelea Wakristo wa Korintho. Lakini ahimidiwe Mungu atiaye bidii ile ile kwa ajili yenu katika moyo wa Tito. Maana aliyapokea kweli yale maonyo; tena, huku akizidi kuwa na bidii, alisafiri kwenda kwenu kwa hiari yake mwenyewe,” 2Kor 8:16-17. Mtume Paulo alimtuma huko kwa sababu kuu mbili; kwanza, kuimarisha maisha ya imani ya jumuiya hiyo ya Korintho. Na pili, kwa shughuli za kimisionari.

Uinjilishaji huu ulikuwa mgumu sana kwa sababu walipambana na kila aina ya upinzani kwa ajili ya habari njema ya wokovu. Mtume Paulo anajua taabu zote hizo na anasema, Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,” 2Tim 1:7. Ni kwa kuushinda woga habari njema zilienea kila pande za dunia. Nasi leo tunajionea na kujivunia majitoleo yao katika kulihubiri neno la Mungu. Ujumbe anaotupatia leo Mtume Paulo kuhusu habari njema ya wokovu ni huu: Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu,” 2Tim 1:8. Yanipasa mimi na wewe kusimama imara katika imani dhabiti pale nilipo. Anza umisionari huo hapo ulipo kwa kuona kama Kristo, kuwaza kama Kristo, Kuamua kama Kristo, na kutenda kama Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!

Watakatifu Timoteo na Tito Maaskofu. Mtuombee


Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!” 1Kor 9:16

No hay comentarios:

Publicar un comentario