martes, 26 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 3 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 3 YA MWAKA-C

Somo: 2Sam 7:4-17
Zab: 88:4-5, 27-28, 29-30
Injili: Mk 4:1-20
Nukuu:
Kwa maana mimi sikukaa ndani ya nyumba, tangu siku ile niliyowatoa wana wa Israeli katika Misri, hata leo, lakini nimekaa katika hema na maskani,” 2Sam 7:6 

Basi, sasa, mwambie mtumishi wangu, Daudi, maneno haya, Bwana wa majeshi asema hivi, Nalikutwaa katika zizi la kondoo, katika kuwaandama kondoo, ili uwe mkuu juu ya watu wangu, juu ya Israeli,” 2Sam 7:8

nami nimekuwa pamoja nawe kila ulikokwenda, na kuwakatilia mbali adui zako wote mbele yako; nami nitakufanyia jina kuu, kama jina la wakuu walioko duniani,” 2Sam 7:9

Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele,” 2Sam 7:13 

lakini fadhili zangu hazitamwondoka, kama vile nilivyomwondolea Sauli, niliyemwondoa mbele yako,” 2Sam 7:15

Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele,” 2Sam 7:16 

Mpanzi huyo hulipanda neno,” Mk 4:14 

Hawa ndio walio kando ya njia lipandwapo neno; nao, wakiisha kusikia, mara huja Shetani, akaliondoa lile neno lililopandwa mioyoni mwao,” Mk 4:15

Kadhalika na hawa ndio wapandwao penye miamba, ambao kwamba wakiisha kulisikia lile neno, mara hulipokea kwa furaha; ila hawana mizizi ndani yao, bali hudumu muda mchache; kisha ikitokea dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara hujikwaa,” Mk 4:16-17 

Na hawa ndio wale wapandwao penye miiba; ni watu walisikiao lile neno, na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai,” Mk 4:18-19 

Na hawa ndio waliopandwa penye udongo ulio mzuri; ni watu walisikiao lile neno na kulipokea, na kuzaa matunda, mmoja thelathini, mmoja sitini, na mmoja mia,” Mk 4:20 

TAFAKARI: “Na tuutafute  udongo mzuri ili tuzae matuma. Nalo ndilo neno la uzima.”

Wapendwa wana wa Mungu, ulimwengu wetu wa leo umekamatwa na vipaumbele vyake ambavyo ukichunguza kwa undani havina uhai ndani yake. Miaka kumi na tano iliyopita kwa mkristo kwenye hofu ya Mungu kabla ya kuanza safari yake  hakuweza kuondoka nyumbani bila kuhakikisha Rozali yake ipo mfukoni. Leo jambo la kwanza kabla yote kuweka mfukoni ni simu ya mkononi. Na wakati mwingine mtu yupo tayari hata kulala njaa lakini simu yake iwe na salio.

Leo siyo kwamba watu hawaamini uwepo wa Mungu tu, bali hawataki kabisa kusikia habari zake. Mungu aliye Upendo, Huruma, Haki na Amani, amejeuzwa kuwa adui kwa wale walioutanguliza mbele ulimwengu na malimwengu yake. Na pale Mungu anapotafutwa lengo lake ni kumtaka Mungu afanye kadiri ya mapenzi yetu. Mungu huyu tunamtafuta kwa bidii pale mipango yetu inapokwama na hatuna namna ya kujikwamua katika matatizo yetu. Tunamjeuza Mungu wetu kuwa kama Shirika la Msalaba mwekundu.

Leo Yesu anatupa mfano wa Mpanzi akitutaka kuujenga uhusiano mzuri na Mungu kupitia neno lake. Neno la Bwana ni uzima kwetu na neno hilo hututoa mautini na kuingia uzimani. Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani,” Yoh 5:24. Maadui wa neno la Mungu wa kwanza ni shetani na hila zake. Ila shetani wa mtu ni mtu mwenyewe. Unaporuhusu hali ya ukavu ndani ya maisha yako ndivyo hivyo hivyo unavyo yapalilia makazi ya shetani ndani ya nafsi yako.Hawa ndio walio kando ya njia lipandwapo neno; nao, wakiisha kusikia, mara huja Shetani, akaliondoa lile neno lililopandwa mioyoni mwao,” Mk 4:15. Ni vyema kila siku ukawa hata na dakika 15 za kulisoma neno la Mungu na kulifanya lako. Usomapo neno hilo jiulize linasema nin juu ya maisha yako.

Adui wa pili kuhusu neno la Mungu ni dhiki na udhia katika maisha yetu. Katika dhiki za maisha na udhia Yesu anatuambia neno la uzima kwamba Yeye kesha ushinda ulimwengu hivyo tuwe na imani ndani yake. Naye Yesu anasema, Tazama, saa yaja, naam, imekwisha kuja, ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami. Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu,” Yoh 16:32-33. Ndugu yangu bila kushikamana na Kristo aliyeushinda ulimwengu katika dhiki na udhia hutaweza kuushinda ulimwengu huu kwa nguvu zako mwenyewe. Kuzitumainia nguvu zako ni kuelekea kushindwa kabisa. Kadhalika na hawa ndio wapandwao penye miamba, ambao kwamba wakiisha kulisikia lile neno, mara hulipokea kwa furaha; ila hawana mizizi ndani yao, bali hudumu muda mchache; kisha ikitokea dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara hujikwaa,” Mk 4:16-17

Adui wa tatu wa neno la Mungu ni shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine. Leo watu wengi lengo la maisha yao yote huongozwa na tamaa ya kupata vitu. Msukumo huu wa kutaka zaidi kila siku una misingi yake katika udanganyifu wa kuwa nikiwa na vingi nitakuwa na furaha zaidi, nitakuwa wa muhimu, na nitakuwa salama; lakini mawazo hayo yote matatu si ya kweli. Na hawa ndio wale wapandwao penye miiba; ni watu walisikiao lile neno, na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai,” Mk 4:18-19. Mali huleta furaha ya "muda mfupi tu." Na sababu kubwa ndugu yangu, vitu havibadiliki, hivyo vinatuchosha na tunataka vipya, vikubwa, na bora zaidi.

Kuna imani pia kwamba nitapata mali nyingi nitakuwa wa muhimu. Umuhimu wako na mali ni vitu viwili tofauti. Thamani yako haitegemei mali zako, Mungu anasema kitu cha muhimu maishani mwako si vitu! Imani ya watu wengi kuhusu fedha ni kwamba kuwa nazo nyingi kutanipa usalama. Huwezi! Yesu anawaambia wale wafuasi wa Yohane Mbatizaji, “Mnatafuta nini?” Wanafunzi wale wakamjibu,  Rabi, (maana yake, Mwalimu), unakaa wapi?” Yoh 1:38. Anapokaa Yesu ndipo kwenye usalama kupita vitu vyote na hali zote tunazoweza kufikiria. Mt. Augustino anasema, “mioyo yetu haitulii mpaka itakapotulia kwako Ee Bwana.”

Ndugu yangu, utajiri unaweza kupotezwa mara moja kwa sababu zisizozuilika. Usalama halisi unaweza kupatikana katika kile ambacho huwezi kunyang'anywa yaani uhusiano wako na Mungu. Na hawa ndio waliopandwa penye udongo ulio mzuri; ni watu walisikiao lile neno na kulipokea, na kuzaa matunda, mmoja thelathini, mmoja sitini, na mmoja mia,” Mk 4:20. Mt. Augustino anatuwasa kutoka kwenye kanuni yake, "kuna furaha kubwa kuwa na vichache kuliko kuwa na vingi." Hata hivyo tatizo hapa ni kipimo cha huo uchache na huo wingi. Uzima wetu upo katika neno la uzima nalo ndilo ngao yetu katika ulimwengu huu kigeugeu.

Usalama wa Mfalme Daudi upo katika kuujenga uhusiano mzuri na wakaribu na Mungu. Nabii Nathani anampa Mfalme Daudi ujumbe wa Mungu kuhusu hamu yake, yaani, kumjengea nyumba naye hatamwacha kamwe. Kwa maana mimi sikukaa ndani ya nyumba, tangu siku ile niliyowatoa wana wa Israeli katika Misri, hata leo, lakini nimekaa katika hema na maskani,” 2Sam 7:6. Na wakuifanya kazi hii ni Mfalme Daudi na si mwingine. Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele,” 2Sam 7:13. Ndugu yangu, yapo mambo mengi katika maisha yetu yanayofanana na hili jukumu alilopewa Mfalme Daudi. Bila shaka yoyote Kanisa letu la Tanzania leo takribani kila Parokia kuna ujenzi wa Nyumba ya Mungu au Shule. Jukumu hilo ni la kila mbatizwa pale alipo. Kwa kufanya hivyo bila kujibakiza ndivyo tunavyopewa baraka kama alivyohaidiwa Mfalme Daudi.

Shughuli hii ya kujenga Nyumba ya Mungu, yaani, Kanisa ifanywe bila malalamko na manung’uniko kwa sababu Kanisa hili ni baraka kwako kwa milele yote. Watu wataendelea kumsifu na kumwabudu Mungu vizazi na vizazi hata kama hautakuwepo tena katika ulimwengu huu. Baraka hizi hazina kipimo. Mchango wako leo katika ujenzi wa Kanisa au Shule ni hazima kubwa sana, na hasa pale unapojitoa bila kujibakiza kwa hali na mali. Haya ndiyo aliyohaidiwa Mfalme Daudi na ndiyo unayohaidiwa wewe na mimi tutakapotimiza wajibu huu muhimu wa kumjengea Mungu Nyumba-Kanisa. Lakini fadhili zangu hazitamwondoka, kama vile nilivyomwondolea Sauli, niliyemwondoa mbele yako. Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele,” 2Sam 7:15-16. Wakati ndio sasa na timiza wajibu wako huo muhimu mbele za Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo


Katika shida za moyo wangu unifanyie nafasi, Na kunitoa katika dhiki zangu,” Zab 25:17

No hay comentarios:

Publicar un comentario